Hamia kwenye habari

Je Biblia Inaruhusu Mwanamume Awe na Wake Wengi?

Je Biblia Inaruhusu Mwanamume Awe na Wake Wengi?

Jibu la Biblia

 Kwa muda fulani, Mungu aliruhusu mwanamume awe na wake wengi. (Mwanzo 4:19; 16:1-4; 29:18–29) Lakini Mungu hakuanzisha mpango wa mwanamume kuwa na wake wengi. Alimpa Adamu mke mmoja tu.

 Mungu alimwagiza Yesu Kristo akazie mpango aliokuwa ameanzisha awali wa mwanamume kuwa na mke mmoja. (Yohana 8:28) Yesu alipoulizwa kuhusu ndoa, alisema hivi: “Yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.”—Mathayo 19:4, 5.

 Baadaye, mmoja kati ya wanafunzi wa Yesu aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe na kila mwanamke awe na mume wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 7:2) Pia, Biblia inasema kwamba katika kutaniko la Kikristo ni lazima mwanamume aliyefunga ndoa na ambaye ana majukumu ya pekee awe “mume wa mke mmoja.”—1 Timotheo 3:2, 12.