Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Ufunuo 21:1—“Mbingu Mpya na Dunia Mpya”

Ufunuo 21:1—“Mbingu Mpya na Dunia Mpya”

 “Nami nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali, na bahari haipo tena.”​—Ufunuo 21:1, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Kisha, nikaona mbingu mpya na dunia mpya. Mbingu ile ya kwanza na dunia ile ya kwanza vilikuwa vimetoweka, nayo bahari pia haikuwako tena.”​—Ufunuo 21:1, Biblia Habari Njema.

Maana ya Ufunuo 21:1

 Mstari huu unatumia lugha ya mfano kutangaza kwamba Ufalme wa mbinguni wa Mungu utachukua mahali pa serikali zote za wanadamu. Ufalme huo utawaondoa wanadamu waovu na kutawala juu ya jamii mpya ya watu wanaojitiisha kwa hiari kwa mamlaka yake.

 Kitabu cha Ufunuo kimetolewa kupitia “ishara.” (Ufunuo 1:1) Kwa hiyo inapatana na akili kusema kwamba mbingu na dunia zinazotajwa katika mstari huu si halisi bali ni za mfano. Zaidi ya hilo, “mbingu mpya” na “dunia mpya” za mfano zinatajwa katika mistari mingine ya Biblia pia. (Isaya 65:17; 66:22; 2 Petro 3:13) Kuchunguza mistari hiyo pamoja na masimulizi mengine ya Kimaandiko kunatusaidia kuelewa maana yake.

 “Mbingu mpya.” Nyakati nyingine Biblia hutumia neno “mbingu” kuwakilisha utawala au serikali. (Isaya 14:12-14; Danieli 4:25, 26) Hivyo, kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba katika maono ya kinabii, “kwa njia ya mfano mbingu zinawakilisha mamlaka ya kutawala au serikali.” a Katika Ufunuo 21:1, ni wazi kwamba “mbingu mpya” inarejelea Ufalme wa Mungu. Serikali hiyo ya mbinguni, ambayo nyakati nyingine huitwa “Ufalme wa mbinguni,” inatajwa kotekote katika Ufunuo na katika vitabu vingine vya Biblia. (Mathayo 4:17; Matendo 19:8; 2 Timotheo 4:18; Ufunuo 1:9; 5:10; 11:15; 12:10) Ufalme wa Mungu, ambao Mfalme wake ni Yesu, hatimaye utachukua mahali pa “mbingu ya kwanza,” yaani, serikali zote zisizo kamilifu za wanadamu.​—Danieli 2:44; Luka 1:31-33; Ufunuo 19:11-18.

 “Dunia mpya.” Biblia inasema kwamba dunia halisi haitawahi kuharibiwa wala kubadilishwa. (Zaburi 104:5; Mhubiri 1:4) Basi dunia ya mfano ni ipi? Mara nyingi Biblia hutumia neno “dunia” kurejelea wanadamu. (Mwanzo 11:1; 1 Mambo ya Nyakati 16:31; Zaburi 66:4; 96:1) Hivyo, lazima iwe “dunia mpya” inarejelea jamii mpya ya wanadamu wanaojitiisha kwa hiari kwa ufalme wa mbinguni wa Mungu. “Dunia ya kwanza,” au jamii ya wanadamu inayoupinga Ufalme wa Mungu, itapitilia mbali.

 “Bahari haipo tena.” Kama tu ilivyo na sehemu nyingine za Ufunuo 21:1, “bahari” hii ni ya mfano pia. Bahari hiyo, ambayo inachafuka kwa urahisi na mara nyingi inakuwa na dhoruba, inawakilisha wanadamu wenye msukosuko waliotengwa na Mungu. (Isaya 17:12, 13; 57:20; Ufunuo 17:1, 15) Wao pia wataondolewa kabisa. Zaburi 37:10 inasema: “Bado muda mfupi tu, na watu waovu hawatakuwepo tena; utapaangalia mahali walipokuwa, nao hawatakuwepo.”

Muktadha wa Ufunuo 21:1

 Kitabu cha Ufunuo kinatabiri mambo yanayotokea katika “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10) Kulingana na unabii wa Biblia, siku hiyo ilianza mwaka wa 1914 wakati ambapo Yesu alianza kutawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. b Lakini hangeanza kuitawala dunia kikamili mara moja. Kwa kweli, unabii mwingine unasema kwamba hali za ulimwengu zingeharibika sana wakati wa sehemu ya kwanza ya “siku ya Bwana.” Kipindi hicho cha kwanza kinaitwa “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5, 13; Mathayo 24:3, 7; Ufunuo 6:1-8; 12:12) Siku hizo za hatari na zilizojaa taabu zitakapokwisha, Ufalme wa Mungu utaondoa mbingu na dunia za zamani za mfano na kuleta kipindi kipya cha amani na upatano. Raia wa Ufalme huo—“dunia mpya”​—watafurahia kuishi katika hali nzuri kabisa na afya kamilifu.​—Ufunuo 21:3, 4.

 Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Ufunuo.

a McClintock and Strong’s Cyclopedia (1891), Buku la 4, ukurasa wa 122.