Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Waebrania 11:1​—“Imani Ni Kuwa na Hakika ya Mambo Yatarajiwayo”

Waebrania 11:1​—“Imani Ni Kuwa na Hakika ya Mambo Yatarajiwayo”

 “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ambayo hayaonekani.”—Waebrania 11:1, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana.”—Waebrania 11:1, Union Version.

Maana ya Waebrania 11:1

 Mstari huu unaonyesha maana halisi ya neno imani na kwamba linamaanisha mengi zaidi ya kuamini tu.

 “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa.” Katika maandishi ya lugha ya awali ya Kigiriki ya andiko la Waebrania 11:1, neno “imani” linatokeza wazo la mtu kuwa na uhakika, tumaini, au usadikisho kamili. Imani ya aina hiyo haitegemei yale tunayotamani yatendeke bali inategemea “tarajio lililohakikishwa.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “tarajio lililohakikishwa” a linaweza pia kutafsiriwa kuwa “hati miliki,” ikirejelea uthibitisho unaomsadikisha, au kumhakikishia, mmiliki uhalali wa hati hiyo.

 “Imani ni . . . uthibitisho ulio wazi [au “uthibitisho wenye kuridhisha,” maelezo ya chini] wa mambo halisi ambayo hayaonekani.” Imani inategemea uthibitisho hakika. Uthibitisho huo ni wenye nguvu sana hivi kwamba unamsadikisha mtu kwamba hata kama hawezi kuona kinachozungumziwa, jambo hilo ni hakika.

Muktadha wa Waebrania 11:1

 Kitabu cha Waebrania ni barua ambayo Paulo aliwaandikia Wakristo wa karne ya kwanza walioishi ndani na karibu na Yerusalemu. Paulo anazungumzia umuhimu wa imani katika sehemu hii ya barua yake. Kwa mfano anaandika hivi: “Bila imani haiwezekani kumpendeza Mungu vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kuwa yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Baada ya kufafanua imani katika Waebrania 11:1, Paulo anatoa mifano ya wanaume na wanawake katika Biblia walioonyesha sifa hii. Anasimulia jinsi walivyoonyesha imani kwa kutenda kulingana na mapenzi ya Mungu.—Waebrania 11:4-38.

a Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “tarajio lililohakikishwa” katika muktadha huu ni hy·poʹsta·sis, ambalo linaweza kutafsiriwa neno kwa neno kuwa “kile kinachoshikilia msingi.” Katika Kilatini, neno hili linatafsiriwa kuwa sub·stanʹti·a, na limetumiwa katika tafsiri ya King James Version ya Kiingereza kuwa“substance,” neno linalomaanisha sehemu ya msingi inayofanyiza kitu.