Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tunateseka, Tunazeeka, na Kufa?

Kwa Nini Tunateseka, Tunazeeka, na Kufa?

Muumba wetu anatuona sisi kama watoto wake. Kwa hiyo, hataki tuteseke. Lakini, leo watu wanateseka sana. Kwa nini?

Wazazi Wetu wa Kwanza Wamesababisha Tuteseke

“Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, basi kifo kikaenea kwa watu wote.”​​—WAROMA 5:12.

Mungu aliwaumba wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, wakiwa na miili na akili kamilifu. Pia, aliwaweka waishi kwenye paradiso, yaani, bustani maridadi iliyoitwa Edeni. Aliwaambia wanaweza kula matunda ya miti yote lakini wasile matunda ya mti mmoja. Hata hivyo, Adamu na Hawa waliamua kula matunda ya mti ambao Mungu aliwakataza, na hiyo ilikuwa dhambi. (Mwanzo 2:15-17; 3:1-19) Baada ya uasi huo, Mungu aliwafukuza kutoka kwenye bustani hiyo, na wakawa na maisha magumu. Baada ya muda, wakapata watoto na maisha ya watoto hao yakawa magumu pia. Wote walizeeka na kufa. (Mwanzo 3:23; 5:5) Tunakuwa wagonjwa, tunazeeka na kufa kwa sababu sisi sote ni wazao wa Adamu na Hawa.

Tunateseka kwa Sababu ya Roho Waovu

“Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”​​—1 YOHANA 5:19.

“Yule mwovu” ni Shetani. Ni malaika ambaye alimwasi Mungu. (Yohana 8:44; Ufunuo 12:9) Baada ya muda, malaika wengine walijiunga naye na kuwa waasi. Malaika hao wanaitwa roho waovu. Roho hao waovu wanatumia nguvu zao kuwadanganya watu ili wasimtii Muumba wao. Wanawaongoza watu wengi kufanya mambo mabaya. (Zaburi 106:35-38; 1 Timotheo 4:1) Shetani na roho waovu wanafurahia kuwasababishia watu maumivu na mateso.

Wakati Mwingine Tunateseka kwa Sababu ya Kufanya Maamuzi Mabaya

“Lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.”​​—WAGALATIA 6:7.

Tunateseka kwa njia mbalimbali kwa sababu ya dhambi tuliyorithi au kwa sababu tunaishi katika ulimwengu unaoongozwa na Shetani. Lakini, wakati mwingine tunajisababishia mateso. Jinsi gani? Tukifanya mambo mabaya au maamuzi mabaya, tunapata matokeo mabaya pia. Kwa upande mwingine, tunapofanya mambo mazuri, tunapata matokeo mazuri. Kwa mfano, mume ambaye pia ni baba anapokuwa mnyoofu, anapofanya kazi kwa bidii, na kuipenda familia yake anapata vitu vingi vizuri na kufanya familia yake iwe na furaha. Lakini mume anayecheza kamari, mlevi au mvivu anaweza kufanya familia yake iwe maskini. Hivyo, ni jambo la hekima kumsikiliza Muumba wetu. Anataka tupate mambo mengi mazuri, kutia ndani “amani nyingi.”—Zaburi 119:165.

Tunateseka kwa Sababu Tunaishi Katika “Siku za Mwisho”

“Katika siku za mwisho . . . , watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiotii wazazi, . . . wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema.”​​—2 TIMOTHEO 3:1-5.

Leo, watu wengi wana tabia hizo ambazo zilitabiriwa kwenye andiko hilo. Tabia hizo zinatuthibitishia kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” Maandiko pia yalitabiri kwamba katika siku zetu kungekuwa na vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, na magonjwa. (Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:10, 11) Mambo hayo yanafanya tuteseke na tupatwe na kifo.