Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | KWA NINI WATU WAZURI HUPATWA NA MAMBO MABAYA?

Kwa Nini Watu Wazuri Hupatwa na Mambo Mabaya?

Kwa Nini Watu Wazuri Hupatwa na Mambo Mabaya?

Kwa kuwa Yehova Mungu * ndiye Muumba wa vitu vyote na ni mweza-yote, huenda wengi wakadhani kwamba yeye ndiye anayesababisha mambo yote ulimwenguni, kutia ndani mambo mabaya. Hata hivyo, ona yale ambayo Biblia inasema kumhusu Mungu wa kweli:

  •  “Yehova ni mwadilifu katika njia zake zote.”Zaburi 145:17.

  • “Njia zake [za Mungu] zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.”Kumbukumbu la Torati 32:4.

  • “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.”Yakobo 5:11.

Mungu hasababishi mambo mabaya. Hata hivyo, je, anawachochea watu watende mabaya? La hasha. Maandiko yanasema: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’” Kwa nini? Kwa sababu, “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Mungu hamjaribu wala kumshawishi yeyote afanye mabaya. Kwa hiyo, Mungu hasababishi mambo mabaya wala hawachochei watu wafanye mabaya. Basi, ni nini, au ni nani anayesababisha mambo mabaya?

KUWA MAHALI PASIPOFAA WAKATI USIOFAA

Biblia inataja kisababishi kimoja cha mateso yanayotupata inaposema: “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Mhubiri 9:11) Matukio au misiba isiyotazamiwa inapotokea, iwe mtu ataathiriwa au la, itategemea hasa mahali alipo mambo hayo yanapotokea. Miaka 2,000 hivi iliyopita, Yesu Kristo alitaja msiba wa mnara ulioanguka na kuwaua watu 18. (Luka 13:1-5) Hawakufa kwa sababu ya mambo waliyokuwa wamefanya maishani; badala yake walikufa kwa sababu walikuwa chini ya mnara ulipoanguka. Hivi karibuni, Januari 2010 tetemeko kubwa la ardhi lilitokea huko Haiti; na serikali ya Haiti ilisema kwamba zaidi ya watu 300,000 walikufa. Tetemeko hilo liliua watu bila kuchagua, wazuri na wabaya. Ugonjwa pia unaweza kumpata mtu yeyote wakati wowote.

Kwa nini Mungu hazuii watu wazuri wasipatwe na misiba?

Huenda wengine wakauliza: ‘Je, Mungu hangeweza kuzuia misiba hiyo mibaya isitokee? Je, hangewakinga watu wazuri wasipatwe na misiba?’ Ili Mungu azuie misiba kama hiyo, ingemaanisha kwamba anajua mambo mabaya kabla hayajatukia. Kwa kweli Mungu ana uwezo wa kujua yatakayotukia wakati ujao, lakini tunapaswa kujiuliza: Je, Mungu huamua kuchunguza kila jambo litakalotokea wakati ujao?Isaya 42:9.

Maandiko husema: “Mungu wetu yuko mbinguni; kila kitu ambacho alipendezwa kufanya, amekifanya.” (Zaburi 115:3) Yehova hufanya chochote kile anachoona ni muhimu, bali hafanyi kila kitu anachoweza kufanya. Ndivyo ilivyo pia anapoamua kuchunguza wakati ujao. Kwa mfano, baada ya uovu kuenea katika majiji ya kale ya Sodoma na Gomora, Mungu alimwambia Abrahamu hivi: “Nimeazimia kabisa kushuka ili nipate kuona kama wanatenda kabisa kulingana na kile kilio kilicho juu yake ambacho kimenifikia, na ikiwa sivyo, nitajua.” (Mwanzo 18:20, 21) Kwa muda fulani Yehova aliamua kutochunguza jinsi uovu ulivyokuwa umeenea katika majiji hayo. Vivyo hivyo, Yehova anaweza kuamua anachotaka kujua kuhusiana na wakati ujao. (Mwanzo 22:12) Hilo halionyeshi kwa vyovyote kwamba Mungu si mkamilifu au kwamba yeye ni dhaifu. Kwa kuwa “kazi zake ni kamilifu,” Mungu husawazisha kati ya kujua mambo yatakayotukia na kusudi lake; na hawalazimishi kamwe wanadamu watende kwa njia fulani. * (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kwa hiyo, tunafikia mkataa gani? Kwa ufupi: Kwa busara Mungu huamua kuchunguza mambo anayotaka kujua kuhusiana na wakati ujao.

Kwa nini Mungu hawalindi watu wazuri kutokana na uhalifu?

JE, WANADAMU NDIO WANAOSABABISHA?

Kwa kadiri fulani wanadamu ndio wanaosababisha uovu. Hebu ona jinsi Biblia inavyofafanua hatua zinazomwongoza mtu kutenda uovu. “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.” (Yakobo 1:14, 15) Wanadamu wanaposhawishiwa kutenda uovu au kutosheleza tamaa mbaya lazima wapatwe na matatizo. (Waroma 7:21-23) Historia inaonyesha kwamba wanadamu wametenda kikatili sana na kusababisha mateso mengi. Isitoshe, watu waovu huwashawishi watu wawe wapotovu na hivyo kusababisha mambo mabaya.—Methali 1:10-16.

Wanadamu wametenda kikatili sana na kusababisha mateso mengi

Je, Mungu anapaswa kuingilia kati na kuwazuia watu wasifanye mabaya? Hebu fikiria jinsi mwanadamu alivyoumbwa. Maandiko yanasema kwamba mwanadamu aliumbwa kwa mfano wa Mungu. Basi, wanadamu wana uwezo wa kuonyesha sifa kama za Mungu. (Mwanzo 1:26) Wanadamu wamepewa uhuru wa kujiamulia na wanaweza kuchagua kumpenda Mungu na kuwa washikamanifu kwake kwa kufanya mambo yanayompendeza. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Ikiwa Mungu angewalazimisha watu kutenda kwa njia fulani, je hangekuwa akiingilia uhuru wao wa kujiamulia? Kwa kufanya hivyo, wanadamu wangekuwa tu kama mashine zinazofanya kama zilivyoratibiwa! Ingekuwa hivyo pia ikiwa matendo yetu au mambo yote yanayotupata yangeongozwa na bahati, au majaliwa. Tunathamini sana kwamba Mungu anatuheshimu kwa kuturuhusu tujiamulie tutakachofanya! Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba wanadamu wataendelea kuteseka kwa sababu ya makosa na uamuzi mbaya wanaofanya.

JE, SHERIA YA KARMA NDIYO KISABABISHI?

Kama ungemuuliza Mhindu au Mbudha swali lililo kwenye ukurasa wa kwanza wa gazeti hili, labda angejibu hivi: “Mambo mabaya huwapata watu wazuri kwa sababu ya sheria ya Karma. Wanavuna matokeo ya mambo waliyofanya katika maisha yaliyotangulia.” *

Tunapozungumzia fundisho la Karma ni vizuri tuchunguze kila ambacho Biblia inasema kuhusu kifo. Katika bustani ya Edeni, ambapo wanadamu walianzia, Muumba alimwambia hivi mwanamume wa kwanza Adamu: “Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Kama Adamu hangefanya dhambi kwa kumwasi Mungu, angeishi milele. Kifo kilikuwa adhabu ya kutotii amri ya Mungu. Kisha, watoto walipozaliwa, “kifo kikaenea kwa watu wote.” (Waroma 5:12) Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Pia, Biblia inaeleza hivi: “Yeye ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.” (Waroma 6:7) Yaani, watu hawaendelei kulipia dhambi zao baada ya kufa.

Leo, mamilioni ya watu hudhani kwamba matatizo ya wanadamu yanahusiana na sheria ya Karma. Mtu anayeamini sheria hiyo hukubali mateso yanayompata na yale yanayowapata wengine bila kusumbuka. Lakini ukweli ni kwamba imani hiyo haitoi tumaini lolote kuhusu mwisho wa mateso. Inaaminiwa kwamba kitulizo pekee ambacho mtu hupata ni kuzaliwa upya kupitia ujuzi wa kipekee na tabia zinazokubalika katika jamii. Hata hivyo, maoni hayo ni tofauti kabisa na mafundisho ya Biblia. *

CHANZO KIKUU CHA KUTESEKA!

Je, unajua kwamba chanzo kikuu cha mateso ni “mtawala wa ulimwengu”—Shetani Ibilisi?Yohana 14:30

Hata hivyo, chanzo kikuu cha uovu si mwanadamu. Shetani Ibilisi, ambaye mwanzoni alikuwa malaika mwaminifu wa Mungu, “hakusimama imara katika kweli” na akaleta dhambi ulimwenguni. (Yohana 8:44) Alichochea uasi katika bustani ya Edeni. (Mwanzo 3:1-5) Yesu Kristo alimwita “yule mwovu” na “mtawala wa ulimwengu.” (Mathayo 6:13; Yohana 14:30) Wanadamu wengi humfuata Shetani kwa kukubali awashawishi kupuuza mwongozo unaofaa wa Yehova. (1 Yohana 2:15, 16) “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” linasema andiko la 1 Yohana 5:19. Viumbe wengine wa roho ambao ni waovu wamejiunga pia na Shetani. Biblia inaonyesha kwamba Shetani na roho waovu “[wana]ipotosha dunia nzima inayokaliwa” na kusababisha “ole [kwa] dunia.” (Ufunuo 12:9, 12) Kwa hiyo, Shetani Ibilisi ndiye kisababishi kikuu cha uovu.

Ni wazi kwamba Mungu hasababishi mambo mabaya yanayowapata watu; wala hasababishi mateso. Kinyume chake, ameahidi kuondoa uovu, kama makala inayofuata itakavyoonyesha.

^ fu. 3 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.

^ fu. 11 Ili ujue kinachofanya Mungu aruhusu uovu uendelee, soma sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 16 Ili ujifunze mengi kuhusu chanzo cha sheria inayoitwa Karma, soma ukurasa wa 8-12 wa broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 18 Ili ujue Biblia inafundisha nini kuhusu hali ya wafu na tumaini la wafu, soma sura ya 6 na 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?