Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inatufundisha Nini?

Biblia Inatufundisha Nini?

“Hii ndiyo historia ya mbingu na dunia wakati zilipoumbwa.” (Mwanzo 2:4) Kwa maneno hayo, Biblia inaeleza kwa ufupi jinsi sayari yetu ilivyotokea. Je, mambo ambayo Biblia inasema yanapatana na ukweli wa kisayansi? Fikiria mifano hii michache.

Mwanzo: Mbingu na dunia zinaumbwa

Je, ulimwengu umekuwepo sikuzote?

Mwanzo 1:1 inasema: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”

Mpaka kufikia katikati ya karne ya 20, wanasayansi wengi mashuhuri waliamini kwamba ulimwengu umekuwepo sikuzote. Lakini kwa kutegemea uvumbuzi wa hivi karibuni, wanasayansi wengi sasa wanakubali kwamba ulimwengu una mwanzo.

Dunia ilikuwaje mwanzoni?

Mwanzo 1:2, 9 inasema mwanzoni dunia “haikuwa na umbo nayo ilikuwa tupu,” ikiwa imefunikwa na maji.

Maneno hayo yanapatana na utafiti wa hivi karibuni wa kisayansi. Mtaalamu wa biolojia, Patrick Shih, anasema kwamba sayari yetu ilianza ikiwa na “anga lisilo na hewa ya oksijeni . . . na ilikuwa na ardhi yenye mwonekano wa ajabu.” Gazeti la Astronomy linaripoti hivi: “Utafiti mpya unaonyesha kwamba zamani dunia yote ilikuwa imejaa maji na ilikuwa na sehemu ndogo sana ya ardhi iliyoonekana.”

Baada ya muda, angahewa lilibadilikaje?

Mwanzo 1:3-5 inaonyesha kwamba mwanga ulipoanza kupenya angahewa, chanzo chake hakingeweza kuonekana duniani. Ni baada ya muda fulani kupita, ndipo mwezi na jua vingeweza kuonekana kutoka duniani.—Mwanzo 1:14-18.

Biblia haisemi kwamba viumbe hai vyote duniani viliumbwa kwa siku sita zenye saa 24.

Kituo kimoja cha utafiti (Smithsonian Environmental Research Center) kinasema kwamba mwanzoni angahewa la sayari yetu liliruhusu kiwango kidogo sana cha mwanga kifike duniani. Watafiti hao wanasema: “Ukungu mzito wa gesi ya Methani uliifunika dunia nzima.” Baadaye, “ukungu huo wa gesi ya methani ukaondoka na anga likawa la bluu.”

Viumbe wa duniani waliumbwa kwa mpangilio gani?

Mwanzo 1:20-27 inaeleza kwamba samaki walianza kuumbwa, wakafuata ndege, kisha wanyama na mwishowe wanadamu. Wanasayansi wanaamini kwamba samaki wa kwanza walitokea muda mrefu kabla ya wanyama wa kwanza, na kwamba wanadamu walitokea muda mrefu baadaye.

Biblia haisemi kwamba haiwezekani kwa viumbe hai kubadilika baada ya muda fulani kupita

Mambo Ambayo Biblia Haifundishi

Baadhi ya watu wanadai kwamba Biblia haipatani na utafiti wa kisasa wa kisayansi. Hata hivyo, mara nyingi wanatoa madai hayo kwa sababu hawaelewi mambo ambayo Biblia inafundisha.

Biblia haisemi kwamba ulimwengu au dunia imekuwepo kwa miaka 6,000 tu. Badala yake, inasema kwamba dunia na ulimwengu uliumbwa “hapo mwanzo.” (Mwanzo 1:1) Biblia haielezi kihususa muda ambao dunia na ulimwengu umekuwepo.

Biblia haisemi kwamba viumbe hai vyote duniani viliumbwa kwa siku sita zenye saa 24. Badala yake inatumia neno “siku” kurejelea kipindi fulani cha wakati. Kwa mfano, inasema kwamba uumbaji wa sayari yetu na viumbe hai​—katika zile siku sita za uumbaji zinazotajwa kwenye Mwanzo sura ya kwanza—​ulitokea katika kipindi cha wakati kinachoitwa “siku ambayo Yehova * Mungu aliumba dunia na mbingu.” (Mwanzo 2:4) Hivyo, kila siku moja kati ya zile siku sita ambazo Mungu alitumia kuandaa dunia na kuumba viumbe hai, inaweza kuwakilisha kipindi kirefu sana cha wakati.

Biblia haisemi kwamba haiwezekani kwa viumbe hai kubadilika baada ya muda fulani kupita. Kitabu cha Mwanzo kinasema kwamba wanyama waliumbwa “kulingana na aina zao.” (Mwanzo 1:24, 25) Neno “aina” linalotajwa katika Biblia si la kisayansi, lakini inaonekana linarejelea makundi mbalimbali makubwa ya viumbe hai. Hivyo, “aina” moja inaweza kutia ndani jamii nyingi, mbalimbali, za wanyama au mimea yenye tabia fulani zinazofanana. Ufafanuzi huu unaonyesha kwamba inawezekana mabadiliko yalitokea kati ya wanyama au mimea mbalimbali iliyo katika “aina” moja na iliyokuwa katika eneo lilelile.

Una maoni gani?

Kama tulivyoona, Biblia inafafanua kwa njia rahisi na iliyo sahihi mwanzo wa ulimwengu, jinsi dunia ilivyoonekana mwanzoni, na jinsi viumbe hai walivyotokea. Je, inawezekana pia Biblia imemtambulisha kwa usahihi Yule aliyeumba vitu hivyo vyote? Encyclopædia Britannica inasema: “Kwa ujumla, wazo la kwamba uhai ulitokana na chanzo fulani chenye nguvu zinazopita za wanadamu halipingani na uvumbuzi wa kisasa wa kisayansi.” *

^ fu. 17 Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa kwenye Biblia.

^ fu. 20 Encyclopædia Britannica haisemi kwamba viumbe hai viliumbwa.