Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu Unatufundisha Nini?

Ulimwengu Unatufundisha Nini?

Ulimwengu unaendelea kuwashangaza wataalamu wa nyota. Na bado wanaendelea kubuni vifaa bora zaidi vya kuwasaidia kuuchunguza. Wamegundua nini?

Ulimwengu Una Mpangilio Mzuri. Makala moja katika gazeti la elimu ya nyota inasema: “Makundi ya nyota hayajasambaa kiholela angani, badala yake, yamekaa katika mpangilio mzuri sana unaofanana na utando wa buibui.” Hilo linawezekanaje? Wanasayansi wanaamini kwamba siri ya mpangilio huo ni vitu fulani visivyoonekana kwa macho ya binadamu vinavyoitwa mata nyeusi. Watu wengine wamesema kwamba mata nyeusi ni kama “jukwaa lisiloonekana ambapo . . . makundi ya nyota, na makundi ya makundi makubwa zaidi ya nyota . . . yamejipanga na kushikiliwa.”

Inawezekanaje kwamba ulimwengu una mpangilio mzuri hivi? Je, mpangilio huo ulijitokeza wenyewe tu? Fikiria maelezo yaliyotolewa na mwanamume aliyeitwa Allan Sandage. Alijulikana kama “mmoja kati ya wataalamu bora zaidi wa nyota waliokuwa na ushawishi mkubwa zaidi katika karne ya 20,” na ambaye aliamini kwamba kuna Mungu.

Alisema: “Ninaona kwamba haiwezekani mpangilio mzuri kama huo ujitokeze wenyewe tu bila utaratibu wowote. Lazima kuna kanuni fulani ya mpangilio iliyohusika.”

Kila kitu ulimwenguni kiko katika njia sahihi kabisa inayotegemeza uhai. Fikiria kile ambacho wanasayansi wanakiita nguvu dhaifu. Nguvu hiyo inafanya jua liendelee kuwaka kwa kiwango kilekile. Ikiwa nguvu hiyo ingekuwa ndogo zaidi, jua lisingekuwepo. Ikiwa nguvu hiyo ingekuwa kubwa zaidi, jua lingekuwa limeteketea muda mrefu uliopita.

Nguvu dhaifu ni mojawapo ya vitu vilivyo katika kiwango sahihi kabisa ili kutegemeza uhai. Mwandishi wa sayansi Anil Ananthaswamy anasema kwamba ikiwa mojawapo ya vitu hivyo ingekuwa tofauti, “nyota, sayari, na makundi ya nyota yasingekuwepo. Uhai usingekuwepo.”

Ulimwengu una eneo bora ambalo wanadamu wanaweza kuishi. Dunia yetu ina anga hewa linalofaa, kiwango sahihi cha maji, na mwezi wenye ukubwa unaofaa kabisa ili kuhakikisha dunia yetu ina usawaziko. Jarida la National Geographic linasema, “Muundo wa dunia, mazingira yake, na viumbe hai waliomo, hufanya jiwe hili la ajabu [dunia] kuwa sehemu pekee tunayoitambua kwa sasa ambayo wanadamu wanaweza kuishi.” *

Mwandishi mmoja alisema mfumo wetu wa jua, “uko mbali na nyota nyingine” katika kundi letu la nyota. Lakini, kujitenga huko ndiko kunakofanya uhai uwepo duniani. Ikiwa tungeishi karibu na nyota nyingine, yaani, katikati ya kundi letu la nyota au pembeni, mionzi hatari ingekuwa tishio kwa uhai wetu. Badala yake, tumejikuta katika eneo ambalo baadhi ya wanasayansi wanasema ndio “eneo pekee linaloweza kutegemeza uhai katika kundi letu la nyota.”

Kwa kutegemea ujuzi huu wa kisayansi kuhusu ulimwengu na sheria zake, mtaalamu wa fizikia, Paul Davies, alifikia mkataa huu: “Siamini kwamba ulimwengu wetu ulijitokeza tu wenyewe bila kutarajiwa, bila mpangilio wowote, au kwa sababu ya mvurugiko fulani. . . . Bila shaka kuna sababu ya kuwa hapa.” Davies hafundishi kwamba Mungu aliumba ulimwengu na wanadamu, lakini wewe una maoni gani? Inaonekana ulimwengu na dunia ilibuniwa kwa njia ambayo inategemeza uhai. Je, inawezekana kwamba ulimwengu na dunia iko hivyo kwa sababu ilibuniwa?

^ fu. 8 Makala hii ya National Geographic haikukusudiwa itoe wazo kwamba Mungu aliumba dunia na wanadamu. Badala yake, inakazia wazo kwamba dunia ni mahali panapofaa kwa wanadamu kuishi.