Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini andiko la 2 Samweli 21:7-9 linasema kwamba Daudi ‘alimhurumia Mefiboshethi’ na kisha akaruhusu Mefiboshethi auawe?

Baadhi ya watu wanaosoma simulizi hilo haraka-haraka wamejiuliza swali hilo. Lakini mistari hiyo inazungumzia wanaume wawili walioitwa Mefiboshethi, na tunaweza kujifunza jambo fulani kuhusu kilichotokea.

Mfalme Sauli wa Israeli alikuwa na wana saba na binti wawili. Mwana wa kwanza wa Sauli alikuwa Yonathani. Baadaye, mfalme alipata mwana aliyeitwa Mefiboshethi, aliyemzaa na suria aliyeitwa Rispa. Inashangaza kwamba Yonathani pia alikuwa na mwana aliyeitwa Mefiboshethi. Hivyo, Mfalme Sauli alikuwa na mwana aliyeitwa Mefiboshethi, na mjukuu aliyeitwa jina hilo pia.

Pindi fulani, Mfalme Sauli alianza kuwashambulia Wagibeoni walioishi miongoni mwa Waisraeli na alitaka kuwaangamiza. Inaonekana baadhi yao waliuawa. Ni wazi kwamba hilo lilikuwa kosa. Kwa nini? Kwa sababu katika siku za Yoshua, wakuu wa Israeli walikuwa wamefanya agano la amani pamoja na Wagibeoni.​—Yos. 9:3-27.

Bado agano hilo lilikuwa linaendelea katika siku za Mfalme Sauli. Mfalme alitenda kinyume na agano hilo kwa kujaribu kuwaangamiza Wagibeoni. Shambulizi hilo lilitokeza ‘hatia ya damu juu ya Sauli na nyumba yake.’ (2 Sam. 21:1) Hatimaye, Daudi akawa mfalme. Wagibeoni waliookoka walimwambia kuhusu kosa hilo baya. Daudi aliwauliza jinsi ambavyo kosa hilo zito la Sauli lingeweza kufunikwa na hivyo kufungua njia ili Yehova abariki nchi yao. Badala ya kuomba pesa, Wagibeoni waliomba wana saba wa mwanamume ambaye “alipanga njama ya kuwaangamiza” wauawe. (Hes. 35:30, 31) Daudi alikubali ombi lao.​—2 Sam. 21:2-6.

Wakati huo, Sauli na Yonathani walikuwa wamekufa vitani, lakini Mefiboshethi, mwana wa Yonathani alikuwa hai. Alipata ulemavu utotoni kutokana na tukio ambalo halikuhusiana na shambulizi la babu yake dhidi ya Wagibeoni. Daudi alikuwa amefanya agano la urafiki pamoja na Yonathani, ambalo lingewanufaisha wazao wao, kutia ndani Mefiboshethi, mwana wa Yonathani. (1 Sam. 18:1; 20:42) Simulizi hilo linasema: “Mfalme [Daudi] akamhurumia Mefiboshethi, mwana wa Yonathani mwana wa Sauli, kwa sababu ya kiapo ambacho Daudi na Yonathani mwana wa Sauli walikuwa wameapiana mbele za Yehova.”​—2 Sam. 21:7.

Hata hivyo, Daudi alikubali kutimiza ombi la Wagibeoni. Akawapa Wagibeoni wana wawili wa Sauli, ambao mmoja wao aliitwa Mefiboshethi, na wajukuu watano wa Sauli. (2 Sam. 21:8, 9) Hatua hiyo ambayo Daudi alichukua iliondoa hatia ya damu katika nchi.

Tunaweza kujifunza mengi kutokana na simulizi hilo. Sheria ya Mungu iko wazi. Ilisema hivi: “Wana hawapaswi kuuawa kwa sababu ya dhambi za baba zao.” (Kum. 24:16) Yehova hangeruhusu jambo lililowapata wana wawili na wajukuu watano wa Sauli litokee ikiwa hawangekuwa na hatia. Sheria hiyo iliongeza hivi: “Mtu anapaswa kuuawa kwa sababu ya dhambi yake mwenyewe.” Inaonekana kwamba wazao saba wa Sauli waliokufa, walikuwa wameshiriki kwa njia fulani katika jaribio la Sauli la kuwaangamiza Wagibeoni. Matokeo ni kwamba wote saba walikufa kwa sababu ya makosa yao.

Simulizi hili linaonyesha kwamba mtu hawezi kujitetea anapofanya kosa kwa kufikiri au kusema kwamba alikuwa anafuata maagizo. Methali moja yenye hekima inasema hivi: “Lainisha mapito ya miguu yako, na njia zako zote zitakuwa thabiti.”​—Met. 4:24-27; Efe. 5:15.