Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Pesa Zinakutawala au Unazitawala?

Je, Pesa Zinakutawala au Unazitawala?

JE, UNA ugonjwa wa pesa? Inaripotiwa kwamba ugonjwa huo unawaathiri watu wengi sana ulimwenguni. Ugonjwa huo unahusisha nini?

Hivi karibuni Dakt. Roger Henderson, mchunguzi wa magonjwa ya akili huko Uingereza, alibuni jina “ugonjwa wa pesa” ili kufafanua dalili za kimwili na kiakili zinazowapata watu ambao wanafadhaishwa na mahangaiko ya pesa. Dalili hizo zinatia ndani kuishiwa na pumzi, kuumwa na kichwa, kichefuchefu, vipele mwilini, kukosa hamu ya kula, kukasirika bila sababu, woga, na mtazamo usiofaa. “Mahangaiko ya pesa ni kisababishi kikubwa cha mfadhaiko,” anaripoti Henderson.

Hatupaswi kushangazwa kwamba katika miezi ya karibuni watu wengi zaidi wameathiriwa na mahangaiko ya pesa. Matatizo ya kifedha ya sasa katika nchi nyingi yamesababisha watu kupoteza kazi, makao, na akiba zao ulimwenguni pote. Mashirika makubwa ya kifedha yameanguka, na hata mataifa tajiri zaidi yamechukua hatua za dharura ili kuepuka kuangamia kabisa kifedha. Pia katika nchi zinazoendelea, kupanda kwa bei ya chakula na mahitaji mengine ya msingi kumesababisha mahangaiko mengi sana.

Hata wakati watu wana pesa nyingi mahangaiko kuhusu pesa hayaishi. Katika miaka ya karibuni watu walipoanza kusitawi kiuchumi, watu wengi sana walipatwa na mahangaiko kuhusu pesa. Kwa mfano, gazeti la Afrika Kusini linaloitwa The Witness, liliripoti kwamba barani Afrika, “ugonjwa unaenea katika jamii wa kununua vitu kupita kiasi, kuhangaikia sana kupata faida za kifedha, na ufuatiliaji wa vitu vya kimwili.” Gazeti hilo liliorodhesha baadhi ya dalili za “ugonjwa” huo zinazotia ndani “mfadhaiko, madeni, kutumia vitu vibaya, kufanya kazi kupita kiasi, kuhisi ni kana kwamba unanyimwa vitu unavyohitaji, wivu, na mshuko wa moyo.” Ilisemekana kwamba pesa ndizo zilisababisha kuzorota kwa ubora wa uhai wa wanadamu barani Afrika.

Kabla ya matatizo ya kiuchumi yaliyotokea hivi karibuni, India ilikuwa na kipindi cha ukuzi wa kiuchumi kisicho na kifani. Gazeti India Today International liliripoti kwamba mwaka wa 2007 “ilionekana wazi kwamba [nchi hiyo] ilifikia kiwango kipya cha kununua vitu kupita kiasi.” Hata hivyo, wakati huo, wasimamizi walikuwa na wasiwasi kwamba ukuzi huo wa kiuchumi wa India ungetokeza ghasia na jeuri.

Pia katika kipindi hicho, kizazi kipya cha vijana nchini Marekani walikuwa na mwelekeo wa kutumia pesa nyingi kununua bidhaa za bei ghali sana. Hata hivyo, kuwa na pesa nyingi za kutumia hakukuwaletea furaha. Wachunguzi walisema kwamba ufanisi ni mojawapo ya visababishi vikubwa vya uraibu wa kileo, kushuka moyo, na kujiua nchini humo. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba licha ya kuwa na pesa nyingi na mali, “ni Mmarekani mmoja tu kati ya watatu” aliyesema kuwa ana “furaha sana.”

Kwa Nini Wengine Hawaathiriwi?

Kwa upande mwingine, watu wengi, iwe ni matajiri au maskini, wawe chini ya hali nzuri au mbaya, hawana mahangaiko mengi ya pesa na mali. Kwa nini kuna tofauti hiyo?

Katika ripoti yenye kichwa The Meaning of Money, wachunguzi walisema kwamba watu fulani “wanasisimuliwa sana na pesa na kutawaliwa na pesa. Hilo linaweza kusababisha mfadhaiko na matatizo ya kiakili na kihisia.” Kwa kutofautisha walisema hivi: “Wale wanaopanga bajeti kwa uangalifu wanaweza kusimamia mambo yao ya kibinafsi nao wanajihisi vizuri. Wao ndio wanaotawala pesa zao na hawaachi pesa ziwatawale . . . Tunafikiri kwamba wale wanaopanga bajeti kwa uangalifu hawapatwi sana na mfadhaiko na mkazo mwingi.”

Una maoni gani kuhusu pesa? Hali mbaya ya uchumi wa ulimwengu inakuathiri jinsi gani? Je, pesa zinakutawala au wewe ndiye unayezitawala? Labda huna dalili za ule unaoitwa ugonjwa wa pesa. Hata hivyo, iwe wewe ni tajiri au maskini, sisi sote tunaweza kupatwa na matokeo mabaya ya mahangaiko ya pesa. Fikiria jinsi kubadili matumizi yako ya pesa kunavyoweza kukupa amani ya akili na kukufanya uwe na maisha yenye furaha zaidi.