Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia Pesa Zako kwa Hekima

Tumia Pesa Zako kwa Hekima

BIBLIA inasema “kupenda sana fedha ni chanzo cha uovu wote.” (1 Timotheo 6:10, Biblia Habari Njema) Watu fulani wanapenda pesa sana na wanajitoa kabisa ili kujikusanyia mali. Wengine wamekuwa watumwa wa pesa na wamepatwa na matokeo mabaya. Hata hivyo, zinapotumiwa vizuri, pesa zinaweza kufaidi sana. Biblia inasema kwamba “pesa ndizo hutokeza jibu katika mambo yote.”—Mhubiri 10:19.

Ingawa Biblia si kitabu kinachozungumzia mambo ya pesa, ina mashauri yanayoweza kukusaidia kutumia pesa zako kwa hekima. Hatua tano zifuatazo hupendekezwa na washauri wa mambo ya kifedha, na zinapatana na kanuni zilizoandikwa zamani katika Biblia.

Fahamu unachuma pesa ngapi na uhakikishe matumizi yako hayapiti kiasi hicho

Weka akiba. Biblia inaonyesha kwamba Waisraeli walionyeshwa umuhimu wa kuweka akiba. Waliambiwa waweke kando fungu la kumi (au asilimia 10) kila mwaka ili wahudhurie sherehe za kitaifa. (Kumbukumbu la Torati 14:22-27) Vivyo hivyo, mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo wa mapema watenge pesa fulani kila juma ambazo baadaye wangetoa mchango kuwasaidia Wakristo wenzao wenye uhitaji. (1 Wakorintho 16:1, 2) Washauri wengi wa mambo ya kifedha hupendekeza watu waweke akiba. Hakikisha kwamba unaweka pesa zako akiba. Mara tu unapolipwa, weka pesa unazotaka kuhifadhi katika benki au mahali pengine salama. Hilo litakusaidia kupinga vishawishi vyovyote vya kutumia pesa hizo.

Panga bajeti. Hiyo ndiyo njia pekee ya kudhibiti na kupunguza matumizi ya pesa zako. Unapokuwa na bajeti nzuri utajua pesa zako zinaenda wapi na unaweza kufikia miradi yako ya kifedha. Fahamu unachuma pesa ngapi na uhakikishe matumizi yako hayapiti kiasi hicho. Jifunze kutofautisha kati ya vitu unavyohitaji na vile unavyotaka tu. Kuhusiana na jambo hilo, Yesu aliwahimiza wasikilizaji wake kwa hekima ‘wahesabu gharama’ kabla ya kuanza mradi wowote. (Luka 14:28) Biblia inatushauri tuepuke madeni yasiyo ya lazima.—Methali 22:7.

Panga mambo. Fikiria kwa makini mahitaji yako ya wakati ujao. Kwa mfano, ikiwa unapanga kununua nyumba, ni vizuri kupata mkopo wa nyumba ulio na riba ya bei nafuu. Vivyo hivyo, mtu mwenye familia anaweza kuamua kununua bima ya maisha, afya, ulemavu, au bima ya aina nyingine ili kuilinda familia yake. Pia, kufikiria mahitaji yako ya wakati ujao kunaweza kuhusisha kupangia maisha baada ya kustaafu. Andiko la Methali 21:5 linatukumbusha kwamba “mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.”

Jifunze kutofautisha kati ya vitu unavyohitaji na vile unavyotaka tu

Jifunze. Jitahidi kujifunza ustadi mbalimbali na utunze afya yako ya kimwili na kiakili. Kufanya hivyo kutakuletea faida baadaye. Usiache kamwe kujifunza. Biblia inaonyesha kwamba “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri” ni mambo ya maana sana, na inatuhimiza tuendelee kusitawisha mambo hayo.—Methali 3:21, 22; Mhubiri 10:10.

Uwe na usawaziko. Usiache pesa zikutawale. Uchunguzi mmoja baada ya mwingine unaonyesha kwamba watu wenye furaha zaidi ni wale wanaowajali wengine kuliko kuhangaishwa na pesa. Watu fulani wanaruhusu pupa iwafanye wakose usawaziko. Jinsi gani? Baada ya kutosheleza mahitaji yao ya msingi, wao huanza kufuatilia utajiri. Hata hivyo, zaidi ya chakula, mavazi, na makao, mtu anahitaji nini kingine? Haishangazi kwamba mwandikaji wa Biblia aliyenukuliwa mwanzoni mwa makala hii aliandika hivi pia: “Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Timotheo 6:8) Kuridhika kunatusaidia tusipende pesa na tusipatwe na matatizo yanayokuja kwa sababu ya kufanya hivyo.

Kwa kweli, kupenda pesa ndio chanzo cha mambo mengi maovu. Pesa zitakutawala ukiziruhusu. Hata hivyo, zinapotumiwa vizuri, zinaweza kukupa nafasi ya kufuatilia mambo ya maana zaidi maishani, kama vile kuwa na uhusiano wa karibu na familia, marafiki, na Mungu. Lakini, inaonekana kwamba katika ulimwengu huu mtu hawezi kuishi bila mahangaiko ya pesa. Je, sikuzote pesa zitaendelea tu kuwahangaisha watu? Je, kuna tumaini lolote kwamba umaskini utakwisha? Makala ya mwisho katika mfululizo huu itajibu maswali hayo.

Zaidi ya chakula, mavazi, na makao, mtu anahitaji nini kingine?