Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maneno ya Hekima kwa Moyo na Afya

Maneno ya Hekima kwa Moyo na Afya

Maneno ya Hekima kwa Moyo na Afya

“Moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.”—METHALI 14:30.

“Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.”—METHALI 17:22.

● Maneno hayo rahisi lakini yenye maana sana yalisemwa na Mfalme Sulemani wa Israeli karibu miaka 3,000 iliyopita. * Lakini je, ni ya kweli? Wataalamu wa tiba ya kisasa wanasema nini?

Likilinganisha watu watulivu na watu wenye hasira, jarida Journal of the American College of Cardiology lilisema hivi: “Uchunguzi wa hivi karibuni unaonyesha kwamba kuna uhusiano kati ya hasira na uhasama na [magonjwa ya moyo].” Kwa hiyo, jarida hilo lilisema: “Huenda kuzuia na kutibu [magonjwa ya moyo] kukahusisha . . . matibabu ya kawaida ya mwili na dawa, na pia kumsaidia mgonjwa ajifunze kuzuia hasira na uhasama.” Kwa ufupi, moyo mtulivu humfanya mtu awe na afya nzuri kama Biblia inavyosema.

Moyo wenye shangwe unaweza pia kuchangia afya nzuri. Dakt. Derek Cox, afisa wa afya huko Scotland alisema hivi katika ripoti moja ya Shirika la Habari la BBC: “Ikiwa wewe ni mwenye furaha huenda wakati ujao usipatwe na magonjwa kama yale yanayowapata watu wasio na furaha.” Ripoti hiyohiyo ilisema hivi: “Watu wenye furaha wanalindwa pia dhidi ya matatizo kama vile magonjwa ya moyo na kiharusi.”

Kwa nini maneno yenye hekima ya Sulemani na pia yale ya waandikaji wengine wa Biblia yaliyoandikwa zamani sana ni yenye faida hata leo? Jibu ni rahisi. “Mungu akaendelea kumpa Sulemani hekima na uelewaji kwa wingi sana.” (1 Wafalme 4:29) Zaidi ya hilo, maneno hayo yenye hekima yaliandikwa katika lugha rahisi ili wote wafaidike. Na yanapatikana bila malipo yoyote!

Mbona usifanye kusoma Biblia kwa ukawaida kuwe sehemu ya maisha yako? Mamilioni ya watu wamegundua kwamba wanapata shangwe kubwa ‘hekima inapoingia moyoni mwao na ujuzi kupendeza nafsi yao, uwezo wa kufikiri unawatunza, utambuzi unawalinda.’ (Methali 2:10, 11) Je, hilo si jambo lenye kutia moyo sana?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika Biblia, neno “moyo” linarejelea mtu wa ndani, kutia ndani hisia zake.