Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Mawasiliano?—Sehemu ya 2

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Mawasiliano?—Sehemu ya 2

Vijana Huuliza

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Mawasiliano?​—Sehemu ya 2

Orodhesha mambo yaliyoonyeshwa hapa kuanzia na jambo unaloona kuwa muhimu kwako.

․․․․․ faragha yangu

․․․․․ wakati wangu

․․․․․ sifa yangu

․․․․․ marafiki wangu

UMEORODHESHA jambo gani kuwa namba moja kati ya mambo yaliyo hapo juu, yaani, ni jambo gani muhimu zaidi kwako? Jambo hilo, kutia ndani yale mambo mengine matatu yanaweza kuwa hatarini iwapo unatumia kituo cha mawasiliano.

Je, wewe unapaswa kufungua akaunti katika kituo cha mawasiliano? Ikiwa unaishi nyumbani, wazazi wako ndio wanaopaswa kuamua. * (Methali 6:20) Kama tu matumizi mengine yoyote ya Intaneti, vituo vya mawasiliano vina faida zake—na hatari. Ikiwa wazazi wako hawataki ujiandikishe, unapaswa kutii.—Waefeso 6:1.

Kwa upande ule mwingine, wazazi wakikuruhusu utumie kituo cha mawasiliano, unaweza kuepuka hatari zake kwa njia gani? Habari ya “Vijana Huuliza” katika Amkeni! la Julai (Mwezi wa 7) 2011 ilizungumzia maeneo mawili ambayo yanaweza kuhatarishwa—faragha yako na wakati wako. Katika habari hii, tutazungumzia sifa yako na marafiki wako.

SIFA YAKO

Kulinda sifa yako kunamaanisha kwamba unapaswa kuwa mwangalifu usiwape wengine sababu ya kukufikiria vibaya. Kwa mfano, wazia kwamba una gari jipya; halijakwaruzwa wala halijagongwa hata kidogo. Je, hungependa kulidumisha likiwa katika hali hiyo? Ungehisi namna gani ikiwa gari hilo lingeharibiwa kabisa katika aksidenti kwa sababu hukuwa mwangalifu?

Sifa yako inaweza kuathiriwa kwa njia kama hiyo unapotumia kituo cha mawasiliano. Msichana anayeitwa Cara anasema, “Picha moja tu au kitu fulani unachopachika bila kufikiri kinaweza kukuharibia sifa kabisa.” Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo sifa yako inaweza kuathiriwa kupitia . . .

Picha zako. Mtume Petro aliandika hivi: “Mwenendo wenu mbele ya watu wasiomjua Mungu unapaswa kuwa mwema kabisa.” (1 Petro 2:12, Biblia Habari Njema) Umeona nini ikiwa umetazama picha katika kituo cha mawasiliano?

“Nyakati nyingine mtu ambaye ninamheshimu anaweza kupachika picha zinazoonyesha ni kama amelewa.”—Ana, 19.

“Ninajua wasichana ambao hupigwa picha kwa njia inayokazia zaidi sehemu fulani za miili yao. Wanaonekana tofauti sana kwenye kituo cha mawasiliano kuliko wanavyoonekana kihalisi.”—Cara, 19.

Unaweza kusema nini kuhusu mtu ambaye amepachika picha katika kituo cha mawasiliano akiwa (1) amevalia mavazi yenye kuamsha hamu ya ngono au (2) anayeonekana ni kana kwamba amelewa?

1 ․․․․․

2 ․․․․․

Maelezo yako. “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu,” inasema Waefeso 4:29. Wengine wameona kwamba ni rahisi kwa lugha chafu, porojo, au mazungumzo kuhusu ukosefu wa maadili kuanza wanapowasiliana katika vituo vya mawasiliano.

“Watu hawaoni haya wanapotumia kituo cha mawasiliano. Maneno hayasikiki kuwa mabaya unapoyaandika kama yanavyosikika unapoyasema. Huenda usiandike matusi, lakini maneno yako yanaweza kuonyesha unawachezea wengine kimapenzi au hata yanaweza kuwa machafu.”—Danielle, 19.

Unafikiri ni kwa nini watu wengi hawaoni haya wanapoandika mambo kwenye Intaneti?

․․․․․

Je, picha na maelezo unayopachika ni muhimu? Ndiyo! “Shuleni, tumezungumzia sana jambo hilo,” anasema msichana anayeitwa Jane. “Tumezungumzia jinsi waajiri watakavyochunguza habari za mtu anayetaka kuajiriwa zilizo kwenye ukurasa wake katika kituo cha mawasiliano ili wajue tabia yake.”

Katika kitabu Facebook for Parents, Dakt. B. J. Fogg anasema kwamba yeye hufanya hivyo anapotaka kuwaajiri watu kazi. “Mimi huona kufanya uchunguzi huo kuwa haki yangu,” anasema. “Nikifaulu kuingia kwenye akaunti ya mtu anayetaka nimwajiri na nione mambo ya upuuzi, hilo halinifurahishi. Siwezi kumwajiri. Kwa nini? Kwa sababu watu ninaofanya nao kazi wanapaswa kuwa na uwezo mzuri wa kufanya maamuzi.”

Ikiwa wewe ni Mkristo, unapaswa kufikiria jambo lingine muhimu zaidi—jinsi mambo unayopachika yanavyoweza kuwaathiri watu wengine, iwe ni waamini wenzako au la. Mtume Paulo aliandika hivi: “Sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza kwa njia yoyote.”—2 Wakorintho 6:3; 1 Petro 3:16.

Mambo Unayoweza Kufanya

Ikiwa wazazi wako wanakuruhusu utumie kituo cha mawasiliano, chunguza picha ulizopachika na ujiulize: ‘Picha hizi zinafunua nini kunihusu? Je, hivyo ndivyo ninavyotaka kujulikana? Je, nitaaibika iwapo wazazi wangu, mzee Mkristo, au mwajiri wangu wa wakati ujao ataona picha hizi?’ Ukijibu ndiyo kwa swali hilo la mwisho, basi fanya mabadiliko. Hivyo ndivyo Kate mwenye umri wa miaka 21 alivyofanya. “Mzee Mkristo alizungumza nami kuhusu picha niliyokuwa nimepachika,” anasema, “na nilishukuru sana kwamba alifanya hivyo. Nilijua kwamba alitaka kulinda sifa yangu.”

Pia, chunguza kwa uangalifu maelezo ambayo umepachika—kutia ndani maelezo ambayo wengine wamepachika katika ukurasa wako. Usimruhusu yeyote aseme “maneno ya kipumbavu” au “mizaha michafu” hapo. (Waefeso 5:3, 4) “Nyakati nyingine watu hupachika maelezo yenye matusi au yenye maana mbili,” anasema Jane mwenye umri wa miaka 19. “Hata ingawa si wewe uliyeyasema, maneno hayo yanakufanya wewe uwe na sifa mbaya kwa kuwa ni ukurasa wako.”

Ili kulinda sifa yako, unaweza kuweka mipaka gani kuhusu picha na maelezo unayopachika?

․․․․․

MARAFIKI WAKO

Ikiwa ungekuwa na gari jipya, ungemruhusu mtu yeyote tu aingie ndani? Wazazi wako wakikuruhusu ufungue akaunti katika kituo cha mawasiliano, unapaswa kuamua ni nani utakayemruhusu—au kumkubali—awe rafiki yako. Unapaswa kuwa mteuzi kadiri gani?

“Watu wengine huona kwamba kupata marafiki wengi ndilo kusudi lao kuu—kadiri wanavyopata wengi zaidi ndivyo wanavyofurahi. Wanaweza kuwakubali hata watu ambao hawawafahamu vizuri.”—Nayisha, 16.

“Kituo cha mawasiliano hukusaidia uungane tena na watu mliofahamiana zamani. Lakini nyakati nyingine ni afadhali kutoanzisha urafiki tena na watu kama hao.”—Ellen, 25.

Mambo Unayoweza Kufanya

Dokezo: Chunguza na ubadili. Chunguza orodha yako ya marafiki na ufanye marekebisho inapohitajika. Kila wakati unaposoma jina fulani, jiulize:

1. ‘Ninamjua mtu huyu vizuri kadiri gani katika maisha yake ya kawaida?’

2. ‘Mtu huyu hupachika picha na maelezo ya aina gani?’

3. ‘Je, rafiki huyu ananiathiri kwa njia nzuri maishani?’

“Mimi hupitia ‘orodha yangu ya marafiki’ kila mwezi. Ikiwa kuna mtu ambaye sina uhakika naye au ambaye simfahamu vizuri, mimi humwondoa kwenye orodha yangu.”—Ivana, 17.

Dokezo: Uwe na ‘masharti ya kukubali marafiki.’ Jiwekee mipaka ya watu ambao utaomba au kukubali wawe marafiki wako, kama tu unavyofanya kihalisi. (1 Wakorintho 15:33) Kwa mfano, msichana anayeitwa Leanne anasema: “Masharti yangu ni haya: Ikiwa sikufahamu, siwezi kukubali ombi lako la kutaka uwe rafiki yangu. Nikiona jambo fulani kwenye ukurasa wako linalonitia wasiwasi, nitakufuta kutoka kwenye ‘orodha yangu ya marafiki’ na sitakubali uwe rafiki yangu tena hata ukituma ombi lingine.” Wengine wameweka masharti kama hayo.

“Siwezi kumkubali mtu yeyote tu kuwa ‘rafiki.’ Hiyo ni hatari.”—Erin, 21.

“Nimepata maombi kutoka kwa watu niliokuwa nao shuleni wakiomba niwe rafiki zao. Lakini nilipokuwa shuleni nilijitahidi sana kuepuka kufanya urafiki nao; kwa nini niwafanye wawe marafiki sasa?”—Alex, 21.

Hapa chini, andika ‘masharti yako ya kukubali marafiki.’

․․․․․

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Amkeni! haipendekezi wala haishutumu tovuti yoyote ya mawasiliano. Wakristo wanapaswa kuhakikisha kwamba matumizi yao ya Intaneti hayavunji kanuni zozote za Biblia.—1 Timotheo 1:5, 19.

[Blabu katika ukurasa wa 10]

Methali moja ya Biblia inasema: “Ukilazimika kuchagua kati ya sifa nzuri au mali nyingi, chagua sifa nzuri.”—Methali 22:1, Today’s English Version

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Pitia habari hii na ile ya “Vijana Huuliza” iliyo katika toleo la Amkeni! la Julai 2011 pamoja na wazazi wako. Zungumzieni jinsi matumizi yako ya Intaneti yanavyoathiri (1) faragha yako, (2) wakati wako, (3) sifa yako, na (4) marafiki wako.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

TAARIFA KWA WAZAZI

Watoto wako wanaweza kujua mengi kuhusu Intaneti kuliko unavyojua. Lakini hawana uwezo wa kufanya maamuzi yanayofaa kama wewe. (Methali 1:4; 2:1-6) Ni kama vile Parry Aftab, mtaalamu wa usalama kwenye Intaneti, alivyosema: “Vijana wanajua mengi zaidi kuhusu teknolojia. Wazazi wanajua mengi zaidi kuhusu maisha.”

Katika miaka ya karibuni, vituo vya mawasiliano vimekuwa maarufu sana. Je, kijana wako ni mkomavu kiasi cha kutosha kuvitumia? Wewe ndiye utakayeamua. Kama tu kuendesha gari, kuwa na akaunti ya benki, au kutumia kadi ya mkopo, kuna hatari za kutumia vituo vya mawasiliano. Ni nini baadhi ya hatari hizo?

FARAGHA. Vijana wengi hawajui hatari ya kuweka habari nyingi sana kwenye Intaneti. Kuandika mahali wanapoishi, mahali wanapoenda shule, au wakati ambapo wako nyumbani au hawapo kunaweza kuhatarisha usalama wa familia yako.

Unaweza kufanya nini? Watoto wako walipokuwa wachanga uliwafundisha kuangalia pande zote za barabara kabla ya kuvuka. Sasa kwa kuwa wamekuwa wakubwa, wafundishe jinsi ya kutumia Intaneti kwa njia salama. Soma habari kuhusu faragha zilizoonyeshwa katika habari ya “Vijana Huuliza” ya mwezi uliopita. Pia, ona Amkeni! la Oktoba (Mwezi wa 10) 2008, ukurasa wa 3-9. Kisha zungumzia habari hiyo pamoja na kijana wako. Jitahidi kumkazia awe na “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri” anapojitahidi kutumia Intaneti kwa njia salama.—Methali 3:21.

WAKATI. Mtu anaweza kuwa mraibu wa vituo vya mawasiliano. “Baada tu ya kuwa na akaunti hiyo kwa siku kadhaa, singeweza kuacha kuitazama,” anasema Rick mwenye umri wa miaka 23. “Nilitumia saa nyingi kutazama picha na vitu vingine vilivyopachikwa.”

Unaweza kufanya nini? Ukiwa pamoja na watoto wako, soma na uzungumzie habari yenye kichwa “Vijana Huuliza . . . Je, Mimi Ni Mraibu wa Vifaa vya Elektroniki?” iliyo kwenye Amkeni! la Januari (Mwezi wa 1) 2011. Kazia hasa sanduku lenye kichwa “Nilikuwa Mraibu wa Vituo vya Mawasiliano,” kwenye ukurasa wa 26. Msaidie kijana wako awe “mwenye kiasi katika mazoea” na ajiwekee mipaka ya wakati anaotumia kwenye Intaneti. (1 Timotheo 3:2) Mkumbushe kwamba kuna mambo mengine zaidi maishani mbali na kuwasiliana kwenye vituo vya mawasiliano!

SIFA. Methali moja ya Biblia inasema, “Mambo mema au mabaya ambayo watoto hufanya hufunua jinsi walivyo.” (Methali 20:11, Contemporary English Version) Hilo ni kweli kama nini kuhusu Intaneti! Isitoshe, kwa kuwa vituo vya mawasiliano ni vituo vya umma, mambo ambayo watoto wako wanapachika yanaweza kuathiri si sifa yao tu bali pia ile ya familia.

Unaweza kufanya nini? Vijana wanapaswa kujua kwamba kile wanachopachika kwenye Intaneti kinaonyesha wao ni nani. Pia wanahitaji kujua kwamba chochote wanachopachika kwenye Intaneti hubaki humo. “Si rahisi kwa vijana kuelewa wazo la kwamba habari iliyo kwenye Intaneti ni ya kudumu lakini ni muhimu kwamba waanze kujifunza jambo hilo,” anaandika Dakt. Gwenn Schurgin O’Keeffe katika kitabu CyberSafe. “Njia moja ya kuwaeleza watoto jinsi wanavyopaswa kujiendesha kwenye Intaneti ni kuwakumbusha kwamba hawapaswi kusema chochote kwenye Intaneti ambacho hawawezi kusema wanapozungumza na watu hadharani.”

MARAFIKI. “Vijana wengi wangependa kuonwa kuwa maarufu,” anasema Tanya mwenye umri wa miaka 23, “kwa hiyo wako tayari kukubali ‘marafiki’ ambao hawawafahamu kabisa au ambao hawaongozwi na kanuni zozote.”

Unaweza kufanya nini? Msaidie mwana au binti yako aweke ‘masharti ya kukubali marafiki.’ Kwa mfano, Alicia mwenye umri wa miaka 22, haongezi marafiki wa rafiki zake kwenye orodha yake. Anasema, “Ikiwa sikufahamu au sijawahi kukutana nawe uso kwa uso, siwezi kukuongeza kwenye orodha yangu eti tu kwa sababu rafiki yako ni rafiki yangu.”

Wenzi wa ndoa wanaoitwa Tim na Julia walifungua akaunti yao kwenye kituo cha mawasiliano na wangeweza kuitumia kuona marafiki wa binti yao na mambo waliyokuwa wakipachika. “Tulimwambia kwamba ni lazima atuongeze katika orodha yake ya marafiki,” anasema Julia. “Anapowasiliana na watu ni kana kwamba anawakaribisha ndani ya nyumba yetu. Kwa hiyo, tunataka kujua wao ni nani.”

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kama vile tu gari linavyoweza kuharibika linapoendeshwa ovyoovyo, ndivyo sifa yako inavyoweza kuharibika ukipachika picha na maelezo machafu kwenye Intaneti

[Picha katika ukurasa wa 12]

Je, unaweza kumruhusu mtu usiyemjua aingie ndani ya gari lako kwa sababu tu anahitaji usafiri? Basi kwa nini ufanye urafiki na mtu usiyemjua kwenye Intaneti?