Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Jinsi ya Kuishi Maisha Yenye Furaha

Jinsi ya Kuishi Maisha Yenye Furaha

“Nitakuwa na furaha nikifunga ndoa na kupata watoto.”

“Nitakuwa na furaha nikimiliki nyumba yangu mwenyewe.”

“Nitakuwa na furaha nikipata kazi.”

“Nitakuwa na furaha nikiwa na . . .”

JE, UMEWAHI kuhisi hivyo? Je, ulipopata kile ulichokuwa unatamani, furaha yako ilidumu, au ilianza kupungua? Kwa kweli, kufikia lengo au kupata kitu tulichotamani kunaweza kutufanya tuwe na furaha, lakini furaha hiyo huenda isidumu. Furaha ya kudumu haitegemei tu mafanikio au vitu tulivyo navyo. Badala yake, furaha ya kweli inategemea mambo mengi kama tu jinsi mtu anavyohitaji kufanya mambo mbalimbali ili awe na afya nzuri.

Mahitaji yetu yanatofautiana. Kinachokufurahisha wewe huenda kisimfurahishe mwingine. Kwa kuongezea, tunabadilika tunapoendelea kukua. Ingawa hivyo, uthibitisho unaonyesha kwamba kuna mambo ambayo huhusianishwa na furaha. Kwa mfano, furaha ya kweli inahusiana na kuridhika, kutowaonea wivu wengine, kuwapenda watu, na kutokata tamaa. Acheni tuchunguze mambo hayo.

 1. KURIDHIKA

Mwanamume mmoja mwenye hekima alisema hivi: “Pesa ni ulinzi.” Hata hivyo, aliongezea kusema hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato. Hilo pia ni ubatili.” (Mhubiri 5:10; 7:12) Alimaanisha nini? Ingawa ni kweli tunahitaji pesa ili kuishi, tunapaswa kuepuka pupa, kwa sababu hatuwezi kutosheleza tamaa hiyo! Mfalme Sulemani wa Israeli la kale, aliyesema maneno hayo, alifanya utafiti ili kuthibitisha ikiwa kuishi maisha ya anasa kunaleta furaha ya kweli. Aliandika hivi: “Sikuyanyima macho yangu chochote ambacho yaliomba. Sikuunyima moyo wangu shangwe ya aina yoyote.”—Mhubiri 1:13; 2:10.

Baada ya kujikusanyia utajiri, Sulemani alijenga majumba makubwa, alitengeneza mabwawa ya kuogelea na bustani maridadi, na alikuwa na wafanyakazi wengi. Alipata kila kitu alichotaka. Alijifunza nini? Mambo hayo yalimletea furaha kwa kiasi fulani, lakini si kwa muda mrefu. Aliandika hivi: “Na, tazama! kila kitu kilikuwa ubatili na kufuatilia upepo, wala hapakuwa na lolote lenye faida.” Hata aliyachukia maisha! (Mhubiri 2:11, 17, 18) Kwa kweli, Sulemani alitambua kwamba maisha ya kujistarehesha tu hayaleti furaha ya kudumu. *

Je, utafiti wa kisasa unakubaliana na jambo hilo? Makala moja kwenye Jarida la Masomo ya Jinsi ya Kuwa na Furaha (la Kiingereza) inaeleza hivi: “Mara baada ya mtu kutosheleza mahitaji yake ya msingi, vitu vingine atakavyozidi kupata havitamwongezea furaha.” Kwa kweli, utafiti unaonyesha kwamba ikiwa mtu anaamua kufuatilia maisha ya anasa na kupuuza viwango vya maadili na vya kiroho, anaweza kupoteza furaha.

KANUNI YA BIBLIA: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa.”Waebrania 13:5.

2. EPUKA KUWAONEA WIVU WENGINE

Kamusi moja inafafanua wivu kuwa “uchungu au kinyongo kinachotokana na kutambua kwamba mwingine ana kitu ambacho huna, na pia tamaa ya kutaka kuwa na kitu hicho.” Kama tu uvimbe hatari unaoenea haraka, kuwaonea wivu wengine kunaweza kutawala maisha ya mtu na kumfanya akose furaha. Mtu huanzaje kuwaonea wivu wengine? Tunawezaje kutambua kama tuna tatizo hilo? Na tunawezaje kukabiliana nalo?

Kulingana na kitabu Encyclopedia of Social Psychology watu huwa na mwelekeo wa kuwaonea wivu watu ambao wanalingana nao, huenda katika umri, uzoefu, au malezi. Kwa mfano, si rahisi kwa mfanyabiashara kumwonea wivu mwigizaji maarufu. Lakini huenda akamwonea wivu mfanyabiashara mwenzake mwenye mafanikio kuliko yeye.

Mfano: Maofisa fulani katika utawala wa zamani wa Uajemi, hawakumwonea wivu mfalme, badala yake walimwonea wivu Danieli ofisa mwenzao. Kwa sababu ya wivu wao hata walifanya mpango wa kumwua Danieli! Hata hivyo mpango huo haukufanikiwa. (Danieli 6:1-24) Kitabu Encyclopedia of  Social Psychology kinaendelea kusema hivi: “Ni muhimu tutambue kwamba wivu unaweza kutufanya tutake kuwadhuru wengine. Ndiyo maana kuna visa vingi vya ukatili katika historia ya wanadamu ambavyo vimesababishwa na kuwaonea wivu wengine.” *

Kuwaonea wivu wengine kunaweza kumfanya mtu ashindwe kufurahia mambo mazuri maishani

Unawezaje kutambua ikiwa unawaonea wivu wengine? Jiulize hivi: ‘Je, wenzangu wanapofanikiwa mimi hushangilia au huhuzunika? Ikiwa ndugu au dada yangu, mwanafunzi mwenzangu mwenye kipaji, au mfanyakazi mwenzangu anakosa kufanikiwa, je, mimi huhuzunika au hufurahi?’ Majibu yako yataonyesha ikiwa umeanza kuwaonea wivu wengine. (Mwanzo 26:12-14) Kitabu hicho pia kinaendelea kusema hivi: “Kuwaonea wivu wengine kunaweza kumfanya mtu ashindwe kufurahia mambo mazuri maishani na kumfanya asione jambo lolote jema katika maisha. . . . Tabia kama hiyo haiwezi kumletea mtu furaha.”

Tunaweza kupambana na hali hiyo kwa kusitawisha unyenyekevu wa kweli na kiasi, sifa ambazo zitatuwezesha kufurahia na kuthamini uwezo na sifa nzuri za wengine. Biblia inasema hivi: “Bila kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mkiwaona wengine kuwa ni bora kuliko ninyi.”—Wafilipi 2:3.

KANUNI YA BIBLIA: “Na tusiwe wenye kujisifu, wenye kuchochea mashindano juu ya mtu na mwenzake, tukioneana wivu.”Wagalatia 5:26.

3. WAPENDE WATU

Kitabu Social Psychology kinasema: “Ikiwa watu wana uhusiano mzuri miongoni mwao, jambo hilo linaweza kuwafanya wafurahie maisha hata kuliko furaha inayopatikana kwa kuwa na kazi, mshahara mnono, kukubaliwa katika jamii, au kuwa na afya nzuri.” Kwa ufupi, ili wanadamu wawe na furaha ya kweli, wanahitaji kupenda na kupendwa. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema hivi: “Ikiwa . . . sina upendo, mimi si kitu.”—1 Wakorintho 13:2.

Sisi sote tuna nafasi ya kusitawisha upendo. Kwa mfano, Vanessa alikuwa na baba mkatili na mlevi kupindukia. Alipokuwa na umri wa miaka 14, alitoroka nyumbani na hakuwa na makazi maalumu, na hata alimwomba Mungu amsaidie. Kisha, inaonekana kwamba Mungu alimsaidia kwa sababu alianza kuishi na familia iliyofuata kanuni ya Biblia inayosema “upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili.” (1 Wakorintho 13:4) Kuishi na familia hiyo na kujifunza Biblia, kulimsaidia Vanessa kupona kihisia na kiakili. Alisema hivi: “Nilianza kufaulu masomoni na alama zangu zikawa bora.”

Vanessa bado anakumbuka mambo yaliyompata zamani. Hata hivyo, sasa ana ndoa yenye furaha na ni mama wa wasichana wawili.

KANUNI YA BIBLIA: “Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”Wakolosai 3:14.

 4. USIKATE TAMAA

Ni nani ambaye hana shida? Kama Biblia inavyosema, kuna “wakati wa kulia” na “wakati wa kuomboleza.” (Mhubiri 3:4) Kutokata tamaa kunatusaidia kukabiliana kwa mafanikio na hali ngumu. Acha tuchunguze kisa cha Carol na Mildred.

Carol ana kisukari, ugonjwa unaoathiri uti wa mgongo, matatizo ya kupumua, na ugonjwa wa macho ambao umepofusha jicho lake la kushoto. Hata hivyo anasema hivi: “Najitahidi sana nisivunjike moyo kwa muda mrefu. Mimi hujihuzunikia. Lakini naepuka kujifikiria kupita kiasi na namshukuru Mungu kwa sababu ya yale niwezayo kufanya, hasa yale ambayo ninaweza kuwatendea wengine.”

Mildred pia anaugua magonjwa kadhaa, kutia ndani baridi-yabisi, saratani ya matiti, na kisukari. Lakini kama tu Carol, anajitahidi kutofikiria matatizo yake kupita kiasi. Anasema hivi: “Nimejifunza kuwapenda watu na kuwafariji wengine wanapokuwa wagonjwa, ninapofanya hivyo mimi pia hufarijika. Kwa kweli, ninapowafariji wengine, wasiwasi kuhusu hali yangu unapungua.”

Carol na Mildred wanapata shangwe kwa kuwafariji wengine

Ingawa wanawake hao wawili wanazingatia matibabu, jambo kuu kwao, si afya zao, bali mtazamo wao na yale wanayoweza kutimiza. Kwa sababu hiyo wana shangwe na amani ya akili ambayo hakuna mtu anayeweza kuwanyang’anya. Kwa kuongezea, wanapendwa na wanawatia moyo wengine wanaokabili matatizo mbalimbali.

KANUNI YA BIBLIA: “Mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima.”Yakobo 1:12.

Hekima ya Biblia inapotumiwa inakuwa kama “mti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika sana wataitwa wenye furaha.” (Methali 3:13-18) Kwa nini usijionee ukweli wa maneno hayo kwa kutumia hekima hiyo? Zaidi ya yote, Mtunzi wa kitabu hicho kitakatifu, ambaye pia anaitwa “Mungu mwenye furaha,” anataka wewe pia uwe na furaha.—1 Timotheo 1:11.

^ fu. 11 Simulizi kuhusu utafiti huo wa Sulemani linapatikana kwenye Mhubiri 2:1-11.

^ fu. 17 Kisa kimoja kinachothibitisha jambo hilo kinamhusu Yesu Kristo. Andiko la Marko 15:10 linasema kwamba ‘wakuu wa makuhani walitaka auawe kwa sababu ya wivu.’