Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Pesa

Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Pesa

KUNA msemo usemao, “Pesa ndiyo kila kitu.” Kuna ukweli wa kiasi fulani katika msemo huo. Kwa kweli, pesa zinahitajika ili kununua chakula, mavazi, na kukodi au kununua nyumba. Mhariri mmoja wa mambo ya uchumi aliandika hivi: “Pesa ina umuhimu mkubwa sana katika jamii. Ikiwa pesa itaacha kutumika, huenda ndani ya mwezi mmoja tukachanganyikiwa na vita vikatokea.”

Hata hivyo, pesa haiwezi kutimiza kila kitu. Arne Garborg, mtungaji wa mashairi nchini Norway alisema hivi kuhusu pesa: “Unaweza kununua chakula, lakini si hamu ya kula, dawa, lakini si afya; kitanda kizuri, lakini si usingizi; ujuzi, lakini si hekima; mvuto, lakini si uzuri; fahari, lakini si kupendwa; burudani, lakini si furaha; kujulikana, lakini si marafiki; wafanyakazi, lakini si uaminifu.”

Mtu anapokuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu pesa, yaani, anapoziona kuwa njia ya kufikia malengo maishani, anaweza kuridhika kwa kiasi fulani. Biblia hutuonya kwamba “kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine . . . wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:10.

Ona kwamba chanzo cha matatizo ni kupenda pesa wala si pesa zenyewe. Kwa kweli, kuzingatia mno pesa kunaweza kutenganisha marafiki na washiriki wa familia. Fikiria baadhi ya mifano.

Daniel: * “Sikuzote nilifikiri kwamba rafiki yangu Thomas ni mtu mzuri na mnyofu. Hatukuwahi kukosana kwa jambo lolote, mpaka nilipomuuzia gari langu. Sikujua kwamba gari langu lilikuwa na tatizo. Hata hivyo, katika mkataba alikubali kulinunua jinsi lilivyo. Miezi matatu baadaye gari hilo liliharibika. Thomas alifikiri nimemwibia na kwa hasira alisisitiza nimrudishie pesa zake. Nilishtuka sana! Nilipojaribu kumweleza, alikuwa mkali sana. Tatizo lilipohusu pesa, Thomas alibadilika na kuwa mtu mwingine kabisa.”

Esin: “Nesrim ni mdogo wangu wa pekee. Sikuzote tulielewana, lakini sikuwahi kufikiria kwamba siku moja uhusiano wetu ungeharibika kwa sababu ya pesa. Baadaye mambo yalikuwa hivyo. Wazazi wetu walipokufa walituachia urithi na walisisitiza kwamba pesa zigawanywe sawa kati yetu. Hata hivyo, mdogo wangu alienda kinyume cha mapenzi ya wazazi wetu na kudai apewe mali nyingi zaidi. Kwa sababu nilitaka kuheshimu maamuzi ya wazazi wetu, alikasirika sana na kunitishia. Mpaka leo, bado ananichukia sana.”

PESA NA UBAGUZI

Maoni yasiyofaa kuhusu pesa yanaweza kuwafanya watu wawahukumu wengine. Kwa mfano, huenda tajiri akafikiri kwamba watu maskini ni wavivu sana ndiyo maana hawawezi kuboresha maisha yao. Au maskini anaweza kufikiria kwamba matajiri wanapenda sana mali au wana pupa. Leanne, ni kijana kutoka katika familia moja tajiri aliyeathiriwa na aina hiyo ya ubaguzi. Anasimulia hivi:

Shauri la Biblia kuhusu pesa linafaa leo kama ilivyokuwa lilipoandikwa

“Nilijulikana kuwa mtoto wa tajiri. Mara nyingi watu waliniambia hivi: ‘Ukitaka chochote Baba yako anakupa,’ au ‘Usifikiri wote ni matajiri na tunaweza kumiliki magari mazuri kama ya familia yenu.’ Mwishowe niliwaomba rafiki zangu waache kutumia maneno hayo kwa kuwa yananiumiza. Ninataka kujulikana kuwa mtu anayewatendea mema wengine wala si mtu mwenye pesa.”

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia hailaumu pesa wala haishutumu wale walio na pesa—hata wale wenye pesa nyingi. Jambo muhimu si kiasi cha pesa alicho nacho mtu bali mtazamo wake kuhusu kile alicho nacho au kile anachotaka kuwa nacho. Shauri la Biblia kuhusu pesa ni lenye usawaziko na linafaa leo kama ilivyokuwa lilipoandikwa. Fikiria mifano kadhaa.

BIBLIA INASEMA: “Usijitaabishe kutafuta utajiri.”—Methali 23:4.

Kulingana na kitabu cha The Narcissism Epidemic, watu wanaotafuta utajiri wako katika hatari ya “kupatwa na matatizo ya akili; pia wanapata matatizo mengine ya kiafya kama vile vidonda vya koo, maumivu ya mgongo na kichwa, na wengi wao hunywa pombe kupita kiasi na kutumia dawa za kulevya. Inaonekana kwamba kutafuta sana mali hufanya watu wakose furaha.”

BIBLIA INASEMA: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa.”—Waebrania 13:5.

Ni kweli kwamba hata mtu aliyeridhika hupatwa na wasiwasi kuhusu pesa; hata hivyo, halemewi na wasiwasi huo. Kwa mfano, mtu aliyeridhika hatakuwa na wasiwasi kupita kiasi anapokabili hali mbaya ya uchumi. Badala yake, atajitahidi kuwa na mtazamo kama wa mtume Paulo aliyeandika hivi: “Najua jinsi ya kupungukiwa na vyakula, kwa kweli najua jinsi ya kuwa na wingi. Katika mambo yote na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa, jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya kupatwa na uhitaji.” —Wafilipi 4:12.

BIBLIA INASEMA: “Anayetegemea utajiri wake—yeye mwenyewe ataanguka.” —Methali 11:28.

Watafiti wanasema kwamba matatizo ya pesa ni chanzo cha talaka katika ndoa nyingi. Pia, watu wengi hujiua kwa sababu ya matatizo yanayohusu pesa. Inasikitisha sana kwamba baadhi ya watu huona pesa kuwa muhimu kuliko viapo vyao vya ndoa au hata uhai wao! Hata hivyo, wale wenye maoni yenye usawaziko hawategemei sana pesa. Badala yake, wanatambua hekima ya maneno haya ya Yesu: “Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.”—Luka 12:15.

UNA MAONI GANI KUHUSU PESA?

Kujichunguza kunaweza kukusaidia utambue ikiwa unahitaji kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu pesa. Kwa mfano, jiulize maswali yafuatayo.

  • Je, ninavutiwa na mbinu za kupata utajiri wa haraka?

  • Je, ninashindwa kuwaonyesha wengine ukarimu kwa kutumia pesa zangu?

  • Je, ninapenda kuanzisha urafiki na watu ambao muda wote huzungumzia pesa na vitu wanavyomiliki?

  • Je, ninadanganya au kutumia njia nyingine zisizo halali ili kupata pesa?

  • Je, pesa hunifanya nihisi kuwa wa maana kuliko wengine?

  • Je, ninafikiria kuhusu pesa wakati wote?

  • Je, mtazamo wangu kuhusu pesa unahatarisha afya yangu na uhusiano na familia yangu?

    Uwe mkarimu kwa kuwapa wengine vitu vyako

Ikiwa jibu lako ni ndiyo kwa swali lolote kati ya hayo, jitahidi kukataa mawazo na ushawishi wa kupenda mali. Epuka marafiki wanaopenda sana pesa na mali zao. Badala yake, shirikiana na watu wanaoheshimu sana kanuni za juu za maadili kuliko mali.

Usiruhusu kupenda pesa kutie mizizi katika moyo wako. Badala yake, weka pesa mahali pake—zisiwe muhimu kuliko marafiki, familia, hisia, na afya yako. Kwa kufanya hivyo, utaonyesha kwamba una maoni yenye usawaziko kuhusu pesa.

^ fu. 7 Majina katika makala hii yamebadilishwa.