Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Nimeazimia Kuwa Askari-Jeshi wa Kristo

Nimeazimia Kuwa Askari-Jeshi wa Kristo

Niliinua polepole kitambaa cheupe huku risasi zikivuma karibu nami. Wanajeshi waliokuwa wakifyatua risasi waliniamuru nitoke mahali nilipokuwa nimejificha. Niliwaendea nikiwa mwangalifu, bila kujua ikiwa ningeishi au ningekufa. Ni nini kilichofanya niwe katika hali hiyo ngumu?

NILIZALIWA nikiwa mwana wa saba kati ya watoto wanane wa wazazi wenye bidii huko Karítsa, kijiji kidogo nchini Ugiriki. Ulikuwa mwaka 1926.

Mwaka uliotangulia, wazazi wangu walikuwa wamekutana na John Papparizos, Mwanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo) mwenye bidii na aliyeongea sana. Kwa kuwa walipendezwa na jinsi John alivyosababu vizuri akitumia Maandiko, walianza kuhudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia katika kijiji chetu. Mama alikuwa na imani thabiti katika Yehova Mungu, na licha ya kwamba hakujua kusoma, aliwahubiria wengine kila alipopata fursa. Kwa kusikitisha, Baba alikazia fikira kutokamilika kwa watu na hatua kwa hatua akaacha kuhudhuria mikutano ya Kikristo.

Mimi na ndugu zangu tuliheshimu Biblia lakini tulipokuwa tukikua tulikengeushwa na raha za ujanani. Kisha, katika 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza barani Ulaya, tukio fulani kijijini kwetu lilitugutusha. Nicolas Psarras, jirani na binamu yetu, aliyekuwa amebatizwa muda mfupi kabla ya hapo, aliandikishwa katika jeshi la Ugiriki. Nicolas, aliyekuwa na umri wa miaka 20, kwa ujasiri aliwaambia hivi wenye mamlaka katika jeshi: “Siwezi kwenda vitani kwa sababu mimi ni askari-jeshi wa Kristo.” Alishtakiwa katika mahakama ya kijeshi na kuhukumiwa miaka kumi gerezani. Tulishtuka!

Jambo zuri ni kwamba mapema katika 1941, kwa muda mfupi majeshi ya Muungano yaliingia nchini Ugiriki, na Nicolas akaachiliwa kutoka gerezani. Alirudi Karítsa, na kaka yangu, Ilias, akamwuliza maswali mengi ya Biblia. Nami nilisikiliza kwa makini. Baadaye, mimi, Ilias, na mdogo wetu wa kike, Efmorfia, tukaanza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida pamoja na Mashahidi. Mwaka uliofuata, sote watatu tulijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Baadaye, ndugu zangu wanne wakawa Mashahidi waaminifu.

Mwaka 1942, Kutaniko la Karítsa lilikuwa na ndugu na dada vijana wenye umri wa kati ya miaka 15 na 25. Sote tulijua kuwa majaribu makali yalikuwa mbele yetu. Hivyo, ili kujiimarisha, tulikutana kila tulipoweza ili kujifunza Biblia, kuimba nyimbo za kiroho, na kusali. Kwa sababu hiyo, imani yetu iliimarishwa.

Demetrius pamoja na rafiki zake huko Karítsa

VITA VYA WENYEWE KWA WENYEWE

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokaribia kwisha, wakomunisti Wagiriki waliasi dhidi ya serikali ya Ugiriki, hivyo vita vikali vya wenyewe kwa wenyewe vikaanza. Wapiganaji wa kuvizia waliokuwa wakomunisti walizunguka vijijini wakiwalazimisha wanakijiji wajiunge nao. Walipovamia kijiji chetu, waliniteka nyara pamoja na Mashahidi wengine wawili vijana, Antonio Tsoukaris na Ilias. Tuliwaambia kuwa sisi ni Wakristo na hatuungi mkono upande wowote. Hata hivyo, walitulazimisha kutembea hadi Mlima Olympus, mwendo wa saa 12 kutoka kijiji chetu.

Muda mfupi baadaye, ofisa Mkomunisti alituamuru tujiunge na kikundi cha wapiganaji wa kuvizia. Tulipomweleza kwamba Wakristo wa kweli hawaendi vitani, ofisa huyo aliyekuwa amekasirika alitupeleka mbele ya jenerali fulani. Tulipomweleza hali yetu, jenerali huyo alituamuru hivi, “Basi chukueni punda na mwasafirishe wale walioumia kutoka vitani hadi hospitalini.”

Tukamjibu hivi, “Lakini vipi tukikamatwa na majeshi ya serikali? Je, hawatatuona kuwa wanajeshi?” Akasema hivi, “Basi wapelekeeni wanajeshi mikate.” Tukamwuliza hivi, “Lakini vipi ikiwa ofisa fulani ataona tukiwa na punda na kutuamuru tupeleke silaha vitani?” Jenerali huyo alifikiri kwa muda mrefu. Hatimaye, akajibu hivi: “Basi, mnaweza kuchunga kondoo. Kaeni mlimani mkichunga kondoo.”

Kwa hiyo, vita vya wenyewe kwa wenyewe vilipokuwa vikiendelea karibu nasi, sote watatu tulihisi kuwa dhamiri zetu zilituruhusu kuchunga kondoo. Mwaka mmoja baadaye, Ilias, kwa kuwa ndiye aliyekuwa mkubwa, aliruhusiwa kurudi nyumbani kumtunza mama yetu aliyekuwa mjane. Antonio akawa mgonjwa na kuachiliwa huru. Hata hivyo, mimi nikabaki.

Wakati huohuo, jeshi la Ugiriki lilikuwa likiwashinda wakomunisti hatua kwa hatua. Kikundi kilichokuwa kimeniteka kilitoroka kupitia milimani kuelekea nchi jirani ya Albania. Tulipokaribia mpaka, ghafula tulijikuta tumezungukwa na wanajeshi wa Ugiriki. Waasi hao wakaogopa na kukimbia. Nilijificha nyuma ya mti uliokuwa umeanguka, na hapo ndipo nilipokutana na wanajeshi niliotaja mwanzoni.

Nilipowaambia wanajeshi wa Ugiriki kwamba nilikuwa nimetekwa nyara na wakomunisti, walinipeleka nikahojiwe kwenye kambi ya kijeshi karibu na jiji la Véroia, ambalo lilikuwa jiji la kale la Kibiblia la Beroya. Nikiwa huko niliamriwa nichimbe mitaro kwa ajili ya wanajeshi. Nilipokataa, ofisa aliyesimamia mahali hapo aliamuru nipelekwe uhamishoni kwenye kisiwa kilichoogopwa sana ambacho kilitumiwa kama gereza la mateso huko Makrónisos (Makronisi).

KISIWA CHA MATESO

Kisiwa cha Makrónisos kilikuwa kikavu, chenye jua kali, na hali ngumu, kilikuwa juu ya mwamba kwenye eneo la pwani ya Attica, kilomita 50 hivi kutoka Athene. Kisiwa hicho kina urefu wa kilomita 13, na sehemu pana zaidi ya kisiwa hicho ni kilomita mbili na nusu. Lakini tangu 1947 hadi 1958, kilikuwa na wafungwa zaidi ya 100,000, kutia ndani wakomunisti na walioshukiwa kuwa wakomunisti, wapiganaji waasi, na idadi kubwa ya Mashahidi wa Yehova waaminifu.

Nilipowasili huko mapema mwaka 1949, wafungwa walikuwa wamegawanywa katika kambi kadhaa. Niliwekwa katika kambi isiyo na ulinzi mkali pamoja na wanaume wengine wengi. Watu 40 hivi kati yetu walilala ardhini ndani ya hema ambalo lilikusudiwa kutoshea watu 10. Tulikunywa maji machafu na mara nyingi tukala dengu na biringanya. Vumbi na upepo uliovuma kwa kuendelea ulifanya maisha yawe magumu. Angalau hatukuhitajika kusukuma mawe makubwa kutoka upande mmoja wa kisiwa hadi mwingine tena na tena, mateso ya kinyama ambayo yaliwaumiza wafungwa wengi kiakili na kimwili.

Nikiwa na Mashahidi wengine wakiwa uhamishoni kwenye Kisiwa cha Makrónisos

Siku moja nilipokuwa nikitembea ufuoni, nilikutana na Mashahidi kadhaa kutoka katika kambi nyingine. Tulifurahi sana kuonana! Tulijihadhari sana tusijulikane, hivyo tulikutana ilipowezekana. Pia, tuliwahubiria kwa busara wafungwa wengine, na baadhi yao baadaye wakawa Mashahidi wa Yehova. Kufanya hivyo na kusali kutoka moyoni kulitusaidia kubaki imara kiroho.

TANURU YA MOTO

Baada ya “kurekebishwa” kwa miezi kumi, walionikamata waliamua kwamba wakati wangu ulikuwa umefika wa kuvaa mavazi ya kijeshi. Nilipokataa, waliniburuza hadi kwa mkuu wa kambi. Nilimpa mwanamume huyo hati iliyoandikwa hivi: “Nataka tu kuwa askari-jeshi wa Kristo.” Baada ya kunitisha, mkuu wa kambi alinipeleka kwa makamu wake, aliyekuwa askofu mkuu wa kanisa Othodoksi la Ugiriki, ambaye alikuwa amevaa mavazi kamili ya askofu. Nilipojibu maswali yake kwa ujasiri nikitumia Maandiko, alisema hivi akiwa amekasirika: “Mwondoeni hapa. Ana msimamo mkali wa kidini!”

Asubuhi iliyofuata, wanajeshi hao waliniamuru tena nivae mavazi ya kijeshi. Nilipokataa, walinipiga ngumi na vilevile kwa kutumia fimbo ya mbao. Kisha wakanipeleka kwenye hospitali ya kambi ili kuhakikisha ikiwa mifupa yangu ilikuwa imevunjika au la, na baada ya hapo wakaniburuza hadi kambini. Walifanya hivyo kila siku kwa miezi miwili.

Kwa kuwa sikulegeza msimamo, wanajeshi hao ambao walikuwa wamekata tamaa walijaribu mbinu nyingine. Walinifunga mikono nyuma ya mgongo, na kunipiga nyayo bila huruma kwa kutumia kamba. Huku nikihisi maumivu makali, nilikumbuka maneno haya ya Yesu: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa . . . Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwa kabla yenu.” (Mt. 5:11, 12) Mwishowe, baada ya kuteswa kwa muda mrefu, nilipoteza fahamu.

Nilipopata fahamu, nilijikuta kwenye seli yenye baridi kali, bila mkate, maji, au blanketi. Ingawa hivyo, nilihisi nikiwa na utulivu na amani. Kama Biblia inavyoahidi, “amani ya Mungu” ilikuwa ‘ikilinda moyo wangu na nguvu zangu za akili.’ (Flp. 4:7) Siku iliyofuata, mwanajeshi mwenye fadhili alinipa mkate, maji, na koti. Pia, mwanajeshi mwingine alinipa chakula chake. Kupitia njia hiyo na nyingine nyingi, nilihisi kwamba Yehova ananitunza.

Wenye mamlaka waliniona kuwa mwasi asiyeweza kubadilika na kunipeleka Athene mbele ya mahakama ya kijeshi. Nilihukumiwa kifungo cha miaka mitatu kwenye gereza la Yíaros (Gyaros), kisiwa kilicho kilomita 50 hivi mashariki mwa Makrónisos.

“TUNAWEZA KUWAAMINI”

Gereza lenye ulinzi mkali la Yíaros lilikuwa jengo kubwa la matofali mekundu na lilikuwa na wafungwa zaidi ya 5,000 wa kisiasa. Kulikuwa na Mashahidi wa Yehova saba waliokuwa wamefungwa kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote. Ijapokuwa ilikuwa imekatazwa kabisa kukutana, sote saba tulikutana kisiri ili kujifunza Biblia. Pia, tulipokea kwa ukawaida nakala za Mnara wa Mlinzi zilizoingizwa kisiri gerezani, kisha tulizinakili ili tuzitumie tulipojifunza.

Siku moja, tulipokuwa tukijifunza kisiri, mlinzi wa gereza aliingia ghafula na kuchukua machapisho yetu. Tulipelekwa kwenye ofisi ya makamu wa gereza hilo. Tulikuwa na uhakika kabisa kwamba kifungo chetu kingeongezwa. Badala yake, makamu wa gereza alisema hivi: “Tunawajua, na tunaheshimu msimamo wenu. Tunajua tunaweza kuwaamini. Rudini kazini.” Hata aliwapa baadhi yetu kazi rahisi. Mioyo yetu ilijaa shukrani. Hata tukiwa gerezani utimilifu wetu wa Kikristo ulimletea Yehova sifa.

Ushikamanifu wetu ulikuwa na matokeo mengine mazuri. Baada ya kuchunguza kwa ukaribu mwenendo wetu mzuri, mfungwa fulani aliyekuwa profesa wa hisabati alichochewa kuuliza maswali kuhusu imani yetu. Mashahidi walipoachiliwa mapema katika 1951, yeye pia aliachiliwa. Baadaye, alikuwa Shahidi na mtumishi wa wakati wote.

BADO MIMI NI ASKARI-JESHI

Nikiwa na mke wangu, Janette

Nilipoachiliwa huru, nilirudi nyumbani huko Karítsa. Baadaye, mimi pamoja na raia wengine wengi, tulihamia Melbourne, Australia. Huko, nilikutana na Janette, dada Mkristo mwenye sifa nzuri, tukafunga ndoa, na kulea mwana na mabinti watatu katika njia ya Kikristo.

Leo, nina umri wa zaidi ya miaka 90, na bado natumikia nikiwa mzee wa kutaniko. Kwa sababu ya majeraha yangu ya zamani, mwili wangu na miguu huwa na maumivu nyakati nyingine, hasa baada ya kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, nimeazimia kuendelea kuwa “askari-jeshi . . . wa Kristo.”2 Tim. 2:3.