Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 36

Har–Magedoni Ni Habari Njema!

Har–Magedoni Ni Habari Njema!

“Nayo yakawakusanya pamoja . . . Har–Magedoni.”​—UFU. 16:16.

WIMBO 150 Mtafute Mungu Upate Ukombozi

MUHTASARI *

1-2. (a) Kwa nini Har–Magedoni ni habari njema kwa wanadamu? (b) Tutachunguza maswali gani katika makala hii?

JE, UMEWAHI kusikia watu wakitumia neno “Har–Magedoni” kurejelea vita vya nyuklia au janga kubwa la uharibifu wa mazingira? Tofauti na maoni hayo, yale ambayo Biblia inasema kuhusu Har–Magedoni ni habari njema inayotupatia sababu ya kushangilia! (Ufu. 1:3) Vita vya Har–Magedoni vitawaokoa wanadamu, si kuwaangamiza! Jinsi gani?

2 Biblia inaonyesha kwamba vita vya Har–Magedoni vitawaokoa wanadamu kwa kukomesha utawala wa wanadamu. Vita hivyo vitawaokoa wanadamu kwa kuondoa waovu na kuwahifadhi hai waadilifu. Na vitawaokoa wanadamu kwa kuilinda sayari yetu isiharibiwe. (Ufu. 11:18) Ili kutusaidia kuelewa vizuri zaidi mambo hayo, acheni tuchunguze maswali manne: Har–Magedoni ni nini? Ni matukio gani yatakayotangulia Har–Magedoni? Tunaweza kufanya nini ili tuwe miongoni mwa wale watakaookolewa wakati wa Har–Magedoni? Tunaweza kuendeleaje kuwa waaminifu kadiri Har–Magedoni inavyokaribia?

HAR-MAGEDONI NI NINI?

3. (a) Neno “Har–Magedoni” linamaanisha nini? (b) Kulingana na Ufunuo 16:14, 16, kwa nini tunaweza kusema kwamba Har–Magedoni si mahali halisi?

3 Soma Ufunuo 16:14, 16. Neno “Har–Magedoni” linapatikana mara moja tu katika Maandiko, na linatokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “Mlima wa Megido.” (Ufu. 16:16; maelezo ya chini) Megido lilikuwa jiji katika Israeli la kale. (Yos. 17:11) Hata hivyo, neno Har–Magedoni halirejelei eneo halisi duniani. Kihususa, linarejelea hali ambayo “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” wanakusanywa ili kumpinga Yehova. (Ufu. 16:14) Hata hivyo katika makala hii, tutatumia neno “Har–Magedoni” kurejelea vita itakayoanza punde tu baada ya wafalme hao wa dunia kukusanywa. Tunajuaje kwamba neno “Har–Magedoni” linarejelea mahali pa mfano? Kwanza, hakuna mlima halisi wa Megido. Pili, eneo la Megido ni dogo sana na haliwezi kuwatosha “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” na majeshi yao na silaha zao za vita. Tatu, kama tutakavyoona katika makala hii, vita vya Har–Magedoni vitaanza wakati “wafalme” wa dunia watakapowashambulia watu wa Mungu ambao wametawanyika kotekote duniani.

4. Kwa nini Mungu alihusianisha vita vyake vikuu vya mwisho na neno Megido?

4 Kwa nini Yehova alihusianisha vita vikuu vya mwisho na neno Megido? Eneo la Megido na Bonde la Yezreeli lililo karibu, yalikuwa maeneo ambapo vita vingi vilipiganwa. Pindi fulani, Yehova aliwasaidia moja kwa moja watu wake katika vita hivyo. Kwa mfano, “kando ya maji ya Megido,” Mungu alimsaidia mwamuzi Mwisraeli Baraka kulishinda jeshi la Wakanaani lililoongozwa na mkuu wa jeshi aliyeitwa Sisera. Baraka na nabii wa kike Debora walimshukuru Yehova kwa ushindi huo waliopata kimuujiza. Waliimba hivi: “Kutoka mbinguni nyota zilipigana . . . na Sisera. Mafuriko ya Kishoni yaliwafagilia mbali.”—Amu. 5:19-21.

5. Kuna tofauti gani muhimu kati ya vita vya Har–Magedoni na vita vilivyopiganwa na Baraka?

5 Baraka na Debora walimalizia wimbo wao kwa maneno haya: “Maadui wako wote na waangamie, Ee Yehova, lakini wanaokupenda na wawe kama jua linalochomoza katika utukufu wake.” (Amu. 5:31) Katika vita vya Har–Magedoni pia, maadui wa Mungu wataangamia, lakini wale wanaompenda Mungu wataokolewa. Hata hivyo, kuna tofauti moja muhimu kati ya vita hivyo viwili. Katika vita vya Har–Magedoni, watu wa Mungu hawatapigana. Wala hawatabeba silaha! ‘Watakuwa na nguvu wakiendelea kuwa watulivu na kuwa na tumaini’ katika Yehova na majeshi yake ya mbinguni.—Isa. 30:15; Ufu. 19:11-15.

6. Huenda Yehova akatumia njia gani kuwashinda maadui wake katika vita vya Har–Magedoni?

6 Mungu atawashindaje maadui wake katika vita vya Har–Magedoni? Huenda akatumia njia mbalimbali. Kwa mfano, huenda akatumia matetemeko ya ardhi, mvua ya mawe, na radi. (Ayu. 38:22, 23; Eze. 38:19-22) Huenda akawafanya adui zake waangamizane wao kwa wao. (2 Nya. 20:17, 22, 23) Na huenda akatumia malaika wake kuwaangamiza waovu. (Isa. 37:36) Hata iwe Mungu atatumia njia gani, ushindi wake ni hakika. Maadui wake wote wataangamizwa. Na waadilifu wote wataokolewa.—Met. 3:25, 26.

NI MATUKIO GANI YATAKAYOTANGULIA HAR-MAGEDONI?

7-8. (a) Kulingana na 1 Wathesalonike 5:1-6, watawala wa ulimwengu watatangaza tangazo gani lisilo la kawaida? (b) Kwa nini tangazo hilo litakuwa uwongo hatari sana?

7 Tangazo la “amani na usalama” litatolewa kabla ya “siku ya Yehova.” (Soma 1 Wathesalonike 5:1-6.) Kwenye 1 Wathesalonike 5:2, “siku ya Yehova” inarejelea “dhiki kuu.” (Ufu. 7:14) Tutajuaje kwamba dhiki hiyo iko karibu kuanza? Biblia inatueleza kuhusu tangazo lisilo la kawaida kabisa. Tangazo hilo litakuwa ishara inayoonyesha kwamba dhiki kuu iko karibu kuanza.

8 Hilo ndilo lile tangazo la “amani na usalama” lililotabiriwa mapema. Kwa nini watawala wa ulimwengu watatoa tangazo hilo? Je, viongozi wa dini watahusika pia? Inawezekana. Hata hivyo, tangazo hilo litakuwa tu uwongo mwingine unaoenezwa na roho waovu. Lakini uwongo huo utakuwa hatari sana, hasa kwa sababu utawafanya watu wahisi kimakosa kwamba wako salama kabla tu ya kuanza kwa dhiki kuu kuliko zote katika historia ya wanadamu. Naam, “uharibifu wa ghafla [utawapata] mara moja, kama vile maumivu ya kuzaa ya mwanamke mwenye mimba.” Namna gani kuhusu watumishi washikamanifu wa Yehova? Huenda watashtuka kwa sababu siku ya Yehova itaanza ghafla, lakini watakuwa tayari.

9. Mungu atauharibu ulimwengu wa Shetani jinsi gani?

9 Yehova hatauangamiza ulimwengu wote wa Shetani papo hapo kama alivyofanya katika siku za Noa. Badala yake, atauangamiza katika hatua mbili kuu. Kwanza, atamharibu Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo. Kisha, wakati wa Har–Magedoni, ataharibu sehemu iliyobaki ya ulimwengu wa Shetani, kutia ndani mifumo yake ya kisiasa, kijeshi, na kibiashara. Acheni tuchunguze kwa makini zaidi matukio hayo mawili makubwa.

10. Kulingana na Ufunuo 17:1, 6, na 18:24, kwa nini Yehova atamharibu Babiloni Mkubwa?

10 “Hukumu dhidi ya yule kahaba mkubwa.” (Soma Ufunuo 17:1, 6; 18:24.) Babiloni mkubwa ameliletea suto kubwa jina la Mungu. Amefundisha uwongo kumhusu Mungu. Amefanya ukahaba wa kiroho kwa kushirikiana na watawala wa dunia. Ametumia nguvu na ushawishi wake kuwadhulumu kondoo wake. Na amemwaga damu nyingi, kutia ndani damu ya watumishi wa Mungu. (Ufu. 19:2) Yehova atamharibu jinsi gani Babiloni Mkubwa?

11. “Mnyama wa mwituni mwenye rangi nyekundu” ni nani, naye atatumiwaje kutimiza kusudi la Mungu dhidi ya Babiloni Mkubwa?

11 Yehova atamharibu “yule kahaba mkubwa” kwa kutumia zile “pembe kumi” za “mnyama wa mwituni mwenye rangi nyekundu.” Mnyama huyo wa mwituni anafananisha shirika la Umoja wa Mataifa. Zile pembe kumi zinafananisha serikali za ulimwengu zinazounga mkono shirika hilo. Katika wakati uliowekwa wa Mungu, serikali hizo zitamshambulia Babiloni Mkubwa. Watamfanya “kuwa ukiwa na uchi” kwa kupora utajiri wake na kufunua uovu wake. (Ufu. 17:3, 16) Uharibifu huo utakuja ghafla—kana kwamba ni katika siku moja—na utawashtua wale wote waliomuunga mkono. Kwa maana, amekuwa akijigamba hivi: “Ninaketi nikiwa malkia, mimi si mjane, nami sitaona maombolezo kamwe.”—Ufu. 18:7, 8.

12. Yehova hatayaruhusu mataifa yafanye nini, na kwa nini?

12 Mungu hatayaruhusu mataifa yawaharibu watu wake. Wanajivunia kuitwa kwa jina lake, nao wametii amri yake na kutoka kwa Babiloni Mkubwa. (Mdo. 15:16, 17; Ufu. 18:4) Pia, wamefanya kazi kwa bidii kuwasaidia wengine watoke kwa Babiloni Mkubwa. Hivyo, watumishi wa Yehova ‘hawatapokea sehemu ya mapigo yake.’ Hata hivyo, imani yao itajaribiwa.

Popote walipo duniani, watu wa Mungu watamtumaini watakapoanza kushambuliwa (Tazama fungu la 13) *

13. (a) Gogu ni nani? (b) Kulingana na Ezekieli 38:2, 8, 9, ni nini kitakachomfanya Gogu awashambulie watu wa Mungu?

13 Shambulizi la Gogu. (Soma Ezekieli 38:2, 8, 9.) Baada ya mashirika yote ya dini za uwongo kuharibiwa, kutakuwa na dini moja tu duniani, watu wa Mungu watabaki kama mti pekee ulioponyoka uharibifu wa dhoruba kali. Bila shaka, Shetani atakasirika sana. Ataonyesha hasira yake kwa kutumia propaganda za roho waovu, yaani, ‘maneno machafu yaliyoongozwa na roho’—kuchochea muungano wa mataifa kuwashambulia watumishi wa Yehova. (Ufu. 16:13, 14) Muungano huo unaitwa “Gogu wa nchi ya Magogu.” Mataifa hayo yatakapoanza shambulizi lao dhidi ya watu wa Yehova, ndipo vita vya Har–Magedoni vitakapoanza.—Ufu. 16:16.

14. Gogu atatambua nini?

14 Gogu atautumaini ‘mkono wake wa nyama’, yaani, nguvu zake za kijeshi. (2 Nya. 32:8) Sisi tutamtumaini Yehova, Mungu wetu—msimamo ambao kwa mataifa utaonekana kuwa wa kipumbavu. Kwa maana, miungu ya Babiloni Mkubwa mwenye nguvu haikumwokoa kutokana na yule “mnyama wa mwituni” na ‘pembe zake kumi’! (Ufu. 17:16) Kwa hiyo, Gogu atatarajia kushinda kirahisi. “Kama mawingu yanayoifunika nchi,” atawashambulia watu wa Yehova. (Eze. 38:16) Lakini haraka Gogu atatambua kwamba ameingia kwenye mtego. Kama ilivyokuwa kwa Farao katika Bahari Nyekundu, punde si punde Gogu atatambua kwamba anapigana na Yehova.—Kut. 14:1-4; Eze. 38:3, 4, 18, 21-23.

15. Kristo atakamilisha ushindi wake jinsi gani?

15 Akiwa pamoja na majeshi yake ya mbinguni, Kristo atawalinda watu wa Mungu na kumwangamiza Gogu na majeshi yake. (Ufu. 19:11, 14, 15) Lakini vipi kuhusu Shetani, adui mkuu wa Yehova, ambaye propaganda zake za uwongo ziliyaongoza mataifa kwenye Har–Magedoni? Yesu atamtupa yeye pamoja na roho wake waovu katika shimo refu lisilo na mwisho, ambamo watafungwa kwa miaka elfu moja.—Ufu. 20:1-3.

UNAWEZA KUFANYA NINI ILI UOKOLEWE WAKATI WA HAR-MAGEDONI?

16. (a) Tunaonyeshaje kwamba ‘tunamjua Mungu’? (b) Kwa nini kumjua Yehova kutathibitika kuwa baraka wakati wa Har–Magedoni?

16 Iwe tumekuwa katika kweli kwa miaka mingi au la, ili tuokolewe katika Har–Magedoni ni lazima tuonyeshe kwamba ‘tunamjua Mungu’ na ‘tunatii habari njema kumhusu Bwana wetu Yesu.’ (2 The. 1:7-9) ‘Tunamjua Mungu’ kwa kujua mambo anayopenda, anayochukia, na pia viwango vyake. Pia, tunaonyesha kwamba tunamjua tunapompenda na kumtii na kumwabudu yeye peke yake. (1 Yoh. 2:3-5; 5:3) Tunapoonyesha kwamba tunamjua Mungu, tunapata pendeleo la ‘kujulikana naye,’ jambo litakalofanya tuokolewe wakati wa Har–Magedoni! (1 Kor. 8:3) Kwa nini? Kwa sababu ‘kujulikana naye’ kunamaanisha kuwa na kibali chake.

17. Kutii “habari njema kumhusu Bwana wetu Yesu” kunamaanisha nini?

17 “Habari njema kumhusu Bwana wetu Yesu” inatia ndani kweli zote ambazo Yesu alifundisha, zinazopatikana katika Neno la Mungu. Tunaonyesha kwamba tunatii habari njema tunapoitumia maishani mwetu. Utii huo unahusisha kutanguliza kwanza masilahi ya Ufalme, kuishi kulingana na viwango vya Mungu vya uadilifu, na kuutangaza Ufalme wa Mungu. (Mt. 6:33; 24:14) Pia, unahusisha kuwaunga mkono ndugu za Kristo watiwa-mafuta wanapotimiza majukumu mazito waliyo nayo.—Mt. 25:31-40.

18. Ndugu za Kristo watiwa-mafuta watawaonyeshaje “kondoo wengine” fadhili ambazo waliwaonyesha?

18 Hivi karibuni, watumishi wa Mungu watiwa-mafuta watalipa fadhili ambazo “kondoo wengine” waliwaonyesha. (Yoh. 10:16) Jinsi gani? Kabla ya vita vya Har–Magedoni kuanza, idadi kamili ya wale 144,000 watakuwa wamefufuliwa na kwenda mbinguni wakiwa viumbe wa roho wasioweza kufa. Watakuwa sehemu ya majeshi ya mbinguni yatakayomponda Gogu na kuulinda “umati mkubwa” wa watu walio mfano wa kondoo. (Ufu. 2:26, 27; 7:9, 10) Naam, umati mkubwa utafurahi kwelikweli kwamba walipata pendeleo la kuwaunga mkono watumishi wa Yehova watiwa-mafuta walipokuwa wangali duniani!

TUNAWEZA KUENDELEAJE KUWA WAAMINIFU KADIRI MWISHO UNAVYOKARIBIA?

19-20. Licha ya majaribu tunayokabili, tunaweza kuendeleaje kuwa waaminifu kadiri Har–Magedoni inavyokaribia?

19 Katika siku hizi za mwisho zilizo ngumu, watu wengi wa Yehova wanakabili majaribu mbalimbali. Hata hivyo, tunaweza kuvumilia kwa shangwe. (Yak. 1:2-4) Siri ni kudumu katika sala. (Luka 21:36) Mbali na kusali, ni lazima pia tujifunze Neno la Mungu kila siku na kulitafakari, kutia ndani unabii mbalimbali wenye kusisimua unaohusu nyakati zetu. (Zab. 77:12) Kufanya mambo hayo, pamoja na kushiriki kikamili katika huduma, kutafanya imani yetu iendelee kuwa na nguvu na tumaini letu lizidi kuwa halisi!

20 Wazia jinsi utakavyosisimka Babiloni Mkubwa atakapoangamizwa na vita vya Har–Magedoni vitakapokuwa vimekoma! Jambo muhimu hata zaidi, wazia jinsi utakavyokuwa na furaha isiyo na kipimo wakati jina la Mungu na enzi yake kuu itakapokuwa imetetewa kikamili! (Eze. 38:23) Naam, Har–Magedoni ni habari njema kwa wale wanaomjua Mungu, wanaomtii Mwana wake, na kuvumilia mpaka mwisho.—Mt. 24:13.

WIMBO 143 Endeleeni Kufanya Kazi, Kesheni na Kusubiri

^ fu. 5 Watu wa Yehova wamekuwa wakisubiri Har–Magedoni kwa muda mrefu. Katika makala hii, tutazungumzia Har–Magedoni ni nini, ni matukio gani yatakayoitangulia, na jinsi tunavyoweza kuendelea kuwa waaminifu kadiri mwisho unavyokaribia.

^ fu. 71 MAELEZO YA PICHA: Matukio yenye kusisimua yatakapotokea, tutaendelea (1) kushiriki katika huduma kadiri hali zinavyoruhusu, (2) kudumisha ratiba yetu ya kujifunza, na (3) kutumaini ulinzi wa Mungu.

^ fu. 85 MAELEZO YA PICHA: Polisi wanajitayarisha kuvamia nyumba ya familia moja ya Kikristo ambayo ina hakika kwamba Yesu pamoja na malaika wake wanajua kinachoendelea.