Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JINSI YA KUFAIDIKA ZAIDI UNAPOSOMA BIBLIA

Kwa Nini Nisome Biblia?

Kwa Nini Nisome Biblia?

“Nilifikiri kwamba Biblia ni ngumu sana kuielewa.”​—Jovy

“Nilihisi kwamba kusoma Biblia kunachosha.”​—Queennie

“Nilipotazama ukubwa wa Biblia, nilikosa kabisa hamu ya kuisoma.”​—Ezekiel

Je, umewahi kuhisi kama watu waliotajwa hapo juu kuhusu kusoma Biblia? Kwa watu wengi, kusoma Biblia kunaoneka kuwa jambo lenye kuchosha. Lakini namna gani ukijua kwamba Biblia inaweza kukusaidia kuwa na maisha yenye furaha na ya kuridhisha zaidi? Na vipi ukijua kwamba kuna mambo unayoweza kufanya ili ufurahie zaidi kuisoma Biblia? Je, utakuwa tayari kuisoma na kuona jinsi inavyoweza kukunufaisha?

Chunguza maelezo machache ya wale ambao wamefaidika kwa kuisoma Biblia.

Ezekiel, mwenye umri wa miaka 20 hivi anasema: “Zamani, nilikuwa kama mtu anayeendesha gari bila kujua mahali hususa anakoenda. Lakini kusoma Biblia kumenisaidia kupata kusudi la maisha. Biblia ina ushauri unaofaa ninaotumia kila siku.”

Frieda, mwenye umri wa miaka 20 hivi anaeleza: “Nilikuwa mwenye hasira. Lakini kwa sababu ya kuisoma Biblia, nimejifunza jinsi ya kujidhibiti. Hilo limefanya iwe rahisi kwangu kupatana na wengine, na sasa nimekuwa na marafiki wengi.”

Eunice, mwanamke mwenye umri wa miaka 50 hivi, alisema: “Biblia inanisaidia kuboresha utu wangu, na imenisaidia kuacha mazoea fulani mabaya.”

Wasomaji hao pamoja na mamilioni ya watu wengine wamejifunza kwamba kusoma Biblia kunaweza kukusaidia uwe na maisha yenye furaha zaidi. (Isaya 48:17, 18) Miongoni mwa faida unazoweza kupata kwa kusoma Biblia ni (1) kufanya maamuzi mazuri, (2) kupata marafiki wa kweli, (3) kushughulika na mkazo kwa njia nzuri, na (4) muhimu zaidi, kujifunza ukweli kumhusu Mungu. Ushauri wa Biblia unatoka kwa Mungu, kwa hiyo huwezi kupata hasara kwa kuufuata. Mungu hawezi kamwe kutoa ushauri mbaya.

Jambo muhimu ni kujua jinsi unavyoweza kuanza kusoma. Ni mapendekezo gani unayoweza kutumia ili uweze kuanza kusoma Biblia na kufurahia usomaji wako?