Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JINSI YA KUFAIDIKA ZAIDI UNAPOSOMA BIBLIA

Biblia Inawezaje Kuboresha Maisha Yangu?

Biblia Inawezaje Kuboresha Maisha Yangu?

Biblia si kitabu cha kawaida tu. Ni kitabu chenye mashauri kutoka Muumba wetu. (2 Timotheo 3:16) Ujumbe wake unaweza kutunufaisha sana. Kwa kweli, Biblia yenyewe inasema hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.” (Waebrania 4:12) Ina nguvu za kuboresha maisha yetu katika njia kuu mbili. Kwanza, inatoa mwongozo wa maisha ya kila siku, na pili inatusaidia kumjua Mungu na ahadi zake.—1 Timotheo 4:8; Yakobo 4:8.

Jinsi inavyoweza kuboresha maisha yako sasa. Biblia inaweza kukusaidia hata katika mambo ya kibinafsi, kwa kuwa inatoa mwongozo unaofaa kuhusu mambo yafuatayo.

Wenzi fulani wa ndoa waliooana hivi karibuni huko Asia wamefaidika sana na ushauri wa Biblia wenye thamani. Kama ilivyo kwa wenzi wengi wapya, wao walikuwa wakipambana kurekebisha tofauti zao za utu na kuboresha mawasiliano. Hivyo, waliamua kuanza kutumia yale waliyojifunza katika Biblia. Walipata matokeo gani? Vicent, ambaye ni mume katika familia hiyo alisema hivi: “Mambo niliyojifunza katika Biblia yamenisaidia kushugulikia changamoto za ndoa yetu kwa upendo. Kuishi kulingana na Biblia kumetusaidia kuwa na maisha yenye furaha.” Mke wake, Annalou, anakubaliana naye. Anasema hivi: “Kusoma mifano inayotajwa katika Biblia kumetusaidia. Sasa nina furaha na nimeridhika na hali ya ndoa na malengo yetu maishani.”

Kumjua Mungu. Mbali na kueleza kuhusu ndoa, Vicent alisema hivi pia: “Kusoma Biblia, kunafanya nijihisi nikiwa karibu zaidi na Yehova.” Maelezo ya Vicent yanakazia kwamba Biblia inaweza kukusaidia umjue Mungu vizuri. Kwa kufanya hivyo, utanufaika na ushauri wake, na jambo muhimu zaidi ni kwamba utakuwa rafiki yake. Nawe utajifunza kwamba Mungu anaeleza kuhusu wakati ujao ulio mzuri, ambao tutafurahia “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima wa milele. (1 Timotheo 6:19) Hilo ni tumaini zuri sana ambalo huwezi kulipata katika kitabu kingine chochote.

Ukiendelea kusoma Biblia kwa ukawaida, wewe pia utapata faida hizo, yaani, utaboresha maisha yako na utamjua Mungu vizuri. Hata hivyo, unaposoma Biblia, huenda ukajiuliza maswali mengi. Ukikabili hali hiyo, kumbuka mfano mzuri wa ofisa Mwethiopia aliyeishi miaka 2,000 hivi iliyopita. Alikuwa na maswali mengi kuhusu Biblia. Kwa hiyo, alipoulizwa ikiwa anaelewa mambo anayosoma, alijibu hivi: “Kwa kweli, ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” * Kisha, bila kusita akakubali msaada kutoka kwa Filipo, mwalimu mzuri wa Biblia, ambaye alikuwa mwanafunzi wa Yesu. (Matendo 8:30, 31, 34) Vivyo hivyo, ikiwa unapenda kujua mengi kuhusu Biblia, tunakualika utume ombi lako kwenye mtandao kupitia www.dan124.com/sw au kupitia anwani zilizo kwenye gazeti hili. Unaweza pia kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova au kutembelea Jumba la Ufalme lililo jirani na mahali unakoishi. Je, unaweza kuanza kusoma Biblia leo? Ukifanya hivyo, Biblia itakuongoza kwenye maisha bora sana!

Ikiwa una shaka kama unaweza kuitumaini Biblia, tafadhali tazama video fupi yenye kichwa, Tunawezaje Kuwa na Hakika Kwamba Yale Yaliyoandikwa Katika Biblia Ni ya Kweli? Unaweza kuipata katika tovuti ya jw.org/sw, kisha, bofya kitufe cha Kutafuta, na uingize jina la video hiyo

^ fu. 8 Ili kupata habari zaidi kuhusu ushauri wa Biblia, tembelea tovuti yetu ya, jw.org/sw. Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MAJIBU YA MASWALI YA BIBLIA.

^ fu. 11 Pia, soma makala kwenye gazeti hili yenye kichwa “Kuelewa Maandiko Kimakosa, Je, Ni Tatizo Dogo?