Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwasaidia Watu Wenye Ugonjwa wa Akili

Jinsi ya Kuwasaidia Watu Wenye Ugonjwa wa Akili

BIBLIA INASEMA HIVI: “Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”​—METHALI 17:17.

Inamaanisha Nini?

Huenda tukahisi hatuwezi kumsaidia rafiki yetu anapougua ugonjwa wa akili. Lakini tunaweza kumwonyesha jinsi tunavyomjali kwa kumsaidia akabiliane na ugonjwa wake. Jinsi gani?

Hilo Linaweza Kutusaidiaje?

‘Uwe mwepesi wa kusikia.’​—YAKOBO 1:19.

Mojawapo ya njia bora za kumsaidia rafiki yetu ni kumsikiliza anapotaka kuzungumza. Usihisi kwamba unapaswa kujibu kila jambo analosema. Mwambie unamsikiliza na kumjali. Jitahidi kuelewa hisia zake na usimhukumu. Kumbuka anaweza kusema mambo ambayo hakutaka kusema na huenda baadaye akajutia.​—Ayubu 6:2, 3.

“Wafarijini.” —1 WATHESALONIKE 5:14.

Rafiki yako anaweza kuwa na mahangaiko, au akahisi hana thamani yoyote. Kwa kumhakikishia kwamba unamjali unaweza kumfariji na kumtia moyo, hata kama hujui jambo hususa la kumwambia.

“Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote.”​—METHALI 17:17.

Toa msaada hususa. Muulize anahitaji msaada gani, badala ya kuhisi tu unajua jinsi ya kumsaidia. Ikiwa ni vigumu kwa rafiki yako kukwambia mambo anayohitaji, mpendekezee mambo ambayo mnaweza kufanya pamoja, kama vile, kutembea. Au unaweza kujitolea kwenda kumnunulia vitu, kufanya usafi, au shughuli nyingine yoyote.​—Wagalatia 6:2.

‘Uwe na subira.’​—1 WATHESALONIKE 5:14.

Huenda si kila wakati rafiki yako akataka kuzungumza. Mhakikishie rafiki yako kwamba utakuwa tayari kumsikiliza atakapotaka kuongea. Kwa sababu ya ugonjwa wake, rafiki yako anaweza kusema au kufanya mambo yatakayokuumiza. Anaweza kuvunja mipango au kukasirika. Uwe na subira na utambuzi unapomsaidia.​—Methali 18:24.

Utegemezo Wako Unaweza Kumsaidia Rafiki Yako

“Nimemhakikishia kwamba mimi ni rafiki anayeweza kumtumaini. Ingawa sina suluhisho la matatizo yake, ninamsikiliza kwa makini anapozungumza. Wakati mwingine anahitaji tu mtu wa kumsikiliza ili ahisi vizuri.”​—Farrah, a ambaye rafiki yake anaugua ugonjwa wa kujinyima chakula, mahangaiko na kushuka moyo sana.

“Nina rafiki mwenye fadhili na anayenitia moyo. Alinikaribisha nyumbani kwake tule chakula kitamu pamoja. Alinionyesha upendo sana na akafanya iwe rahisi kwangu kumweleza hisia zangu. Jambo hilo lilinitia moyo sana!”​—Ha-eun, mwenye ugonjwa wa kushuka moyo sana.

“Subira ni sifa muhimu sana. Mke wangu anaponikasirisha, mimi hukumbuka kwamba ni ugonjwa wake unafanya atende hivyo wala si utu wake. Hilo hunisaidia nisikasirike na kuwa mwenye ufikirio.”​—Jacob, ambaye mke wake anaugua ugonjwa wa kushuka moyo sana.

“Mke wangu amenifariji na kunisaidia sana. Ninapokuwa na mahangaiko mengi, hanilazimishi kufanya jambo ambalo sitaki kufanya. Wakati mwingine hilo humaanisha hawezi kufanya jambo ambalo anapenda. Yeye ni mtu muhimu sana kwangu kwa sababu ni mkarimu na hana ubinafsi.”​—Enrico, anayeugua ugonjwa wa kuwa na wasiwasi kupita kiasi (anxiety disorder).

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.