Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tunazeeka na Kufa?

Kwa Nini Tunazeeka na Kufa?

MUNGU hakukusudia wanadamu wawe wakifa. Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, waliumbwa bila kasoro yoyote kwenye mwili na akili; wangekuwa hai hadi leo. Maneno ambayo Yehova alimwambia Adamu kuhusu mti fulani uliokuwa kwenye bustani ya Edeni yanathibitisha jambo hilo.

Mungu alimwambia Adamu: “Siku utakapokula matunda [ya mti huo] hakika utakufa.” (Mwanzo 2:17) Sheria hiyo haingekuwa na maana yoyote ikiwa Mungu alikusudia baadaye Adamu azeeke na kufa. Adamu alielewa vizuri kwamba ikiwa hangekula matunda ya mti huo, angeendelea kuwa hai.

MUNGU HAKUKUSUDIA WANADAMU WAWE WAKIFA

Maisha ya Adamu na Hawa hayakutegemea matunda ya mti huo—bustani ilikuwa na miti mingi ya matunda. (Mwanzo 2:9) Kutokula matunda ya mti huo mmoja kungeonyesha kwamba wanamtii Yule aliyewapa uhai. Pia, kungeonyesha kwamba wanatambua haki ya Mungu ya kuwaongoza.

KWA NINI ADAMU NA HAWA WALIKUFA?

Ili kuelewa ni kwa nini Adamu na Hawa walikufa, tunahitaji kuchunguza mazungumzo fulani ambayo madhara yake tunayaona hadi leo. Shetani Ibilisi alimtumia nyoka kusema uwongo mbaya sana. Simulizi la Biblia linasema: “Basi nyoka alikuwa mwenye kujihadhari kuliko wanyama wote wa mwituni walioumbwa na Yehova Mungu. Kwa hiyo, akamuuliza mwanamke: ‘Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?’”—Mwanzo 3:1.

Hawa akamjibu: “Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani. Lakini Mungu amesema hivi kuhusu matunda ya mti ulio katikati ya bustani: ‘Msiyale, wala msiyaguse; la sivyo mtakufa.’” Kisha nyoka akamwambia Hawa: “Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunguliwa nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” Kwa maneno hayo, Shetani alimaanisha kwamba Yehova ni mwongo na alikuwa akiwanyima wazazi wetu kitu fulani kizuri.—Mwanzo 3:2-5.

Hawa aliamini kile alichosikia. Akauangalia ule mti. Akaona kwamba matunda yake ni yenye kuvutia sana; yanatamanisha! Akanyoosha mkono, akachuma matunda ya mti huo, na kuanza kula. Biblia inaendelea kusema: “Baadaye, akampa pia mume wake baadhi ya matunda hayo alipokuwa pamoja naye, naye akaanza kula.”—Mwanzo 3:6.

Mungu alimwambia Adamu: “Siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.”​—MWANZO 2:17

Bila shaka, Mungu aliumia sana kuona watoto wake aliowapenda wakimkosea kimakusudi! Aliamua kufanya nini? Yehova alimwambia Adamu: “[Utarudi] ardhini, kwa kuwa ulitolewa humo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Mwanzo 3:17-19) Hivyo, “siku zote za maisha ya Adamu zilikuwa miaka 930, kisha akafa.” (Mwanzo 5:5) Adamu hakwenda mbinguni wala katika makao fulani ya roho. Kabla ya Yehova kumuumba kutoka kwenye mavumbi, Adamu hakuwepo. Kwa hiyo alipokufa, alipoteza uhai na mwili wake ukarudi kuwa mavumbi. Hakuendelea kuishi. Inasikitisha sana!

HATUJAKAMILIKA—KWA NINI?

Adamu na Hawa walipoteza ukamilifu na tarajio la kuishi milele kwa sababu walivunja sheria ya Mungu kimakusudi. Miili yao ilianza kubadilika; ukamilifu ukatoweka na wakawa wenye dhambi. Madhara ya uamuzi wao hayakuishia hapo. Waliwarithisha watoto wao hali hiyo. Waroma 5:12 inasema: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, basi kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”

Biblia inasema kwamba dhambi na kifo ni kama “kifuniko kinachowafunika watu wote na kifuniko kilichosokotwa juu ya mataifa yote.” (Isaya 25:7) Kifuniko hicho kinawafunika wanadamu kama ukungu wenye sumu usioepukika. Kwa hakika, “katika Adamu wote wanakufa.” (1 Wakorintho 15:22) Paulo aliuliza swali ambalo sisi pia tunajiuliza: “Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” Je, kuna yeyote?—Waroma 7:24.