Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari Nchini Mexico

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari Nchini Mexico

INACHANGAMSHA moyo kuona idadi inayoongezeka ya vijana Mashahidi wakirahisisha maisha yao ili washiriki zaidi katika huduma ya Kikristo. (Mt. 6:22) Wanafanya mabadiliko gani? Ni matatizo gani wanayokabili? Ili tujue, acheni tuwafahamu vizuri baadhi ya wale wanaotumikia nchini Mexico.

“ILIBIDI TUFANYE BADILIKO”

Dustin na Jassa kutoka Marekani walifunga ndoa mnamo Januari 2007. Muda mfupi baadaye, walitimiza tamaa yao ya muda mrefu ya kununua mashua na kuishi ndani yake. Mashua yao ilitia nanga karibu na Astoria, Oregon, Marekani, mji maridadi ulio karibu na Bahari ya Pasifiki unaozungukwa na vilima vyenye misitu na milima iliyofunikwa na theluji. Dustin anasema hivi: “Kila mahali ulipotazama, mandhari ilivutia sana!” Wenzi hao wa ndoa walihisi kwamba walikuwa wakiishi maisha rahisi huku wakimtegemea Yehova. Waliwaza hivi: ‘Tunaishi katika mashua yenye ukubwa wa mita 7.9, tunafanya kazi ya muda, tunahudhuria mikutano katika kutaniko la lugha ya kigeni, na mara kwa mara tunafanya upainia msaidizi.’ Hata hivyo, baada ya muda mfupi walifikia mkataa kwamba walikuwa wakijidanganya. Dustin anasema hivi: “Badala ya kuunga mkono kutaniko, tulitumia wakati mwingi kuirekebisha mashua yetu.  Tulijua kwamba ili tumtangulize Yehova maishani mwetu, ilibidi tufanye badiliko.”

Jassa anaongeza hivi: “Kabla ya kufunga ndoa, niliishi Mexico ambako nilishirikiana na kutaniko la lugha ya Kiingereza. Nilifurahia kutumikia huko, nami nilitamani sana kurudi.” Ili kuimarisha tamaa yao ya kutumikia nchi nyingine, Dustin na Jassa walianza kusoma katika ibada yao ya familia masimulizi ya maisha ya ndugu na dada waliohamia nchi zenye mashamba yaliyo tayari kuvunwa. (Yoh. 4:35) Dustin anasema: “Tulitaka kupata shangwe hiyo.” Rafiki zao walioishi Mexico walipowaeleza kuwa kikundi fulani kipya kinahitaji msaada, Dustin na Jassa wakaamua kujitolea. Wakaacha kazi zao, wakauza mashua yao, na kuhamia Mexico.

“NDIO UAMUZI BORA ZAIDI TULIOWAHI KUFANYA”

Dustin na Jassa waliishi katika mji wa Tecomán, umbali wa kilomita 4,345 kusini mwa Astoria, karibu na Bahari ya Pasifiki. Dustin anasema hivi: “Badala ya upepo mwanana na mandhari ya milima, tunakabiliana na joto kali sana na kila mahali kuna miti mingi ya malimau.” Mwanzoni hawakupata kazi za kuajiriwa. Kwa sababu hawakuwa na pesa za kutosha, walikula wali na maharagwe mara mbili kwa siku, kila juma. Jassa anasema hivi: “Tulipoanza kuchoshwa na chakula hicho, wanafunzi wetu wa Biblia walitupatia maembe, ndizi, mapapai, na mifuko iliyojaa malimau!” Baada ya muda, wenzi hao waliajiriwa kazi na shule moja ya Taiwan inayofundisha lugha kupitia intaneti. Sasa, pesa wanazopata kutokana na kazi hiyo zinatosheleza mahitaji yao ya kila siku.

Dustin na Jassa wanahisije kuhusu maisha yao mapya? Wanasema hivi: “Kuhamia kwetu hapa ndio uamuzi bora zaidi tuliowahi kufanya.” Wanaongeza hivi: “Uhusiano wetu pamoja na Yehova na kati yetu wenyewe umekuwa imara kuliko tulivyotarajia. Kila siku tunafanya mambo mengi pamoja kama vile kushiriki katika utumishi wa shambani, kuzungumza kuhusu jinsi ya kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia, na kutayarisha mikutano. Pia, hatuna mikazo tuliyokuwa nayo zamani.” Wanaongezea hivi: “Sasa tunathamini zaidi ukweli wa ahadi ambayo hatukuielewa kikamili mwanzoni, iliyo katika Zaburi 34:8, ‘Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.’”

NI NINI KINACHOWACHOCHEA—MAELFU YA WAFANYAKAZI WANAOJITOLEA?

Ndugu na dada zaidi ya 2,900, waseja na waliofunga ndoa, wengi wao wakiwa na umri wa miaka 20 na 30 hivi wamehamia maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme nchini Mexico. Kwa nini Mashahidi hao wote wamekubali kufanya kazi hiyo ngumu? Kikundi kimoja kilipoulizwa swali hilo, kilitoa sababu tatu kuu. Ni sababu zipi?

Leticia na Hermilo

 Ili kuonyesha kwamba wanampenda Yehova na wanadamu wenzao. Leticia alibatizwa akiwa na umri wa miaka 18. Anasema hivi: “Nilipojiweka wakfu kwa Yehova, nilijua kwamba hilo lilimaanisha kumtumikia kwa moyo na nafsi yote. Kwa hiyo, ili kumwonyesha Yehova kwamba ninampenda kwa moyo wangu wote, nilitaka kutumia nguvu na wakati zaidi katika utumishi wake.” (Marko 12:30) Hermilo, ambaye sasa amemwoa Leticia, alikuwa na miaka 20 hivi alipohama ili kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Anasema hivi: “Niligundua kwamba kuwasaidia watu kutosheleza mahitaji yao ya kiroho ndiyo njia bora zaidi ya kuwaonyesha jirani zangu upendo.” (Marko 12:31) Hivyo, alihama jiji lenye ufanisi la Monterrey alikofanya kazi katika benki na kufurahia maisha yenye starehe, na kuhamia katika mji mdogo.

Essly

Ili kupata shangwe ya kweli inayodumu. Muda mfupi baada ya kubatizwa, Leticia alienda na dada painia mwenye uzoefu katika mji wa mbali na kuhubiri huko kwa mwezi mmoja. Leticia anakumbuka hivi: “Nilishangaa sana. Kuona jinsi watu walivyoitikia vizuri ujumbe wa Ufalme kuliniletea shangwe nyingi sana. Mwishoni mwa mwezi huo, nilijiambia, ‘Hili ndilo ninalotaka kufanya maishani mwangu!’” Pia Essly, dada mseja mwenye umri wa miaka 20 hivi alivutiwa kuingia katika utumishi huo alipoona shangwe ya wengine. Alipokuwa katika shule ya sekondari, alikutana na Mashahidi wengi wenye bidii waliotumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa. Anasema hivi: “Kuziona nyuso zenye shangwe za ndugu na dada hao kulinichochea nitamani kuwa na maisha kama yao.” Dada wengi wamehisi kama Essly. Kwa kweli, nchini Mexico zaidi ya dada waseja 680 wanatumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi. Wamewawekea mfano mzuri kama nini vijana kwa wazee!

Ili kuishi maisha yenye kusudi na yanayoridhisha. Alipomaliza masomo ya sekondari, Essly alipata fursa ya kulipiwa masomo ya chuo kikuu. Rafiki zake walimtia moyo akubali fursa hiyo na kufuatilia “maisha ya kawaida,” yaani, kupata digrii, kazi, gari, na kusafiri anavyotaka. Lakini hakufuata mashauri yao. Essly anasema hivi: “Baadhi ya rafiki zangu Wakristo walifuatilia mambo hayo, na niligundua kwamba miradi ya kiroho haikuwa muhimu tena kwao. Niliona pia kwamba mwishowe walivunjika moyo kwa sababu ya matatizo waliyokabili walipojihusisha sana na mambo ya ulimwengu huu. Nilitaka kutumia ujana wangu kumtumikia Yehova kikamili kabisa.”

Racquel na Phillip

Essly alichukua masomo ya ziada yaliyomsaidia kupata kazi na kujitegemeza kifedha huku akifanya upainia, kisha akahamia eneo lenye uhitaji mkubwa  zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Pia alijitahidi kujifunza lugha ngumu za kienyeji za Waotomi na Watlapaneco. Sasa, anapofikiria miaka mitatu aliyohubiri katika maeneo ya mbali, Essly anasema hivi: “Kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi kumeniletea uradhi na kusudi la kweli maishani. Zaidi ya yote, kumeimarisha zaidi uhusiano wangu pamoja na Yehova.” Phillip na Racquel, wenzi wa ndoa wenye umri wa miaka 30 hivi kutoka Marekani wanakubaliana na maneno hayo. Wanasema hivi: “Ulimwengu unabadilika haraka sana hivi kwamba wengi huishi wakiwa na wasiwasi. Lakini kutumikia katika maeneo ambayo bado tunapata wengi wanaosikiliza ujumbe wa Biblia kunatufanya tuwe na kusudi halisi maishani. Ni jambo linaloridhisha sana!”

JINSI YA KUKABILIANA NA—HALI NGUMU

Verónica

Bila shaka, si jambo rahisi kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Tatizo moja ni kujitegemeza kifedha. Ili kujitegemeza, unahitaji kuwa tayari kuishi kulingana na hali za eneo unalotumikia. Verónica, painia mwenye uzoefu anasema hivi: “Katika eneo moja nilikotumika, nilifanya kazi ya kupika na kuuza vyakula vyepesi vya bei nafuu. Katika eneo lingine, niliuza nguo na kuwa kinyozi. Kwa sasa, ninasafisha nyumba ya mtu fulani na kuwafundisha wazazi kuwasiliana na watoto wao wachanga.”

Kuzoea utamaduni na desturi tofauti kunaweza kuwa jambo gumu hasa ikiwa unaishi kati ya wenyeji wanaoishi mashambani. Hali ilikuwa hivyo kwa Phillip na Racquel walipotumikia katika eneo lenye watu wanaozungumza Kinahuatl. Phillip anasema hivi: “Utamaduni wao ni tofauti sana na wetu.” Ni nini kilichowasaidia kukabiliana na hali hiyo? Phillip anaendelea kusema: “Tulikazia fikira mambo mazuri tuliyoona kwa Wanahuatl, kama vile uhusiano wao wa karibu katika familia, jinsi walivyoshughulika na wenzao kwa unyoofu, na pia ukarimu wao.” Racquel anaongeza hivi: “Tulijifunza mengi tulipoishi huko na tulipotumikia pamoja na ndugu na dada zetu wenyeji.”

JINSI YA KUJITAYARISHA

Ikiwa ungependa kutumikia katika maeneo ya mbali ambako msaada unahitajiwa, utajitayarishaje? Ndugu na dada ambao wamewahi kufanya utumishi huo wanasema hivi: Kabla ya kuhama, anza kurahisisha maisha yako na ujifunze kuridhika. (Flp. 4:11, 12) Ufanye nini kingine? Leticia anasema hivi: “Niliepuka kazi ambazo zingenilazimu kuishi katika eneo moja kwa muda mrefu. Nilifanya hivyo ili niweze kuhamia popote wakati wowote.” Hermilo anasema: “Nilijifunza kupika, kufua nguo na kupiga pasi.” Verónica anasema hivi: “Nilipokuwa nikiishi nyumbani na wazazi na ndugu zangu, nilisaidia kufanya usafi na kujifunza kupika vyakula vyenye lishe visivyogharimu sana. Nilijifunza pia kutunza pesa.”

Amelia na Levi

Levi na Amelia kutoka Marekani, ambao wamekuwa wenzi wa ndoa kwa miaka minane sasa, wanaeleza jinsi kutoa sala hususa kulivyowasaidia kujitayarisha kutumika nchini Mexico. Levi anasema hivi: “Tulihesabu kiasi cha pesa tulichohitaji ili kutumikia kwa mwaka mmoja katika nchi nyingine na kusali ili Yehova atusaidie kupata kiasi hicho.” Baada ya miezi kadhaa, waliweza kuweka kiasi cha pesa walichotaja katika sala yao, nao wakahama mara moja. Levi anasema: “Yehova alijibu ombi letu hususa, na sasa ilikuwa zamu yetu kutenda kulingana na ombi hilo.” Amelia anaongeza hivi: “Tulifikiri kwamba tungekaa kwa mwaka mmoja tu, lakini tumekuwa hapa kwa miaka saba sasa, nasi hatufikirii kuondoka! Kuishi hapa kunatupa fursa ya kujionea kihalisi utegemezo wa Yehova. Kila siku tunajionea uthibitisho wa wema wake.”

Adam na Jennifer

Adam na Jennifer, wenzi wa ndoa kutoka Marekani wanaotumikia katika eneo la lugha ya Kiingereza nchini Mexico, wanasema kwamba sala pia iliwasaidia sana. Wanapendekeza hivi: “Usisubiri mpaka hali ziwe nzuri kabisa. Taja katika sala tamaa yako ya kutumikia katika nchi ya kigeni, kisha utende kulingana na sala zako. Rahisisha maisha yako, iandikie ofisi ya tawi ya nchi unayotaka kutumikia, na baada ya kuhesabu gharama, hama!” * Ukifanya hivyo, utakuwa na maisha yenye kusisimua na yenye baraka nyingi za kiroho.

^ fu. 21 Kwa habari zaidi, tazama makala yenye kichwa, “Je, Unaweza ‘Kuvuka Uingie Makedonia’?” katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Agosti 2011.