Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri ya Furaha ya Familia

Kutatua Matatizo

Kutatua Matatizo

Mume anasema: “Baada ya kufunga ndoa, mimi na Sarah * tuliishi na familia yetu nyumbani kwa wazazi wangu. Siku moja, msichana aliyekuwa rafiki ya ndugu yangu aliniomba nimpeleke nyumbani kwao kwa gari letu. Nilikubali nami nikaenda pamoja na mwana wetu mdogo. Lakini niliporudi nyumbani, Sarah alikuwa amekasirika sana. Tulianza kugombana mbele ya familia yetu, alinishutumu kwamba ninavutiwa kimahaba na wanawake wengine. Nilikasirika na kuanza kusema mambo yaliyomkasirisha hata zaidi.”

Mke anasema: “Mwana wetu ana tatizo baya sana la afya, na wakati wa kisa hicho, tulikuwa na matatizo ya kifedha. Hivyo, Fernando alipoondoka nyumbani pamoja na msichana huyo na mwana wetu, nilikasirika kwa sababu kadhaa. Aliporudi nyumbani, nilitaka ajue nilivyohisi. Tuligombana sana na kutukanana. Baadaye nilihisi vibaya sana.”

WENZI wa ndoa wanapogombana, je, inamaanisha hawapendani tena? Hapana! Fernando na Sarah, walionukuliwa hapo juu, wanapendana sana. Lakini, hata katika ndoa bora, mara kwa mara matatizo yatatokea.

Kwa nini yanatokea, na unaweza kufanya nini ili kuyazuia yasiharibu ndoa yako? Kwa kuwa ndoa ni mpango ulioanzishwa na Mungu, ni jambo la hekima kuchunguza yale ambayo Neno lake, Biblia, linasema kuhusu jambo hilo.—Mwanzo 2:21, 22; 2 Timotheo 3:16, 17.

Kuyaelewa Matatizo

Wenzi wengi wa ndoa wanataka kutendeana kwa upendo na fadhili. Hata hivyo, Biblia inafunua uhakika wa mambo inaposema kwamba “wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Hivyo, matatizo yanapotokea huenda ikawa vigumu kujizuia. Na ugomvi unapoanza, ni vigumu sana kwa watu fulani kuepuka mazoea mabaya, kama vile kupiga makelele na kutukanana. (Waroma 7:21; Waefeso 4:31) Ni mambo gani mengine yanayoweza kufanya hali iwe mbaya?

Kwa kawaida, mume na mke wana njia tofauti za kuwasiliana. “Tulipooana,” anasema Michiko, “niligundua kwamba tuna njia tofauti kabisa za kuzungumzia mambo. Sipendi kuzungumza tu kuhusu yaliyotokea bali pia kwa nini yalitokea na yalitokea jinsi gani. Lakini inaonekana mume wangu anapenda kujua tu yaliyotokea.”

Kuna wengine walio na tatizo kama la Michiko. Katika ndoa nyingi, huenda mwenzi mmoja akataka kuzungumzia tatizo kwa urefu, lakini mwenzake hapendi kuzozana na hivyo anaepuka kulizungumzia. Nyakati nyingine, kadiri mwenzi mmoja anavyozidi kufuatilia jambo ndivyo yule mwingine anavyojitahidi kuliepuka. Je, umeona hali hiyo ikisitawi katika ndoa yako? Je, sikuzote inaonekana kwamba mmoja wenu ni mzungumzaji huku yule mwingine akiepuka mazungumzo?

Jambo lingine la kufikiria ni jinsi malezi ya mtu yanavyoweza kuwa na uvutano juu ya maoni yake kuhusu jinsi wenzi wa ndoa wanavyopaswa kuzungumza. Justin, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka mitano, anasema: “Familia yetu ni ya watu wanyamavu nami ninashindwa kuzungumzia waziwazi hisia zangu. Hilo linamfadhaisha mke wangu. Familia yao ni ya watu wanaopenda sana kuzungumza na hivyo si vigumu kwake kunieleza jinsi anavyohisi.”

Kwa Nini Tujitahidi Kutatua Matatizo?

Watafiti wamegundua kwamba ishara inayotegemeka ya kuonyesha jinsi ndoa itakavyokuwa yenye furaha si idadi ya mara ambazo wenzi wa ndoa wanasema kuwa wanapendana. Pia, uhusiano mzuri wa kingono na usalama wa kifedha si mambo ya maana zaidi. Badala yake, jambo linaloonyesha vizuri zaidi kwamba ndoa inafanikiwa ni uwezo wa mume na mke wa kutatua matatizo yoyote yanayotokea katika ndoa yao.

Zaidi ya hilo, Yesu alisema kwamba watu wawili wanapofunga ndoa, Mungu ndiye anayewaunganisha wala si mwanadamu. (Mathayo 19:4-6) Hivyo, ndoa nzuri inamletea Mungu heshima. Kwa upande mwingine, ikiwa mume hampendi na hamfikirii mke wake, huenda Yehova Mungu akapuuza sala zake. (1 Petro 3:7) Ikiwa mke hamheshimu mume wake, kwa kweli hamheshimu Yehova, aliyemweka mume awe kichwa cha familia.—1 Wakorintho 11:3.

Siri ya Mafanikio —Epuka Kuzungumza kwa Njia Yenye Kuumiza

Haidhuru unazungumza kwa njia gani au una malezi gani, kuna namna fulani za kuzungumza unazopaswa kuepuka ili ufaulu kutumia kanuni za Biblia na kutatua matatizo kwa mafanikio. Jiulize maswali yafuatayo:

‘Je, ninajizuia nisilipize kisasi?’

“Kufinya pua ndiko hutokeza damu, na kuchochea hasira ndiko hutokeza ugomvi,” inasema methali moja yenye hekima. (Methali 30:33) Hilo linamaanisha nini? Fikiria mfano huu. Maoni yanayotofautiana kuhusu kusawazisha bajeti ya familia (“tunapaswa kutumia pesa kwa hekima”) yanaweza kubadilika haraka na kuwa mashambuliano kati ya wenzi wa ndoa (“unaharibu pesa”). Ni kweli kwamba mwenzi wako ‘akifinya pua yako’ kwa kukushambulia kwa maneno, huenda ukataka ‘kufinya’ pua yake pia. Hata hivyo, kulipiza kisasi kunachochea tu hasira na kunaharibu mambo hata zaidi.

Mwandikaji wa Biblia, Yakobo alionya hivi: “Tazameni! Ni moto mdogo tu unaohitajika ili kuuwasha mwitu mkubwa! Basi, ulimi ni moto.” (Yakobo 3:5, 6) Wenzi wa ndoa wanapokosa kuzuia ulimi wao, moto mdogo au matatizo madogo yanaweza kugeuka haraka na kuwa moto mkubwa, yaani, ugomvi makali. Na upendo hauwezi kusitawi katika ndoa ambayo mara kwa mara inateketezwa na mioto mikubwa kama hiyo ya ugomvi mkali.

Badala ya kulipa kisasi, je, unaweza kumwiga Yesu, ambaye alipotukanwa “hakujibu kwa matukano”? (1 Petro 2:23) Njia ya haraka ya kumaliza ugomvi ni kukubali maoni ya mwenzi wako na kuomba msamaha kwa kuchangia tatizo.

JARIBU KUFANYA HIVI: Wakati ujao tatizo likitokea, jiulize: ‘Nitapata hasara gani nikikubali kwamba kuna jambo linalomhangaisha mwenzi wangu? Nimefanya nini ili kuchangia tatizo hili? Ni nini kinachonizuia nisiombe msamaha kwa makosa yangu?’

‘Je, ninapuuza au kupunguza uzito wa hisia za mwenzi wangu?’

“Ninyi nyote iweni na akili zinazopatana,” Neno la Mungu linaamuru. (1 Petro 3:8) Fikiria sababu mbili zinazoweza kukuzuia usifuate shauri hilo. Kwanza, huenda hufahamu maoni au hisia za mwenzi wako. Kwa mfano, akihangaishwa na tatizo fulani kuliko wewe, huenda ukamwambia, “Unahangaika kupita kiasi.” Pengine nia yako ni kumsaidia awe na maoni yanayofaa kuhusu tatizo hilo. Hata hivyo, maneno kama hayo hayawatulizi watu wengi. Waume na wake wanahitaji kujua kwamba wapendwa wao wanawaelewa na kuwahurumia.

Kuwa na kiburi kupita kiasi kunaweza pia kumfanya mtu apuuze hisia za mwenzi wake. Mtu mwenye kiburi anajaribu kujiinua kwa kuwadharau wengine daima. Anaweza kufanya hivyo kwa kuwapa wengine majina ya kuwavunjia heshima au kwa kuwalinganisha isivyofaa. Fikiria mfano wa Mafarisayo na waandishi wa siku za Yesu. Yeyote—hata Farisayo mwenzao—alipotoa maoni yaliyotofautiana na ya watu hao wenye kiburi, walimtukana na kusema mambo ya kumvunjia heshima. (Yohana 7:45-52) Yesu alikuwa tofauti. Aliwahurumia watu walipomweleza jinsi walivyohisi.—Mathayo 20:29-34; Marko 5:25-34.

Fikiria jinsi unavyotenda mwenzi wako anapokufunulia hisia zake. Je, maneno, sauti, na ishara zako za uso zinaonyesha kwamba unamhurumia? Au unapuuza haraka hisia zake?

JARIBU KUFANYA HIVI: Katika majuma yajayo, chunguza jinsi unavyozungumza na mwenzi wako. Ukimpuuza au ukisema jambo linalomvunjia heshima, mwombe msamaha haraka.

‘Je, nyakati zote ninafikiri kwamba nia ya mwenzi wangu ni ya ubinafsi?’

“Je, Ayubu amemwogopa Mungu bure? Je, wewe hukuweka ukuta kumzunguka yeye na kuzunguka nyumba yake na kuzunguka kila kitu alicho nacho pande zote?” (Ayubu 1:9, 10) Kwa kusema hivyo, Shetani alitilia shaka nia ya mwanamume huyo mwaminifu, Ayubu.

Wenzi wa ndoa wasipojihadhari, wanaweza kufanya vivyo hivyo. Kwa mfano, mwenzi wako akikutendea jambo zuri, je, unajiuliza anataka nini au anajaribu kufunika nini? Mwenzi wako akikosea, je, unaona hilo kuwa uthibitisho wa kwamba yeye ni mwenye ubinafsi na asiyejali? Je, unakumbuka upesi makosa kama hayo aliyofanya zamani na kuongeza kosa hilo jipya katika orodha yako?

JARIBU KUFANYA HIVI: Andika orodha ya mambo mazuri ambayo mwenzi wako amekutendea na sababu nzuri ambazo huenda zilimchochea akutendee hivyo.

Mtume Paulo aliandika hivi: “Upendo . . . hauweki hesabu ya ubaya.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Upendo wa kweli unajua kwamba tunakosea. Lakini hauweki hesabu ya ubaya. Paulo alisema pia kwamba upendo “huamini mambo yote.” (1 Wakorintho 13:7) Si kwamba upendo wa aina hiyo unaamini kitu chochote kile, bali uko tayari kutumaini. Si wenye kutilia mashaka. Upendo ambao Biblia inatuhimiza tuwe nao uko tayari kusamehe, nao unawachochea watu kuwa na maoni mazuri kuhusu nia ya wengine. (Zaburi 86:5; Waefeso 4:32) Wenzi wa ndoa wakiwa na upendo kama huo kati yao, watakuwa na ndoa yenye furaha.

JIULIZE . . .

  • Ni makosa gani waliyofanya wenzi wa ndoa waliotajwa mwanzoni mwa habari hii?

  • Ninaweza jinsi gani kuepuka kufanya makosa kama yao katika ndoa yangu?

  • Ni jambo gani kati ya yale yaliyotajwa katika habari hii ninayohitaji kufanyia kazi zaidi?

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.