Barua ya Kwanza ya Petro 3:1-22

  • Wake na waume (1-7)

  • Iweni na hisia-mwenzi; tafuteni amani (8-12)

  • Kuteseka kwa ajili ya uadilifu (13-22)

    • Muwe tayari kutetea tumaini lenu (15)

    • Ubatizo na dhamiri njema (21)

3  Vivyo hivyo, ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu,+ ili ikiwa kuna wale wasiotii lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao,+  kwa sababu wameshuhudia kwa macho yao mwenendo wenu ulio safi kiadili+ pamoja na heshima kubwa.  Kujipamba kwenu kusiwe kwa nje—kusuka nywele na kuvaa mapambo ya dhahabu+ au mavazi bora—  bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika mapambo yasiyoharibika ya roho ya utulivu na ya upole,+ ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.  Kwa maana hapo zamani ndivyo walivyokuwa wakijipamba wale wanawake watakatifu, waliomtumaini Mungu, wakijitiisha kwa waume zao,  kama Sara alivyomtii Abrahamu, akimwita bwana.+ Nanyi mmekuwa watoto wake, mradi tu mnaendelea kutenda mema, bila kuogopa.+  Enyi waume, vivyo hivyo endeleeni kukaa nao kulingana na ujuzi.* Wapeni heshima+ kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke, kwa kuwa wao pia ni warithi pamoja nanyi+ wa pendeleo lisilostahiliwa la uzima, ili sala zenu zisizuiwe.  Mwishowe, ninyi nyote fikirini kwa upatano,*+ muwe na hisia-mwenzi, upendo wa kindugu, huruma nyororo,+ na unyenyekevu.+  Msilipe ubaya kwa ubaya+ au matukano kwa matukano.+ Badala yake, lipeni kwa baraka,+ kwa sababu mliitwa kwenye mwendo huu, ili mrithi baraka. 10  Kwa maana “yeyote anayependa uzima na kuona siku zilizo njema, lazima aulinde ulimi wake usiseme mabaya+ na midomo yake isiseme udanganyifu. 11  Na aache mabaya,+ atende mema;+ na atafute amani na kuifuatilia.+ 12  Kwa maana macho ya Yehova* yanawatazama waadilifu, na masikio yake yanasikiliza dua yao,+ lakini uso wa Yehova* uko dhidi ya wale wanaotenda maovu.”+ 13  Kwa kweli, ni nani atakayewadhuru mkifanya yaliyo mema kwa bidii?+ 14  Lakini hata mkiteseka kwa ajili ya uadilifu, ninyi ni wenye furaha.+ Hata hivyo, msiogope kile wanachokiogopa,* wala msiwe na wasiwasi.+ 15  Bali mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu anayewauliza sababu ya tumaini mlilo nalo, lakini mkifanya hivyo kwa upole+ na heshima kubwa.+ 16  Iweni na dhamiri njema,+ ili katika kila jambo ambalo wanasema vibaya dhidi yenu, wale wanaosema vibaya dhidi yenu waaibishwe+ kwa sababu ya mwenendo wenu mzuri mkiwa wafuasi wa Kristo.+ 17  Kwa maana ni afadhali kuteseka kwa sababu mnatenda mema,+ ikiwa ni mapenzi ya Mungu kuruhusu jambo hilo, kuliko kuteseka kwa sababu mnatenda maovu.+ 18  Kwa maana Kristo alikufa mara moja kwa wakati wote kwa ajili ya dhambi,+ mtu mwadilifu kwa ajili ya wasio waadilifu,+ ili awaongoze ninyi kwa Mungu.+ Aliuawa katika mwili,+ lakini akafanywa kuwa hai katika roho.+ 19  Na katika hali hiyo alienda na kuwahubiria roho walio gerezani,+ 20  ambao mwanzoni hawakuwa watiifu Mungu alipokuwa akingoja kwa subira* katika siku za Noa,+ safina ilipokuwa ikijengwa,+ ambayo ndani yake watu wachache, yaani, nafsi nane,* walichukuliwa salama kupitia maji.+ 21  Ubatizo, ambao unalingana na hili, unawaokoa ninyi sasa pia (si kwa kuondoa uchafu wa mwili, bali kwa ombi linalotolewa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema),+ kupitia ufufuo wa Yesu Kristo. 22  Yeye yuko kwenye mkono wa kuume wa Mungu,+ kwa maana alienda mbinguni, nao malaika na mamlaka na nguvu vilitiishwa kwake.+

Maelezo ya Chini

Au “mkiwafikiria na kuwajali; kuwaelewa.”
Au “kwa umoja wa akili.”
Au labda, “msiogope vitisho vyao.”
Tnn., “subira ya Mungu ilikuwa ikingoja.”
Au “watu wanane.”