Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MKARIBIE MUNGU

“Umeyafunua . . . kwa Watoto”

“Umeyafunua . . . kwa Watoto”

Je, ungependa kujua ukweli kumhusu Mungu, yaani, yeye ni nani, viwango vyake ni nini, na mapenzi yake nini? Katika Neno lake, Biblia, Yehova Mungu anafunua ukweli wote kujihusu. Lakini si kila mtu anayesoma Biblia anaweza kuelewa kikamili kweli hizo. Kwa nini? Kwa sababu ni pendeleo kuelewa kweli hizo za kiroho; si kila mtu anayezipokea. Acheni tuchunguze mambo ambayo Yesu alisema kuhusu jambo hilo.—Soma Mathayo 11:25.

Andiko hilo linaanza kwa maneno haya: “Wakati huo Yesu akajibu, akasema.” Hivyo, huenda Yesu anataka kusema kuhusu jambo ambalo tu limetukia. Alikuwa ametoka kuwakemea watu ambao walikataa kuwa wafuasi wake katika majiji matatu ya Galilaya ambako alikuwa amefanya miujiza yenye nguvu. (Mathayo 11:20-24) Huenda ukajiuliza, ‘Mtu angewezaje kuona miujiza ya Yesu na asiamini kweli alizofundisha?’ Walikataa kuamini kwa sababu ya mtazamo wa ukaidi wa mioyo yao.—Mathayo 13:10-15.

Yesu alijua kwamba ili tuelewe kweli za kiroho zinazopatikana katika Biblia, tunahitaji mambo mawili: Msaada wa Mungu na mtazamo unaofaa wa moyo. Yesu anaeleza: “Ninakusifu wewe hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye akili na umeyafunua kwa watoto.” Je, unaona ni kwa nini kuelewa kweli hizo za Biblia ni pendeleo? Yehova ana haki ya kuamua watu atakaowafunilia kweli kwa sababu ndiye “Bwana wa mbingu na dunia.” Mungu hana ubaguzi na hivyo amewapa watu wote fursa ya kuelewa kweli hizo. Hivyo, ni kwa msingi gani amefunua kweli za Biblia kwa watu fulani na si kwa wengine?

Yehova huwapa kibali wanyenyekevu, bali si wenye kiburi. (Yakobo 4:6) Amewaficha kweli wenye “hekima na wenye akili,” yaani, watu walio na hekima ya kilimwengu na wasomi wenye kiburi, wenye kujitegemea wanaohisi hawahitaji msaada wake. (1 Wakorintho 1:19-21) Hata hivyo, amefunua kweli hizo kwa “watoto”—wale wanamtafuta wakiwa na moyo mnyoofu, wanyenyekevu kama watoto. (Mathayo 18:1-4; 1 Wakorintho 1:26-28) Mwana wa Mungu, Yesu, alijionea watu kama hao. Viongozi wengi wa kidini wenye kiburi waliokuwa na elimu ya juu, hawakuelewa maana ya ujumbe wa Yesu, lakini wavuvi wanyenyekevu walielewa. (Mathayo 4:18-22; 23:1-5; Matendo 4:13) Wakati huohuo, baadhi ya matajiri na wasomi walioonyesha unyenyekevu wa kweli walikuja kuwa wafuasi wa Yesu.—Luka 19:1, 2, 8; Matendo 22:1-3.

Tuchunguze swali lililoulizwa mwanzoni: Je, ungependa kujua ukweli kumhusu Mungu? Ikiwa ndivyo, unaweza kupata faraja kwa kujua kwamba Mungu hawapi kibali wale wanaojiona kuwa wenye hekima ya kilimwengu. Badala yake, anawapa kibali wale wanaodharauliwa na watu wenye hekima ya kilimwengu. Ikiwa unajifunza Neno la Mungu ukiwa na mtazamo unaofaa wa akili na moyo, unaweza kuwa miongoni mwa wale ambao Yehova huwapa zawadi yenye thamani, yaani, kuelewa kweli kumhusu yeye. Kujua kweli hizo kutafanya maisha yako yawe na kusudi sasa na kutakusaidia kupata “uzima ulio wa kweli,” yaani, uhai usio na kikomo katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ulio karibu kuja ambao Mungu ameahidi. *1 Timotheo 6:12, 19; 2 Petro 3:13. ▪

Usomaji wa Biblia Unaopendekezwa kwa Mwezi wa Januari

Mathayo 1-21

^ fu. 7 Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujifunza ukweli kumhusu Mungu na makusudi yake. Wanawafundisha watu Biblia nyumbani bila malipo, kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?