Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Misiba ya Asili—Je, Inathibitisha Kwamba Mungu Ni Mkatili?

Misiba ya Asili—Je, Inathibitisha Kwamba Mungu Ni Mkatili?

WENGINE HUSEMA: “Mungu anatawala ulimwengu, kwa hiyo anasababisha misiba ya asili, basi lazima awe mkatili.”

BIBLIA INASEMA NINI? “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) “Yule mwovu” ni nani? Biblia inaonyesha kwamba ni Shetani. (Mathayo 13:19; Marko 4:15) Je, huo ni ukweli? Fikiria jambo hili: Ikiwa Shetani anatawala ulimwengu, basi anawashawishi wanadamu wawe na ubinafsi, pupa, na kukosa busara kama yeye. Je, hilo halitusaidii kutambua ni kwa nini wanadamu wanaharibu mazingira duniani? Wataalamu wengi wanaonya kwamba kuharibiwa kwa mazingira huchangia kuleta misiba ya asili, labda kwa kuisababisha, au kufanya iwe mabaya zaidi, au kufanya wanadamu wapatwe kwa urahisi zaidi na misiba hiyo.

Basi, kwa nini Mungu anamruhusu Shetani awe na mamlaka hivyo? Hali hiyo ilianza mwanzoni mwa historia ya wanadamu, wazazi wetu wa kwanza walipokataa Mungu awe Mtawala wao. Tangu wakati huo, wanadamu wengi wameasi pia. Uamuzi huo wa kukataa utawala wa Mungu umefanya ulimwengu wa wanadamu uongozwe na Shetani, adui ya Mungu. Hivyo, Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30) Je, Shetani atatawala milele? Hapana!

Yehova * anaona mateso ambayo Shetani anasababisha. Kwa kweli, Mungu anahuzunishwa sana na mateso yanayowapata wanadamu. Kwa mfano, kuhusu matatizo ambayo yaliwapata Waisraeli, Biblia inasema hivi kumhusu Mungu: “Wakati wa taabu zao zote hilo lilimtaabisha.” (Isaya 63:9) Kwa sababu ana huruma, hivi karibuni, Mungu amepanga kuondoa utawala wa Shetani! Amemchagua Mwanawe, Yesu Kristo, awe Mtawala mwenye haki na uadilifu milele.

JINSI UNAVYOHUSIKA: Ingawa utawala wa Shetani umeshindwa kuzuia watu wasipatwe na misiba ya asili, utawala wa Yesu hautashindwa. Pindi moja, Yesu aliwalinda wanafunzi wake wakati wa dhoruba kali. Simulizi hilo la Biblia linasema: “Akaukemea upepo na kuiambia bahari: ‘Nyamaza, utulie!’ Na upepo ukapunguka, kukawa utulivu mkubwa.” Wanafunzi wakasema: “Kwa kweli huyu ni nani, kwa sababu hata upepo na bahari zinamtii?” (Marko 4:37-41) Tukio hilo linatuhakikishia kwamba Yesu atawalinda wanadamu watiifu atakapotawala akiwa Mfalme.—Danieli 7:13, 14.

^ fu. 5 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.