Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dini Inategemeka Kuhusiana na Vita?

Je, Dini Inategemeka Kuhusiana na Vita?

Alberto alikuwa mwanajeshi kwa karibu miaka kumi. Anakumbuka hivi: “Mchungaji wetu alituombea akisema ‘Mungu yuko pamoja nanyi.’ Hata hivyo, nilijiambia, ‘Ninaenda kuua, lakini Biblia husema, “usiue.”’”

Ray alikuwa mwanajeshi wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Wakati mmoja alimuuliza mchungaji: “Unakuja kwenye meli yetu na kutuombea ushindi. Je, adui zetu hawafanyi hivyo pia?” Mchungaji alimwambia Bwana hutenda kwa njia ya ajabu.

Kama watu wengi, huenda wewe pia hukubaliani na jibu la mchungaji huyo.

BIBLIA INAFUNDISHA NINI?

Yesu alisema mojawapo ya amri kuu za Mungu ni: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Marko 12:31) Je, Yesu alisema kumpenda jirani kungetegemea taifa au mahali mtu huyo anapoishi? Hapana. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) Upendo kati yao ungekuwa wa pekee sana hivi kwamba ungekuwa alama ya kuwatambulisha. Wangekuwa tayari kutoa uhai wao kwa ajili ya wenzao badala ya kuwaua.

Wakristo wa mapema waliishi kupatana na maneno ya Yesu. Kitabu The Encyclopedia of Religion kinasema hivi: “Mababa wa mapema wa kanisa, kutia ndani Tertullian na Origen, walithibitisha kwamba Wakristo walizuiwa kutoa uhai wa binadamu, kanuni iliyowazuia wasishiriki katika jeshi la Roma.”

MASHAHIDI WA YEHOVA WANAFANYAJE?

Kwa sababu Mashahidi wa Yehova wanaishi karibu katika kila nchi, wao hujikuta katika pande zinazopigana wakati wa vita. Hata hivyo, wao hujitahidi kudumisha alama inayowatambulisha, yaani, upendo.

Je, viongozi wa kidini wamewafundisha watu

Kwa mfano, wakati wa vita vya kikabila kati ya Wahutu na Watutsi nchini Rwanda mwaka wa 1994, Mashahidi wa Yehova hawakushiriki kabisa vita hivyo. Mashahidi wa kabila moja walificha wale wa kabila lingine, hata ingawa kufanya hivyo kulihatarisha uhai wao. Mashahidi wawili Wahutu waliokuwa wamewaficha ndugu zao Watutsi walipokamatwa, wapiganaji wa kikundi cha Interahamwe cha Wahutu waliwaambia hivi, “Mnapaswa kufa kwa sababu mmewasaidia Watutsi kutoroka.” Kwa kusikitisha, Mashahidi hao wawili waliuawa.Yohana 15:13.

Una maoni gani: Je, Mashahidi wa Yehova wanatenda kupatana na amri ya Yesu kuhusu upendo wa kujidhabihu?