Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Majibu ya Maswali ya Biblia

Majibu ya Maswali ya Biblia

Je, Mungu husikiliza sala zote?

Mungu husikiliza watu wa mataifa yote. (Zaburi 145:18, 19) Neno lake, Biblia, hutuhimiza tumweleze jambo lolote linalotuhangaisha. (Wafilipi 4:6, 7) Hata hivyo, si sala zote zinazompendeza Mungu. Kwa mfano, hapendezwi na sala zenye maneno yanayorudiwa-rudiwa.Soma Mathayo 6:7.

Pia, Yehova hapendezwi na sala za watu wanaovunja sheria zake kimakusudi. (Methali 28:9) Kwa mfano, katika nyakati za Biblia, Mungu alikataa kuwasikiliza Waisraeli waliokuwa na hatia ya kuua. Kwa kweli, ni lazima tutimize mambo fulani ili Mungu atusikilize.Soma Isaya 1:15.

Tunapaswa kufanya nini ili Mungu atusikilize?

Ili Mungu atusikilize tunapaswa kusali tukiwa na imani. (Yakobo 1:5, 6) Ni lazima tuwe na hakika kwamba yupo na anatujali. Tunaweza kuimarisha imani yetu kwa kujifunza Biblia kwa sababu imani ya kweli hutegemea uthibitisho na uhakika unaopatikana katika Neno la Mungu.Soma Waebrania 11:1, 6.

Tunapaswa kusali kwa unyoofu na kwa unyenyekevu. Hata Yesu, Mwana wa Mungu, alisali kwa unyenyekevu. (Luka 22:41, 42) Hivyo, badala ya kumwambia Mungu jambo la kufanya, tunapaswa kujitahidi kuelewa sheria zake kwa kusoma Biblia. Na hivyo tunaweza kusali kupatana na mapenzi ya Mungu.Soma 1 Yohana 5:14.