Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Lugha Zote Zilianzia Kwenye “Mnara wa Babeli”?

Je, Lugha Zote Zilianzia Kwenye “Mnara wa Babeli”?

“Yehova akawatawanya juu ya uso wote wa dunia kutoka huko, nao pole kwa pole wakaacha kulijenga lile jiji. Hiyo ndiyo sababu liliitwa jina lake Babeli, kwa sababu huko ndiko Yehova alikuwa amevuruga lugha ya dunia yote.”Mwanzo 11:8, 9.

JE, KWELI jambo hilo lililoandikwa katika Biblia lilitukia? Je, watu walianza kuzungumza lugha tofauti kwa wakati mmoja kama inavyoelezwa? Watu fulani hudhihaki simulizi la Biblia kuhusu chanzo cha lugha za wanadamu na jinsi zilivyosambaa. Mwandikaji mmoja anadai hivi: “Hekaya ya Mnara wa Babeli ni moja kati ya hadithi za kipumbavu zaidi.” Hata rabi mmoja Myahudi alisema hiyo ni “njia isiyopatana na akili ya kufafanua chanzo cha mataifa.”

Kwa nini watu hawakubaliani na simulizi la Babeli? Kwa ufupi, linapingana na nadharia fulani zinazohusu chanzo cha lugha. Kwa mfano, wasomi fulani hudokeza kwamba vikundi vya lugha havikuanza tu kwa ghafula bali vilitokea hatua kwa hatua kutoka kwa “lugha moja ya asili.” Wengine huamini kwamba lugha kadhaa za msingi zilianza zenyewe zikiwa sauti zisizoeleweka, na hatua kwa hatua zikawa miundo bora ya maneno. Nadharia hizo na nyinginezo zimefanya wengi wakubaliane na Profesa W. T. Fitch, aliyeandika hivi katika kitabu chake The Evolution of Language: “Bado hatujapata majibu yenye kusadikisha.”

Wataalamu wa vitu vya kale na watafiti wamegundua nini kuhusiana na chanzo na ukuzi wa lugha za wanadamu? Je, uvumbuzi wao unathibitisha nadharia zilizotajwa? Au je, uvumbuzi wao unaunga mkono simulizi la Babeli? Kwanza acheni tuchunguze kwa undani simulizi hilo la Biblia.

LILITUKIA WAPI NA WAKATI GANI?

Biblia inasema kwamba kuvurugwa kwa lugha na kutawanyika kwa watu kulitokea “katika nchi ya Shinari,” ambayo baadaye iliitwa Babilonia. (Mwanzo 11:2) Hilo lilitukia lini?  Biblia inasema: “Dunia [yaani, wanadamu] ilikuwa imegawanyika,” katika siku za Pelegi, ambaye alizaliwa miaka 250 hivi kabla ya Abrahamu. Basi, inaonekana matukio ya Babeli yalitukia miaka 4,200 hivi iliyopita.Mwanzo 10:25; 11:18-26.

Wasomi fulani hudai kwamba lugha za kisasa zimetokana na lugha moja ya msingi, lugha ya asili ambayo wanadhani ilizungumzwa karibu miaka 100,000 iliyopita. * Wengine hudai lugha za kisasa zinahusiana na lugha fulani za msingi ambazo zilizungumzwa karibu miaka 6,000 iliyopita. Lakini wataalamu wa lugha hutambuaje lugha ambazo hazizungumzwi sasa? “Hilo ni jambo gumu,” linasema gazeti Economist. “Tofauti na wanabiolojia, wataalamu wa lugha hawana mabaki ya lugha za kale yanayoweza kuwasaidia kuchunguza wakati uliopita.” Gazeti hilo linaongezea kwamba wataalamu wa lugha wanaoamini mageuzi hufikia mkataa kwa kutumia “hesabu za kukisiwa.”

Hata hivyo, kuna “mabaki ya lugha za kale.” Mabaki hayo ni nini, na yanafunua nini kuhusu chanzo cha lugha za wanadamu? Kitabu The New Encyclopædia Britannica hueleza hivi: “Maandishi ya kale zaidi ya lugha, yaani mabaki ya lugha ambayo wanadamu wamepata, yaliandikwa miaka 4,000 au 5,000 hivi iliyopita.” Wataalamu wa vitu vya kale walipata wapi “mabaki ya lugha,” au “maandishi ya kale ya lugha”? Kwenye eneo la chini la Mesopotamia, mahali ambapo Shinari ilikuwa. * Basi uthibitisho huo unaunga mkono mambo yanayotajwa katika Biblia.

LUGHA TOFAUTI, NJIA TOFAUTI ZA KUFIKIRI

Simulizi la Biblia linasema kwamba Mungu alichukua hatua ya “kuvuruga lugha yao ili wasiweze kusikilizana lugha.” (Mwanzo 11:7) Ikawaje? Wajenzi “wakaacha kulijenga lile jiji” la Babeli na wakatawanyika “juu ya uso wote wa dunia.” (Mwanzo 11:8, 9) Hivyo, Biblia haisemi kwamba lugha zote za kisasa zilitokana na “lugha moja ya asili.” Badala yake, inaeleza kuhusu kutokea ghafula kwa lugha mpya zilizo kamili, kila moja ikiwa na uwezo wa kueleza hisia na mawazo mbalimbali ya wanadamu na kila lugha ikiwa tofauti kabisa na nyinginezo.

Bamba la barua ya maandishi ya kikabari, kutoka Mesopotamia, karne ya tatu K.W.K.

Namna gani lugha zinazozungumzwa leo? Je, zinatofautiana kimsingi? Mwanasayansi Lera Boroditsky, aliandika: “Wataalamu wa lugha walipochunguza lugha zilizo duniani (walichunguza chache kati ya lugha 7,000 hivi), waligundua tofauti nyingi sana.” Naam, ingawa huenda kuna ulinganifu katika matamshi ya kundi moja la lugha, kama vile lugha za Kikantoni na Kihakka zinazozungumzwa China kusini, kimsingi kundi hilo linatofautiana na makundi mengine, kama vile Kikatalani au Kivalencia nchini Hispania.

Lugha huongoza mawazo ya watu na jinsi wanavyofafanua vitu mbalimbali kama vile rangi, idadi, mahali, na pande tofauti. Kwa mfano, katika lugha fulani unaweza kusema, “Kuna mdudu  kwenye mkono wako wa kulia.” Lakini katika lugha nyingine, “Kuna mdudu kwenye mkono wako wa kusini-magharibi.” Tofauti kama hizo zinaweza kutatanisha sana. Haishangazi kwamba wajenzi huko Babeli walishindwa kuendelea na kazi yao.

JE, NI SAUTI ZISIZOELEWEKA AU NI MIUNDO YA MANENO?

Wanadamu walizungumza lugha gani mwanzoni? Biblia husema kwamba mwanamume wa kwanza, Adamu, alibuni maneno mapya alipowapa majina wanyama na ndege. (Mwanzo 2:20) Pia, Adamu alitunga shairi lililoeleza jinsi alivyohisi kumwelekea mkewe, naye mkewe alieleza waziwazi amri ya Mungu na matokeo ya kutotii. (Mwanzo 2:23; 3:1-3) Basi, lugha ya kwanza kabisa iliwawezesha wanadamu kuwasiliana kikamili na kujieleza kwa ustadi.

Kuvurugwa kwa lugha huko Babeli kuliathiri uwezo wa wanadamu wa kufanya kazi. Hata hivyo, kama lugha ya kwanza, lugha zao mpya zilikuwa na miundo ya maneno. Baada ya karne chache, wanadamu walijenga majiji makubwa, walipanga majeshi yenye nguvu, na kufanya biashara za kimataifa. (Mwanzo 13:12; 14:1-11; 37:25) Je, wangefanya maendeleo hayo bila kutumia lugha yenye mpangilio na muundo wa maneno? Kulingana na Biblia, lugha ya kwanza ya wanadamu na lugha zilizoanzishwa Babeli, hazikuwa sauti zisizoeleweka, bali lugha zenye miundo ya maneno.

Watafiti wa kisasa wanaunga mkono jambo hilo. Kitabu The Cambridge Encyclopedia of Language kinasema: “Kila utamaduni ambao umechunguzwa, hata wa watu wasio na maendeleo ya kisasa, una lugha kamili, yenye muundo wa maneno kama tu lugha za mataifa yaliyoendelea.” Vivyo hivyo, katika kitabu chake The Language Instinct, Profesa Steven Pinker wa Chuo cha Harvard anasema: “Hakuna lugha iliyopitwa na wakati.”

WAKATI UJAO WA LUGHA

Baada ya kuchunguza kwa undani “mabaki” ya lugha, tofauti za kimsingi kati ya makundi ya lugha, na miundo maalumu ya lugha za zamani, tunaweza kufikia mkataa gani? Wengi wameamua kwamba simulizi la Biblia kuhusu matukio ya Babeli ni ufafanuzi wa kweli.

Biblia hutuambia Yehova Mungu alivuruga lugha huko Babeli kwa sababu watu walimwasi. (Mwanzo 11:4-7) Hata hivyo, aliahidi kwamba “[ange]badilisha lugha ya vikundi vya watu na kuwapa lugha safi, ili wote waliitie jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega.” (Sefania 3:9) ‘Lugha hii safi,’ yaani, ukweli ulio katika Neno la Mungu, inawaunganisha watu ulimwenguni pote leo. Basi tunaweza kutarajia kwamba wakati ujao Mungu atawaunganisha wanadamu hata zaidi kwa kuwapa lugha moja, na kuondoa mvurugo uliotokea Babeli.

^ fu. 8 Nadharia kuhusu lugha hasa hutegemea wazo la kwamba wanadamu walitokana na nyani. Ili kupata habari zaidi kuhusu madai hayo, ona ukurasa wa 27-29 wa broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 9 Wataalamu wa vitu vya kale wamefukua piramidi kadhaa, minara ya hekalu yenye ngazi karibu na Shinari. Biblia inasema kwamba wajenzi wa mnara wa Babeli hawakutumia mawe bali walitumia matofali na lami kama saruji. (Mwanzo 11:3, 4) Huko Mesopotamia, “ilikuwa vigumu kupata mawe,” kinasema kitabu The New Encyclopædia Britannica, ingawa lami ilipatikana kwa wingi.