Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Kuna Mateso Mengi?

Kwa Nini Kuna Mateso Mengi?

Ili kuelewa kwa nini kuna mateso mengi na kwa nini wanadamu wameshindwa kuondoa mateso hayo, tunahitaji kujua chanzo cha mateso. Tunashukuru kwamba Biblia inatusaidia kujua chanzo cha matatizo. Katika makala hii, tutachunguza sababu tano za msingi zinazofanya watu wateseke sana. Tunakualika uchunguze kwa makini kile ambacho Biblia inasema kuhusu chanzo cha mateso.2 Timotheo 3:16.

MATOKEO YA UTAWALA MBAYA

Biblia inasema hivi: “Mtu yeyote mwovu anapotawala, watu huugua.”Methali 29:2.

Historia imejaa rekodi ya watawala wa kimabavu ambao waliwasababishia raia mateso chungu nzima. Ni kweli kwamba si viongozi wote hutawala kimabavu. Huenda wengine wakawa na nia ya kuwasaidia watu. Hata hivyo, wanapopata mamlaka, mara nyingi jitihada zao hushindwa kwa sababu ya mizozano ya kisiasa. Au huenda wakatumia mamlaka yao vibaya ili wajifaidishe, na kuwasahau wananchi. “Historia inaonyesha jitihada na malengo ambayo hayakutimizwa,”  akasema aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Henry Kissinger.

Biblia pia inasema hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Wanadamu hawana hekima na uwezo wa kuongoza mambo yao yote kwa mafanikio. Ikiwa wanadamu hawawezi kuongoza hatua zao, wanawezaje kuongoza hatua za taifa? Umeona kwa nini watawala wa kibinadamu hawawezi kuondoa mateso? Mara nyingi, mateso yamesababishwa na utawala mbaya!

MATOKEO YA DINI YA UWONGO

Yesu alisema hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”Yohana 13:35.

Viongozi wa kila dini au dhehebu huhubiri kuhusu upendo na umoja. Hata hivyo, hawawafundishi wafuasi wao kupendana na hivyo wameshindwa kuondoa ubaguzi. Badala ya kuwasaidia watu kupendana, mara nyingi dini imekuwa chanzo cha migawanyiko, ubaguzi, na mapigano miongoni mwa watu na kati ya mataifa. Mwishoni mwa kitabu chake kiitwacho Christianity and the World Religions, mwanatheolojia Hans Küng aliandika: “Mapambano mabaya zaidi katika historia ni yale ambayo yamehusisha dini.”

 Kwa kuongezea, viongozi wengi wa kidini wamekubali maadili mapotovu kingono na ngono za jinsia moja. Hilo limesababisha kuenea kwa magonjwa, utoaji wa mimba, mimba zisizotakiwa, kuvunjika kwa ndoa na familia, na hivyo kusababisha maumivu na mateso mengi.

UBINAFSI NA KUTOKAMILIKA KWA WANADAMU

“Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.”Yakobo 1:14, 15.

Sisi sote hufanya makosa kwa sababu tumerithi dhambi na tunahitaji kupambana na tamaa ya ‘kufanya mambo yanayopendwa na mwili.’ (Waefeso 2:3) Huenda ikawa rahisi kufanya dhambi tunaposhawishiwa kutosheleza tamaa zetu. Tukikubali kushawishiwa, matokeo ya matendo yetu yanaweza kuwa mabaya.

Mwandishi P. D. Mehta aliandika: “Chanzo kikubwa cha matatizo yetu ni tamaa isiyoweza kudhibitiwa, pupa, na kujitakia makuu.” Mazoea mabaya kama vile ulevi, kutumia dawa za kulevya, kucheza kamari, na uasherati, yameharibu maisha ya watu wengi katika jamii na kusababisha mateso kwa familia, marafiki, na watu wengine. Kwa sababu ya kutokamilika kwa wanadamu, tunaelewa Biblia inaposema: “Kwa maana tunajua kwamba uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja mpaka sasa.”Waroma 8:22.

UVUTANO WA MASHETANI

Biblia inasema Shetani ni “mungu wa mfumo huu wa mambo” na anashirikiana na roho waovu wenye nguvu wanaoitwa mashetani.2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 12:9.

Kama Shetani, roho hao waovu pia hujitahidi sana kuwapotosha wanadamu. Mtume Paulo alitaja jambo hilo aliposema: “Tuna kushindana mweleka, si juu ya damu na mwili, bali juu ya serikali, juu ya mamlaka, juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.”Waefeso 6:12.

Ingawa roho waovu hufurahia kuwasumbua watu, hilo si lengo lao kuu. Lengo lao ni kuwapotosha watu wasimwabudu Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova. (Zaburi 83:18) Matendo kama vile unajimu, uchawi, na uaguzi ni kati ya mbinu ambazo roho waovu hutumia ili kuwadhibiti na kuwapotosha watu. Ndiyo maana Yehova hutuonya kuhusu hatari hizo na huwalinda wote wanaompinga Shetani na roho waovu.Yakobo 4:7.

TUNAISHI KATIKA “SIKU ZA MWISHO”

Miaka elfu mbili hivi iliyopita, Biblia ilitabiri: “Ujue jambo hili, ya kwamba katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”

Ili kufafanua ugumu wa nyakati hizo, Biblia inaendelea kusema: “Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, . . . wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” Bila shaka, kuna mateso mengi leo kwa sababu tunaishi katika “siku za mwisho.”2 Timotheo 3:1-4.

Kutokana na sababu tulizochunguza, umeona kwa nini wanadamu hawawezi kuondoa kabisa mateso, hata kama wana nia nzuri? Hivyo basi, tunaweza kupata wapi msaada? Tunapaswa kumtegemea Muumba wetu, ambaye ameahidi ‘kuzivunja kazi za Ibilisi’ na wafuasi wake. (1 Yohana 3:8) Makala ifuatayo itaeleza kile ambacho Mungu atafanya ili kuondoa mateso.