Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Watatu Waliotafuta Ukweli Karne ya 16—Je, Waliupata?

Watu Watatu Waliotafuta Ukweli Karne ya 16—Je, Waliupata?

“KWELI ni nini?” Yesu alipokuwa akishtakiwa aliulizwa swali hilo na Pontio Pilato, aliyekuwa gavana Mroma wa Yudea katika karne ya kwanza. (Yohana 18:38) Bila shaka, Pilato hakuwa akitafuta ukweli. Swali lake lilifunua jinsi alivyokuwa na shaka na alivyokosa imani. Inaonekana Pilato alifikiri kwamba ukweli ni jambo lolote ambalo mtu anaamua kuamini au alilofundishwa kuamini, yaani, haiwezekani kutambua ukweli. Watu wengi leo wanaamini hivyo.

Katika karne ya 16 watu walioenda kanisani huko Ulaya walishindwa kutambua ukweli. Ingawa walifunzwa kutoka utotoni kuamini ukuu wa papa na mafundisho ya kanisa Katoliki, walikabili mafundisho mapya yaliyosambazwa na Marekebisho ya Kidini, yaliyokuwa yakienezwa barani Ulaya wakati huo. Wangeamini nini? Wangetambuaje ukweli?

Enzi hizo, miongoni mwa wengine kulikuwa na wanaume watatu ambao walijitahidi kutafuta ukweli. * Walitofautishaje kati ya mafundisho ya kweli na ya uwongo? Walipata nini? Acheni tuone.

‘ACHENI BIBLIA ITUONGOZE SIKUZOTE’

Wolfgang Capito, alikuwa kijana aliyekuwa mfuasi wa dini. Alisomea tiba, sheria, na theolojia na akawa kasisi katika parokia mwaka wa 1512 kisha akawa kasisi aliyeshirikiana na askofu mkuu wa Mainz.

Mwanzoni, Capito alijaribu kupunguza bidii ya wanaharakati wa Marekebisho ya Kidini waliopinga mafundisho ya Kikatoliki. Hata hivyo, baada ya muda Capito alianza kuunga mkono Marekebisho ya Kidini. Alifanya nini? Alipochunguza mafundisho mbalimbali, Capito aliamini kwamba “chanzo bora cha kuamua mafundisho ya kidini ni Biblia, kwa sababu ilikuwa na mambo hakika,” akaandika mwanahistoria James M. Kittelson. Hivyo, Capito alifikia mkataa kuwa Maandiko hayaungi mkono ibada ya watakatifu na fundisho la kanisa kwamba mkate na divai hugeuka kimuujiza na kuwa mwili na damu halisi ya Yesu. (Ona sanduku “ Ili Kuona Kama Mambo Hayo Ndivyo Yalivyo.”) Mwaka wa 1523, Capito aliacha cheo chake cha kutumika pamoja na askofu mkuu, na akahamia jiji la Strasbourg, ambalo lilikuwa kitovu cha Marekebisho ya Kidini.

Nyumba ya Capito huko Strasbourg ikawa mahali walipokutana watu walioshuku mafundisho  ya dini ili kuzungumzia mambo ya kidini na Biblia. Ingawa baadhi ya wanaharakati wa Marekebisho ya Kidini waliunga mkono fundisho la Utatu, kulingana na kitabu The Radical Reformation, maandishi ya Capito “hayakutaja Utatu.” Kwa nini? Capito alipendezwa na jinsi mwanatheolojia Mhispania, Michael Servetus alivyotumia Biblia kupinga Utatu. *

Mtu aliyepinga fundisho la Utatu angeadhibiwa vikali, basi Capito alikuwa mwangalifu kuhusu kutangaza msimamo wake. Hata hivyo, maandishi yake yanaonyesha kwamba alishuku fundisho la Utatu hata kabla hajakutana na Servetus. Baadaye, kasisi fulani Mkatoliki aliandika kwamba Capito na wenzake “walizungumzia faraghani mafundisho yasiyoeleweka ya kidini na wakapinga Utatu Mtakatifu.” Miaka mia moja baadaye, Capito aliorodheshwa wa kwanza kati ya waandikaji maarufu waliopinga Utatu.

Wolfgang Capito aliamini kwamba “kupuuza Maandiko” ndilo kosa kubwa lililofanywa na kanisa

Capito aliamini kwamba Biblia ndicho chanzo cha ukweli. Aliandika hivi: “Sikuzote acheni Biblia na sheria ya Kristo iongoze mafundisho ya theolojia.” Kulingana na Dakt. Kittelson, Capito “alisisitiza kwamba kasoro kubwa ya wanatheolojia ni kupuuza Maandiko.”

Martin Cellarius (anayejulikana pia kama Martin Borrhaus), kijana aliyeishi katika nyumba ya Capito mwaka wa 1526, alikuwa pia na tamaa hiyo ya kujua ukweli wa Neno la Mungu.

“UJUZI KUMHUSU MUNGU WA KWELI”

Ukurasa wa kwanza wa kitabu On the Works of God, cha Martin Cellarius ambamo alilinganisha itikadi za kanisa na mafundisho ya Biblia

Cellarius alizaliwa 1499 na alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa theolojia na falsafa. Alianza kufanya kazi ya ualimu huko Wittenberg, Ujerumani. Kwa kuwa Marekebisho ya Kidini yalianzia huko Wittenberg, baada ya muda Cellarius alifahamiana na Martin Luther na watu wengine waliotaka kurekebisha mafundisho ya kanisa. Cellarius angetofautishaje kati ya mawazo ya wanadamu na mafundisho ya Biblia?

Kulingana na kitabu Teaching the Reformation, Cellarius aliamini kwamba ufahamu wa kweli hutokana na “kujifunza Maandiko kwa bidii, kulinganisha Maandiko kwa ukawaida, kusali, na vilevile kutubu.” Cellarius alipata nini baada ya kuichunguza Biblia?

Mnamo Julai 1527, Cellarius alichapisha kitabu On the Works of God (Kuhusu Kazi za Mungu), kilichokuwa na mambo aliyojifunza. Aliandika kwamba sakramenti, yaani, mkate na divai ilikuwa mifano tu. Kulingana na Profesa Robin Barnes, pia kitabu cha Cellarius “kilikuwa na ufafanuzi wa unabii wa maandiko kuhusu kipindi kinachokuja cha msiba mkubwa na mateso ambacho kingefuatwa na marekebisho ya ulimwenguni pote.”2 Petro 3:10-13.

Jambo lingine la kupendeza ni maelezo ya Cellarius kumhusu Yesu Kristo. Ingawa hakupinga Utatu moja kwa moja, Cellarius alionyesha tofauti kati ya “Baba wa Mbinguni” na “Mwanawe Yesu Kristo” na akaandika kwamba Yesu alikuwa mmoja kati ya miungu na wana wengi wa Mungu Mweza-Yote.Yohana 10:34, 35.

Kitabu cha Robert Wallace kinachoitwa Antitrinitarian Biography (1850), kinasema kwamba maandishi ya Cellarius hayakufuata fundisho la Utatu lililoenezwa sana katika karne ya 16. *  Wasomi fulani wamesema kwamba Cellarius alipinga Utatu. Amefafanuliwa kuwa mtu aliyetumiwa na Mungu “kufundisha ujuzi kumhusu Mungu wa kweli na Kristo.”

TUMAINI LA MAREKEBISHO YA KIDINI

Karibu mwaka wa 1527, Johannes Campanus aliyeonwa kuwa msomi bora nyakati hizo, vilevile alihamia Wittenberg. Ingawa alihusika na shughuli za Marekebisho ya Kidini, Campanus hakukubaliana na mafundisho ya Martin Luther. Kwa nini?

Campanus hakuamini mkate na divai hugeuka na kuwa mwili halisi wa Yesu na pia hakuamini kuunganishwa kwa mifano hiyo. * Kulingana na mwandishi André Séguenny, Campanus aliamini kwamba “Mkate hubaki kuwa mkate, lakini sakramenti, huwakilisha mwili wa Kristo.” Kwenye mkutano uliofanywa huko Marburg Colloquy ili kujadili jambo hilo, Campanus hakuruhusiwa kueleza mambo aliyojifunza katika Biblia. Baadaye aliepukwa na wanaharakati wenzake wa Marekebisho ya Kidini huko Wittenberg.

Katika kitabu chake cha Restitution, Johannes Campanus alipinga fundisho la Utatu

Wanaharakati wa marekebisho ya kidini hasa walikasirishwa na itikadi ya Campanus kuhusu Baba, Mwana, na roho takatifu. Katika kitabu chake cha 1532 kiitwacho Restitution, Campanus alifundisha kwamba Yesu na Baba yake ni watu wawili tofauti. Alieleza kwamba Baba na Mwana ni “kitu kimoja,” kama vile mume na mke wanavyounganishwa kuwa “mwili mmoja,” lakini ni watu wawili tofauti. (Yohana 10:30; Mathayo 19:5) Campanus alisema Maandiko yanatumia ulinganisho huo kuonyesha kwamba Baba ana mamlaka kuliko Mwana: “Kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.”1 Wakorintho 11:3.

Namna gani roho takatifu? Vilevile Campanus alitumia Biblia kusema: “Hakuna andiko linaloonyesha kwamba Roho Takatifu ndiye mtu wa tatu . . . Roho ya Mungu hutumiwa kutenda, kwamba Mungu hutayarisha na kufanya mambo yote kupitia nguvu zake za kiroho.”Mwanzo 1:2.

Luther alimwita Campanus mkufuru na adui wa Mwana wa Mungu. Mwanaharakati mwingine wa marekebisho alipendekeza Campanus auawe. Lakini Campanus hakuvunjika moyo. Kulingana na kitabu The Radical Reformation, “Campanus alisadiki kwamba Kanisa lilipotea baada ya kuacha mafundisho ya kwanza ya Biblia yaliyofuatwa na mitume kuhusu cheo cha Mungu na hali ya wanadamu.”

Campanus hakukusudia kamwe kuanzisha kikundi cha kidini. Alikuwa ametafuta ukweli “kati ya madhehebu na wanaharakati wa marekebisho,” lakini hakuupata. Basi alitumaini kwamba Kanisa Katoliki, lingefanya marekebisho na kurudisha mafundisho ya kweli ya Kikristo. Hata hivyo, viongozi Wakatoliki walimkamata Campanus, na huenda alifungwa zaidi ya miaka 20 gerezani. Wanahistoria wanaamini kwamba alikufa karibu mwaka wa 1575.

 “HAKIKISHENI MAMBO YOTE”

Kujifunza Biblia kwa bidii kuliwasaidia, Capito, Cellarius, Campanus, na wengine kutofautisha kati ya ukweli na uwongo. Ingawa baadhi ya mambo waliyoamini hayakuwa sahihi, wanaume hao walichunguza Maandiko kwa unyenyekevu na wakathamini ukweli waliojifunza.

Mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana yaliyo mazuri.” (1 Wathesalonike 5:21) Ili kukusaidia katika jitihada zako za kutafuta ukweli, Mashahidi wa Yehova wamechapisha kitabu kinachoitwa Biblia Inafundisha Nini Hasa? Ili upate nakala bila malipo, tafadhali ona ukurasa wa 16 wa gazeti hili, au utembelee Tovuti yetu, jw.org/sw.

^ fu. 4 Ona sanduku “Acheni Vyote Viwili Vikue Pamoja Mpaka Mavuno,” kwenye ukurasa wa 44 wa kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 8 Ona makala “Michael Servetus—Alitafuta Ukweli Akiwa Peke Yake,” katika gazeti Amkeni! la Mei 2006 lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 17 Kuhusu jinsi Cellarius alivyotumia neno “mungu” kurejelea Kristo, kitabu hicho kinasema: “Limechapishwa deus, na si Deus, jina hilo la pili linatumiwa tu kumtambulisha Mungu Mweza-Yote.”

^ fu. 20 Kuunganishwa kwa sakarementi ni fundisho la Luther kwamba mkate na divai “huungana” na mwili wa Kristo wakati wa Mlo wa Bwana.