Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | MAONI YA MUNGU KUHUSU KUVUTA SIGARA

Maoni ya Mungu Kuhusu Kuvuta Sigara

Maoni ya Mungu Kuhusu Kuvuta Sigara

Naoko, aliyetajwa kwenye makala ya kwanza, anasema hivi kuhusu kilichomsaidia aache kuvuta sigara: “Nilibadili maisha yangu baada ya kujifunza kuhusu sifa na kusudi la Mungu.” Mambo aliyojifunza yanapatikana kwenye Biblia. Ingawa Biblia haitaji tumbaku, inatusaidia kujua maoni ya Mungu kuhusu kuvuta sigara. * Ujuzi wa Biblia umewasaidia watu wengi kuepuka au kuacha kuvuta sigara. (2 Timotheo 3:16, 17) Acheni tuchunguze madhara matatu yanayojulikana sana ya kuvuta sigara na tuone maoni ya Biblia.

HUSABABISHA URAIBU

Tumbaku ina kemikali iitwayo nikotini ambayo husababisha uraibu haraka zaidi. Nikotini husisimua na vilevile kutuliza hisia. Kuvuta sigara hupeleka nikotini haraka kwenye ubongo tena na tena. Mvuto mmoja wa sigara ni sawa na dozi moja, hivyo mvutaji wa kawaida anaweza kuvuta dozi 200 kwa siku, ambacho ni kiwango cha juu kuliko dawa yoyote ile. Ndiyo maana nikotini husababisha uraibu mkubwa sana. Mtu aliyezoea kuvuta sigara hujihisi vibaya anapokawia kuvuta.

“Unakuwa mtumwa wa yule unayemtii.”Waroma 6:16

Je, inawezekana kumtii Mungu na wakati uleule uwe mtumwa wa sigara?

Biblia inatusaidia kuelewa jambo hilo inaposema hivi: “Je, hamjui kwamba ikiwa mnaendelea kujitoa wenyewe kwa yeyote kuwa watumwa ili kumtii yeye, ninyi ni watumwa wake kwa sababu mnamtii yeye?” (Waroma 6:16) Mtu anapofikiria kila mara kuhusu kuvuta sigara, anakuwa mtumwa wa tabia chafu. Hata hivyo, Mungu, ambaye jina lake ni Yehova, anataka tuwe huru, si uhuru tu wa kuepuka madhara ya kimwili bali pia madhara ya kiroho, yaani, mtazamo wetu wa akili. (Zaburi 83:18; 2 Wakorintho 7:1) Hivyo, mtu anapojifunza kumpenda na kumheshimu Yehova, anatambua kwamba Mungu anastahili kilicho bora na kwamba hawezi kumtumikia Mungu huku akiwa mtumwa wa tabia inayodhuru. Mtu akitambua ukweli huo atachochewa kuepuka tamaa mbaya.

Olaf, anayeishi Ujerumani alianza kuvuta sigara alipokuwa na umri wa miaka 12, na alifanikiwa kushinda zoea hilo lililodumu miaka 16. Alisema hivi: “Nilipovuta sigara mara ya kwanza sikuona ubaya wowote. Lakini baada ya miaka kadhaa ikawa vigumu sana kuacha. Siku moja sikuwa na sigara, nilikata tamaa hivi kwamba nikakusanya vipande vya mabaki ya sigara na kutengeneza sigara kwa kutumia karatasi. Ninapokumbuka jambo hilo ninaaibika sana.” Aliachaje kuvuta sigara? Anasema hivi, “Jambo lililonisaidia ni tamaa yangu ya kumpendeza Yehova. Niliacha kabisa baada ya kujifunza kuhusu  upendo wa Mungu kwa wanadamu na tumaini la wakati ujao.”

KUVUTA SIGARA HUHARIBU MWILI

Jarida The Tobacco Atlas linasema hivi: “Kuvuta sigara . . . kumethibitishwa kisayansi kwamba kunadhuru karibu viungo vyote mwilini na husababisha magonjwa na kifo.” Inajulikana kwamba kuvuta sigara husababisha magonjwa kama vile kansa, ugonjwa wa moyo, na wa mapafu. Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, kuvuta sigara ni chanzo kikuu cha vifo vitokanavyo na magonjwa ya kuambukiza kama vile kifua kikuu.

“Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.”Mathayo 22:37

Je, unamheshimu Mungu na kumpenda ikiwa unauchafua mwili aliokupa kwa kuvuta sigara?

Kupitia Neno lake, Biblia, Yehova Mungu anatufundisha jinsi ya kuwa na maoni yanayofaa kuhusu uhai, mwili na uwezo wetu. Mwanaye, Yesu, alikazia jambo hilo aliposema hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Bila shaka, Mungu anataka tutumie vizuri na kuthamini uhai na mwili wetu. Tunapoendelea kujifunza kumhusu Yehova na ahadi zake, tutapendezwa na kuthamini wema wake. Hilo litatuchochea kuepuka jambo lolote linalochafua mwili wetu.

Jayavanth, ambaye ni daktari nchini India, alivuta sigara kwa miaka 38. Anasema hivi: “Nilisoma kuhusu madhara ya kuvuta sigara kwenye majarida mbalimbali ya afya. Nilijua ubaya wa kuvuta sigara na niliwashauri wagonjwa waache sigara. Hata hivyo, nilishindwa kuacha licha ya kujaribu mara tano au sita.” Ni nini kilichomsaidia afaulu? Anasema: “Niliacha kuvuta sigara baada ya kujifunza Biblia. Tamaa ya kumpendeza Yehova ilinichochea kuacha kabisa tabia hiyo.”

KUVUTA SIGARA HUWADHURU WENGINE

Moshi wa sigara una madhara sana. Kupumua moshi unaotoka kwa mtu anayevuta sigara kunaweza kusababisha kansa na magonjwa mengine, na kila mwaka watu 600,000 wasiovuta sigara hufa, hasa wanawake na watoto. Shirika la Afya Ulimwenguni linaonya hivi: “Moshi wa sigara  unaweza kumdhuru mtu asiyevuta bila kujali kiwango cha moshi anachopumua.”

“Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.”Mathayo 22:39

Je, unaweza kuwapenda watu wa familia yako na jirani zako ikiwa unahatarisha uhai wao kwa moshi wa sigara?

Kulingana na Yesu, kumpenda jirani, yaani, familia yetu, rafiki zetu, na wengine ni amri ya pili, ya kwanza ikiwa ni kumpenda Mungu. Yesu alisema hivi: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:39) Tukiwa na tabia inayowadhuru wengine, hatuwezi kusema tunampenda jirani. Upendo wa kweli unatuchochea kufuata ushauri huu wa Biblia: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.

Armen, anayeishi Armenia anakumbuka hivi: “Watu wa familia yangu walinisihi niache kuvuta sigara kwa sababu iliwaathiri. Hata hivyo, sikukubali kwamba kuvuta sigara kuliwasababishia matatizo.” Anasema hivi kuhusu kilichomsaidia: “Mambo niliyojifunza katika Biblia na kumpenda Yehova kulinisaidia niache kuvuta sigara na kukubali kwamba kuvuta sigara kuliniathiri mimi na wengine pia.”

KUVUTA SIGARA KUTAKOMESHWA MILELE!

Kujifunza Biblia kuliwasaidia Olaf, Jayavanth, na Armen kuacha tabia iliyowadhuru wao wenyewe na pia watu wengine. Waliacha kuvuta sigara si kwa sababu tu walijua madhara yake, bali pia kwa kuwa walimpenda Yehova walitamani kumfurahisha. Upendo unakaziwa kwenye andiko 1 Yohana 5:3, linalosema: “Kwa maana kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” Huenda ikawa vigumu kufuata kanuni za Biblia, lakini ukimpenda Mungu kwa moyo wote, ni rahisi kumtii.

Kupitia mpango wa elimu wa ulimwenguni pote, Yehova Mungu anawaweka watu huru kutoka kwenye utumwa wa tumbaku. (1 Timotheo 2:3, 4) Hivi karibuni, Yehova kupitia Ufalme wake, yaani, serikali ya mbinguni inayoongozwa na Mwanawe, Yesu Kristo, ataondoa mfumo wa kibiashara wenye pupa ambao umesababisha mamilioni ya watu kuwa watumwa wa tumbaku. Ataondoa janga la kuvuta sigara na kuwasaidia wanadamu kuwa wakamilifu kimwili na kiakili.—Isaya 33:24; Ufunuo 19:11, 15.

Ikiwa unatamani kuacha kuvuta sigara, usikate tamaa. Ukijifunza kumpenda Yehova na kukubali maoni yake, wewe pia unaweza kufanikiwa kuacha kuvuta sigara. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia ujifunze na kutumia kanuni za Biblia. Uwe na uhakika kwamba kama unatamani Yehova akusaidie kuacha kuvuta sigara, atakupatia nguvu unazohitaji ili ufanikiwe.—Wafilipi 4:13.

^ fu. 3 Katika makala hii kuvuta sigara kunatia ndani kuvuta moshi wa sigara, kiko, au kupitia mirija. Hata hivyo, kanuni zinazozungumziwa katika makala hii zinahusu mambo kama vile kutafuna tumbaku, kunusa, kuvuta sigara za kielektroniki iliyo na nikotini, na matumizi mengineyo.