Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Mashahidi wa Yehova Ni Nani?

Mashahidi wa Yehova Ni Nani?

“Kwa miaka mingi nimemfahamu Mike. Ni Shahidi wa Yehova. Hata hivyo nimeshindwa kuielewa dini yake. Yehova ni nani? Kwa nini Mashahidi hawasherehekei sikukuu? Je, Mike alikuwa akijihusisha na dhehebu la ajabu?”—Becky, California, Marekani.

“Jirani zangu walipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, niliwaza hivi: ‘Jina Mashahidi wa Yehova linamaanisha nini? Jina la dini hiyo ni la ajabu sana!’”—Zenon, Ontario, Kanada.

“Mimi na mke wangu tulifikiri kwamba Mashahidi wa Yehova walitutembelea kwa kuwa hatukwenda kanisani siku hiyo. Tulifikiri pia kwamba ikiwa makanisa makubwa hayakuwa na kile tulichokuwa tunatafuta, dhehebu la ajabu la Mashahidi wa Yehova halitaweza.”—Kent, Washington, Marekani.

“Kusema kweli, sikujua wao ni nani na wanaamini nini.”—Cecilie, Esbjerg, Denmark.

Huenda umewaona wakihubiri nyumba kwa nyumba au hadharani, wakitoa machapisho yanayotegemea Biblia, na kuwafundisha watu Biblia bila malipo. Huenda umepewa gazeti hili na mmoja wao. Hata hivyo, bado unajiuliza, Mashahidi wa Yehova ni nani? Huenda una maoni kama ya watu walionukuliwa mwanzoni.

Utapata wapi majibu ya maswali hayo? Utaijuaje imani ya Mashahidi wa Yehova, jinsi huduma na majumba yao ya ibada yanavyogharimiwa, na kwa nini wao hukutembelea nyumbani kwako na kukuhubiria katika maeneo ya umma?

“Nilisoma mambo mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova katika Intaneti. Nilisikia uvumi na kuwasikiliza watu wengi wakisema vibaya kuwahusu. Matokeo ni kwamba nilianza kuwa na maoni mabaya kuhusu Mashahidi wa Yehova,” anasema Cecilie. Hata hivyo, baada ya muda fulani alizungumza na Mashahidi wa Yehova na akapata majibu yenye kuridhisha.

Je, ungependa kupata majibu sahihi ya maswali yako kuhusu Mashahidi wa Yehova? Tunakutia moyo utafute majibu sahihi kutoka kwa Mashahidi wa Yehova, wachapishaji wa gazeti hili. (Methali 14:15) Tunatumaini kwamba makala zinazofuata zitakusaidia utufahamu sisi, imani yetu, na kazi tunayofanya.