Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msaada kwa Wanaotendewa kwa Jeuri Nyumbani

Msaada kwa Wanaotendewa kwa Jeuri Nyumbani

 “Jeuri dhidi ya wanawake ni tatizo kubwa la kiafya linalohitaji kushughulikiwa haraka kama tu ugonjwa wa mlipuko,” linasema Shirika la Afya Duniani. Shirika hilo linakadiria kwamba asilimia 30 ya “wanawake wote walioolewa au waliokuwa katika mahusiano, wametendewa kwa jeuri iwe kwa kupigwa kihalisi au kutendewa vibaya kingono” na wenzi wao. Ripoti ya Umoja wa Mataifa inakadiria kwamba katika kipindi cha mwaka mmoja, wanawake 137 walikufa kila siku duniani baada ya kutendewa kwa jeuri na mwenzi wao au mtu wa familia. a

 Ijapokuwa takwimu hizo zinaonyesha ukubwa wa tatizo la kutendewa kwa jeuri nyumbani, haziwezi kutuelezea maumivu halisi na ya kihisia wanayopata wale wanaotendewa kwa jeuri.

 Je, unatendewa kwa jeuri? Au je, unamfahamu mtu anayetendewa hivyo? Ikiwa ndiyo, ona msaada unaopatikana katika Biblia.

  Si kosa lako hivi kwamba unatendewa kijeuri

  Unaweza kupata msaada

  Hauko peke yako

  Kutendewa kwa jeuri kutakwisha

  Jinsi unavyoweza kumsaidia anayetendewa kwa jeuri

 Si kosa lako hivi kwamba unatendewa kijeuri

 Biblia inasema nini: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Waroma 14:12.

 Kumbuka jambo hili: Anayekutendea kwa jeuri atatoa hesabu.

 Ikiwa mwenzi wako anakulaumu wewe kwamba matendo yako ndiyo chanzo cha yeye kukutendea kwa jeuri, hayuko sahihi. Wake wanapaswa kupendwa wala si kutendewa kwa jeuri.—Wakolosai 3:19.

 Wakati mwingine, huenda anayekutendea kwa jeuri anafanya hivyo kwa sababu ya matatizo ya kihisia, malezi, au matumizi mabaya ya kileo. Hata hivyo, bado atatoa hesabu machoni pa Mungu kwa jinsi anavyokutendea. Pia, ni jukumu lake kufanya yote awezayo kubadili tabia yake.

 Unaweza kupata msaada

 Biblia inasema nini: “Mambo hufanikiwa kupitia washauri wengi.”—Methali 15:22.

 Kumbuka jambo hili: Ikiwa unahisi hauko salama au haujui la kufanya, wengine wanaweza kukusaidia.

 Kwa nini huenda ukahitaji msaada kutoka kwa wengine? Kuna mambo mengi yanayohusika mtu anapotendewa kwa jeuri. Huenda isiwe rahisi kwako kuamua jambo linalofaa kufanya kwa kuwa haujui ni mambo gani muhimu kati ya haya:

  •   Usalama wako

  •   Uamuzi utakaowafaa watoto wako

  •   Hali yako ya kifedha

  •   Upendo wako kwa mwenzi wako

  •   Tamaa yako ya kuendelea na uhusiano ikiwa mwenzi wako ataacha vitendo vyake

 Ni kweli kwamba huenda ukahisi umechanganyikiwa na usijue jambo la kufanya. Unaweza kupata wapi msaada?

 Rafiki au ndugu wa familia anayetegemeka anaweza kukusaidia kwa maneno na matendo. Kuongea na mtu anayekujali kunaweza kuwa na matokeo mazuri sana.

 Piga simu katika vituo vinavyotoa msaada kwa wanaotendewa kwa jeuri ambapo utapata msaada bila kukawia. Wahudumu wa vituo hivyo wanaweza kukusaidia kujua jambo la kufanya ili uwe salama. Ikiwa mwenzi wako atatambua kwamba ana tatizo na kwa unyoofu atataka kubadilika, wahudumu wa vituo hivyo wanaweza kumsaidia kwa kumwambia hatua za kwanza anazopaswa kuchukua.

 Vyanzo vingine vya msaada wakati wa dharura vinaweza kukusaidia ukiwa hatarini na unahitaji msaada wa haraka. Vyanzo hivyo vinatia ndani madaktari, wauguzi, au wataalamu wengine waliozoezwa kushughulikia hali hizo.

 Hauko peke yako

 Biblia inasema nini: “Yehova b yuko karibu na wale waliovunjika moyo; huwaokoa waliopondeka roho.”—Zaburi 34:18.

 Kumbuka jambo hili: Mungu ameahidi kukusaidia.

 Yehova anakujali sana. (1 Petro 5:7) Anaelewa vizuri sana mawazo na hisia zako za ndani kabisa. Anaweza kukufariji kupitia Neno Lake, Biblia. Angependa uzungumze naye kupitia sala. Unaposali, unaweza kumwomba akupatie hekima na nguvu utakazohitaji ili kushughulikia hali yako.—Isaya 41:10.

 Kutendewa kwa jeuri kutakwisha

 Biblia inasema nini: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, na hakuna yeyote atakayewaogopesha.”—Mika 4:4, maelezo ya chini.

 Kumbuka jambo hili: Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni familia zote zitaishi kwa amani.

 Ni Yehova Mungu peke yake atakayeondoa kabisa matatizo yetu yote. Biblia inatuahidi hivi: “Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Wakati huo hatutakumbuka tena mambo mabaya badala yake tutafurahia mambo mengi mazuri. (Isaya 65:17) Biblia inakupatia wewe ahadi hizo za wakati ujao utakaokuwa na amani.

a Ingawa makala hii inataja wanawake kuwa ndio wanaotendewa kwa jeuri, mambo mengi yanayotajwa yanawahusu pia wanaume wanaokabili hali hizo.

b Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.