Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA NNE

Yesu Kristo Ni Nani?

Yesu Kristo Ni Nani?
  • Yesu ana jukumu gani muhimu?

  • Alitoka wapi?

  • Alikuwa mtu wa aina gani?

1, 2. (a) Kwa nini kujua jina la mtu mashuhuri hakumaanishi kwamba unamjua vizuri? (b) Watu wana maoni gani yanayotofautiana kumhusu Yesu?

KUNA watu wengi mashuhuri ulimwenguni. Baadhi yao wanajulikana sana katika jamii zao, majiji yao, au nchi zao. Wengine wanajulikana ulimwenguni pote. Hata hivyo, kujua tu jina la mtu fulani mashuhuri, hakumaanishi kwamba unamjua vizuri. Haimaanishi kwamba unajua malezi yake na utu wake kabisa.

2 Watu ulimwenguni pote wamesikia kumhusu Yesu Kristo, ingawa aliishi duniani miaka 2,000 hivi iliyopita. Hata hivyo, wengi hawajui kwa kweli Yesu alikuwa nani. Baadhi yao husema kwamba alikuwa mtu mzuri tu. Wengine wanadai kwamba alikuwa nabii tu. Na wengine wanaamini kwamba Yesu ni Mungu na anapaswa kuabudiwa. Je, anapaswa kuabudiwa?

3. Kwa nini ni muhimu ujue ukweli kumhusu Yesu?

3 Ni muhimu ujue ukweli kumhusu Yesu. Kwa nini? Kwa sababu Biblia inasema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Ndiyo, kujua ukweli kumhusu Yehova Mungu na Yesu Kristo kutakuwezesha kupata uzima wa milele katika paradiso duniani. (Yohana 14:6) Isitoshe, Yesu alionyesha kwa njia bora zaidi jinsi ya kuishi na kuwatendea wengine. (Yohana 13:34, 35) Katika sura ya kwanza ya kitabu hiki tulizungumzia ukweli kumhusu Mungu. Sasa, na tuchunguze mambo ambayo Biblia inafundisha kumhusu Yesu Kristo.

MASIHI ALIYEAHIDIWA

4. Majina “Masihi” na “Kristo” yanamaanisha nini?

4 Zamani kabla ya Yesu kuzaliwa, Biblia ilikuwa imetabiri kuja kwa yule ambaye Mungu angemtuma akiwa Masihi, au Kristo. Majina “Masihi” (kutokana na neno la Kiebrania) na “Kristo” (kutokana na neno la Kigiriki) yanamaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Huyo aliyeahidiwa angetiwa mafuta, yaani, angewekwa rasmi na Mungu katika cheo cha pekee. Katika sura za baadaye za kitabu hiki, tutajifunza mengi kuhusu jukumu muhimu la Masihi kuhusiana na kutimia kwa ahadi za Mungu. Pia tutajifunza kuhusu baraka ambazo Yesu anaweza kutuletea hata sasa. Hata hivyo, kabla Yesu hajazaliwa, watu wengi walijiuliza, ‘Ni nani atakayekuwa Masihi?’

5. Wanafunzi wa Yesu walisadiki nini kumhusu?

5 Katika karne ya kwanza W.K., wanafunzi wa Yesu wa Nazareti walisadiki kabisa kwamba ndiye alikuwa Masihi aliyeahidiwa. (Yohana 1:41) Simoni Petro, mmoja wa wanafunzi hao, alimwambia Yesu waziwazi: “Wewe ndiye Kristo.” (Mathayo 16:16) Hata hivyo, wanafunzi hao wangewezaje kuwa na hakika kwamba Yesu kwa kweli ndiye Masihi aliyeahidiwa? Namna gani sisi?

6. Toa mfano unaoonyesha jinsi Yehova amewasaidia watu waaminifu kumtambua Masihi.

6 Manabii wa Mungu walioishi kabla ya Yesu walitabiri mambo mengi kumhusu Masihi. Mambo hayo yangewasaidia watu wengine kumtambua. Kwa mfano: Tuseme umeombwa uende kwenye kituo cha mabasi chenye shughuli nyingi au kwenye kituo cha magari-moshi au kwenye uwanja wa ndege kumpokea mtu ambaye hujapata kukutana naye. Ingefaa ikiwa mtu fulani angekupa habari zaidi kumhusu, sivyo? Vivyo hivyo, kupitia manabii wa Biblia, Yehova ametueleza mambo mengi kuhusu utendaji wa Masihi na mambo ambayo yangempata. Kutimia kwa unabii huo mbalimbali kungewasaidia watu waaminifu wamtambue waziwazi.

7. Ni mambo gani mawili yaliyotabiriwa kuhusiana na Yesu ambayo yalitimia?

7 Fikiria mifano miwili tu. Kwanza, zaidi ya miaka 700 mapema, nabii Mika alitabiri kwamba Yule aliyeahidiwa angezaliwa Bethlehemu, mji mdogo katika Yuda. (Mika 5:2) Yesu alizaliwa wapi hasa? Katika mji huohuo! (Mathayo 2:1, 3-9) Pili, karne nyingi mapema, unabii ulio katika Danieli 9:25 ulionyesha mwaka hususa ambao Masihi angetokea, yaani, 29 W.K. * Kutimia kwa unabii huo na unabii mwingine mbalimbali kunathibitisha kwamba Yesu alikuwa Masihi aliyeahidiwa.

Baada ya kubatizwa, Yesu akawa Masihi, au Kristo

8, 9. Uthibitisho wa kwamba Yesu alikuwa Masihi ulionekanaje wazi alipobatizwa?

8 Uthibitisho zaidi wa kwamba Yesu ndiye Masihi ulionekana wazi mwishoni mwa mwaka wa 29 W.K. Huo ndio mwaka ambao Yesu alimwendea Yohana Mbatizaji ili abatizwe katika Mto Yordani. Yehova alikuwa amemwahidi Yohana kwamba angempa ishara ili amtambue Masihi. Yohana aliona ishara hiyo Yesu alipobatizwa. Biblia inasimulia lililotukia: “Baada ya kubatizwa Yesu akapanda mara moja kutoka katika maji; na, tazama! mbingu zikafunguliwa, naye akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu yake. Tazama! Kulikuwa pia na sauti kutoka mbinguni iliyosema: ‘Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.’” (Mathayo 3:16, 17) Baada ya kusikia na kuona kilichotukia, Yohana hakuwa na shaka kwamba Yesu alitumwa na Mungu. (Yohana 1:32-34) Wakati roho ya Mungu au nguvu ya utendaji ilipomiminwa juu yake siku hiyo, Yesu akawa Masihi au Kristo, ambaye aliwekwa rasmi kuwa Kiongozi na Mfalme.—Isaya 55:4.

9 Utimizo wa unabii wa Biblia na ushuhuda wa Mungu mwenyewe unaonyesha wazi kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. Lakini Biblia inajibu maswali mengine mawili muhimu kumhusu Yesu Kristo: Alitoka wapi? Na alipokuwa mwanadamu, alikuwa mtu wa aina gani?

YESU ALITOKA WAPI?

10. Biblia inafundisha nini kuhusu maisha ya Yesu kabla ya kuja duniani?

10 Biblia inafundisha kwamba Yesu aliishi mbinguni kabla ya kuja duniani. Mika alitabiri kwamba Masihi angezaliwa Bethlehemu na alisema pia kwamba asili Yake “ni kutoka nyakati za kale.” (Mika 5:2) Mara nyingi, Yesu mwenyewe alisema kwamba aliishi mbinguni kabla ya kuwa mwanadamu. (Yohana 3:13; 6:38, 62; 17:4, 5) Akiwa kiumbe wa roho mbinguni, Yesu alikuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Yehova.

11. Biblia inaonyeshaje kwamba Yesu ndiye Mwana mpendwa zaidi wa Yehova?

11 Yesu ni Mwana mpendwa zaidi wa Yehova—na kuna sababu nzuri. Anaitwa “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” kwa sababu aliumbwa kwanza na Mungu. * (Wakolosai 1:15) Kuna jambo lingine linalomfanya Mwana huyu awe wa pekee. Yeye ni ‘Mwana mzaliwa-pekee.’ (Yohana 3:16) Hilo linamaanisha kwamba ni Yesu peke yake aliyeumbwa moja kwa moja na Mungu. Pia Mungu alimtumia Yesu peke yake kuumba vitu vingine vyote. (Wakolosai 1:16) Pia, Yesu anaitwa “Neno.” (Yohana 1:14) Hilo linamaanisha kwamba alizungumza kwa niaba ya Mungu, akiwasilisha ujumbe na maagizo kwa wana wengine wa Baba yake, yaani, malaika na wanadamu.

12. Tunajuaje kwamba Mwana mzaliwa wa kwanza halingani na Mungu?

12 Je, Mwana huyo mzaliwa wa kwanza yuko sawa na Mungu kama wengine wanavyoamini? Biblia haifundishi hivyo. Kama tulivyoona katika fungu lililotangulia, Mwana huyo aliumbwa. Basi ni wazi kwamba alikuwa na mwanzo, lakini Yehova Mungu hana mwanzo wala mwisho. (Zaburi 90:2) Mwana huyo mzaliwa-pekee hakujaribu kamwe kuwa sawa na Baba yake. Biblia inafundisha wazi kwamba Baba ni mkuu kuliko Mwana. (Yohana 14:28; 1 Wakorintho 11:3) Yehova peke yake ndiye “Mungu Mweza-Yote.” (Mwanzo 17:1) Kwa hiyo, hakuna yeyote anayelingana naye. *

13. Biblia humaanisha nini inapomwita Mwana “mfano wa Mungu asiyeonekana”?

13 Yehova na Mwana mzaliwa wake wa kwanza walikuwa na uhusiano wa karibu mabilioni ya miaka kabla ya mbingu zenye nyota na dunia kuumbwa. Walipendana kwelikweli! (Yohana 3:35; 14:31) Mwana huyo mpendwa alikuwa tu kama Baba yake. Ndiyo sababu Biblia inamwita Mwana huyo “mfano wa Mungu asiyeonekana.” (Wakolosai 1:15) Ndiyo, kama vile mwana wa mwanadamu anavyoweza kufanana na baba yake katika njia mbalimbali, Mwana huyo wa kimbingu alionyesha sifa na utu wa Baba yake.

14. Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova alizaliwaje akiwa mwanadamu?

14 Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova alikubali kuacha makao yake mbinguni na kuja kuishi duniani kama mwanadamu. Lakini huenda ukajiuliza, ‘Iliwezekanaje kiumbe wa roho kuzaliwa kama mwanadamu?’ Ili kutimiza hilo, Yehova alifanya muujiza. Alihamisha uhai wa Mwana wake wa kwanza kutoka mbinguni na kuutia katika tumbo la bikira Myahudi aliyeitwa Maria. Yesu hakuwa na baba wa kibinadamu. Basi, Maria alimzaa mwana mkamilifu na kumwita Yesu.—Luka 1:30-35.

YESU ALIKUWA MTU WA AINA GANI?

15. Tunawezaje kumjua Yehova vizuri zaidi kupitia Yesu?

15 Mambo ambayo Yesu alisema na kutenda alipokuwa duniani yanatusaidia kumjua vizuri. Pia, kupitia Yesu tunapata kumjua Yehova vizuri zaidi. Kwa nini? Kumbuka kwamba Mwana huyo anamwakilisha Baba yake kikamilifu. Ndiyo sababu Yesu alimwambia mwanafunzi wake hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Vitabu vinne vya Biblia vinavyoitwa Injili, yaani, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana, vinatuambia mengi kuhusu maisha, utendaji, na sifa za Yesu Kristo.

16. Yesu alifundisha ujumbe gani wa msingi, nayo mafundisho yake yalitoka wapi?

16 Watu wengi walimjua Yesu kuwa “Mwalimu.” (Yohana 1:38; 13:13) Alifundisha nini? Ujumbe wake wa msingi ulikuwa “habari njema ya ufalme,” yaani, Ufalme wa Mungu, serikali ya mbinguni itakayotawala dunia nzima na kuwaletea wanadamu watiifu baraka za milele. (Mathayo 4:23) Ujumbe huo ulikuwa wa nani? Yesu mwenyewe alisema hivi: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma,” Yehova. (Yohana 7:16) Yesu alijua kwamba Baba yake anataka wanadamu wasikie habari njema ya Ufalme. Katika Sura ya 8, tutajifunza mengi zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu na mambo ambayo utatimiza.

17. Yesu alifundisha wapi, na kwa nini alijitahidi sana kuwafundisha wengine?

17 Yesu alifundisha wapi? Kila mahali penye watu—mashambani, majijini, vijijini, sokoni, na nyumbani kwao. Yesu hakungoja watu wamjie. Alienda walipokuwa. (Marko 6:56; Luka 19:5, 6) Kwa nini Yesu alijitahidi sana na kutumia wakati mwingi kuhubiri na kufundisha? Kwa sababu Mungu alitaka afanye hivyo. Sikuzote Yesu alifanya mapenzi ya Baba yake. (Yohana 8:28, 29) Hata hivyo, kulikuwa na sababu nyingine iliyomfanya ahubiri. Aliusikitikia umati wa watu waliokuja kumwona. (Mathayo 9:35, 36) Walikuwa wamepuuzwa na viongozi wao wa kidini ambao walipaswa kuwafundisha kweli kumhusu Mungu na makusudi yake. Yesu alijua kwamba watu hao walitamani sana kusikia ujumbe wa Ufalme.

18. Ni sifa zipi za Yesu zinazokuvutia sana?

18 Yesu alikuwa mchangamfu na mwenye hisia nyingi. Kwa hiyo watu walimwona kuwa mtu mwenye fadhili na urafiki. Hata watoto walifurahia ushirika wake. (Marko 10:13-16) Yesu hakuwa na ubaguzi. Alichukia ufisadi na ukosefu wa haki. (Mathayo 21:12, 13) Aliwaheshimu wanawake ingawa wakati huo walikuwa wakidharauliwa na kunyimwa haki zao. (Yohana 4:9, 27) Yesu alikuwa mnyenyekevu kikweli. Pindi moja, aliosha miguu ya mitume wake, kazi ambayo kwa kawaida ilifanywa na mtumishi wa hali ya chini.

Yesu alihubiri kila mahali penye watu

19. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Yesu alihangaikia mahitaji ya wengine?

19 Yesu alihangaikia mahitaji ya wengine. Hilo lilionekana wazi alipoongozwa na nguvu za roho ya Mungu kufanya miujiza ya uponyaji. (Mathayo 14:14) Kwa mfano, mtu fulani aliyekuwa na ukoma alimjia Yesu na kusema: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu alihisi kana kwamba yeye mwenyewe ndiye aliyekuwa akiumia na kuteseka. Alimsikitikia, akaunyoosha mkono wake, akamgusa, na kusema: “Ninataka. Takasika.” Na mtu huyo aliyekuwa mgonjwa akapona. (Marko 1:40-42) Je, unaweza kuwazia jinsi mtu huyo alivyohisi?

MWAMINIFU MPAKA MWISHO

20, 21. Yesu aliwekaje mfano bora wa utii mshikamanifu kwa Mungu mpaka kifo?

20 Yesu aliweka mfano bora wa utii mshikamanifu kwa Mungu. Aliendelea kuwa mwaminifu kwa Baba yake wa mbinguni chini ya hali zote na licha ya upinzani na magumu mbalimbali. Yesu alifaulu kupinga kwa uthabiti vishawishi vya Shetani. (Mathayo 4:1-11) Wakati mmoja, baadhi ya watu wa ukoo wa Yesu mwenyewe hawakumwamini, hata walisema kwamba alikuwa “amerukwa na akili.” (Marko 3:21) Hata hivyo, Yesu hakuwaruhusu wamkengeushe; bali aliendelea kufanya kazi ya Mungu. Ijapokuwa alitukanwa na kutendewa vibaya, Yesu alijizuia, hakujaribu kuwadhuru wapinzani wake.—1 Petro 2:21-23.

21 Yesu aliendelea kuwa mwaminifu mpaka alipokufa kifo cha kikatili na uchungu mikononi mwa adui zake. (Wafilipi 2:8) Fikiria mambo aliyovumilia usiku wa mwisho wa maisha yake akiwa mwanadamu. Alikamatwa, akashtakiwa na mashahidi wa uwongo, akahukumiwa na mahakimu wafisadi, akachekwa na umati, na kuteswa na askari. Akiwa ametundikwa kwenye mti wa mateso, alivuta pumzi ya mwisho akipaaza sauti: “Imetimizwa!” (Yohana 19:30) Hata hivyo, siku tatu baada ya Yesu kufa, Baba yake wa mbinguni alimfufua na kumfanya hai katika roho. (1 Petro 3:18) Majuma machache baadaye, alirudi mbinguni. Akiwa huko, ‘aliketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu’ na kungoja apokee mamlaka ya kifalme.—Waebrania 10:12, 13.

22. Yesu alitimiza nini kwa kuendelea kuwa mwaminifu mpaka kifo?

22 Yesu alitimiza nini kwa kuendelea kuwa mwaminifu mpaka kifo? Kifo cha Yesu kinatuwezesha kupata uzima wa milele katika dunia itakayokuwa paradiso kama vile Yehova alivyokusudia mwanzoni. Sura inayofuata itazungumzia jinsi kifo cha Yesu kinavyotuwezesha kupata uzima.

^ fu. 7 Unaweza kupata maelezo kuhusu unabii wa Danieli uliotimia kuhusiana na Yesu katika nyongeza “Jinsi Unabii wa Danieli Ulivyotabiri Kutokea kwa Masihil.”

^ fu. 11 Yehova anaitwa Baba kwa sababu yeye ndiye Muumba. (Isaya 64:8) Yesu anaitwa Mwana wa Mungu kwa sababu aliumbwa na Mungu. Vivyo hivyo, malaika wengine na Adamu wanaitwa wana wa Mungu.—Ayubu 1:6; Luka 3:38.

^ fu. 12 Unaweza kupata uthibitisho zaidi unaoonyesha kwamba Mwana mzaliwa wa kwanza halingani na Mungu katika nyongeza “Ukweli Kuhusu Baba, Mwana, na Roho Takatifu.”