Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 2

Mungu Ni Nani?

Mungu Ni Nani?

1. Kwa nini tumwabudu Mungu?

Mungu wa kweli ndiye Muumba wa vitu vyote. Hana mwanzo wala mwisho. (Zaburi 90:2) Yeye ndiye Chanzo cha habari njema inayopatikana katika Biblia. (1 Timotheo 1:11) Kwa kuwa Mungu ndiye aliyetuumba, tunapaswa kumwabudu yeye peke yake.​—Soma Ufunuo 4:11.

2. Mungu yukoje?

Hakuna mwanadamu ambaye amewahi kumwona Mungu kwa kuwa yeye ni Roho. Mungu hana mwili wa nyama na damu kama viumbe wanaoishi hapa duniani. (Yohana 1:18; 4:24) Hata hivyo, tunaweza kutambua utu wa Mungu kupitia vitu alivyoumba. Kwa mfano, matunda na maua ya aina mbalimbali yanafunua upendo na hekima ya Mungu. Ukubwa wa ulimwengu unafunua nguvu za Mungu.​—Soma Waroma 1:20.

Tunaweza kujifunza mengi zaidi kuhusu utu wa Mungu kwa kuisoma Biblia. Kwa mfano, Biblia inatueleza mambo ambayo Mungu anapenda na anayochukia, na jinsi anavyoshughulika na watu katika hali mbalimbali.​—Soma Zaburi 103:7-10.

3. Je, Mungu ana jina?

Yesu alisema: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Ingawa Mungu ana majina mengi ya cheo, ana jina moja tu. Linatamkwa kwa njia tofauti katika kila lugha. Katika Kiswahili kwa kawaida jina hilo linatamkwa “Yehova.” Lakini watu fulani wanalitamka “Yahweh.”​—Soma Zaburi 83:18.

Jina la Mungu limeondolewa katika Biblia nyingi na mahali pake kuchukuliwa na majina ya cheo Bwana au Mungu. Lakini Biblia ilipoandikwa, jina la Mungu lilipatikana mara 7,000 hivi. Yesu alifanya jina la Mungu lijulikane alipokuwa akiwafundisha watu kuhusu Mungu.​—Soma Yohana 17:26.

Tazama video Je, Mungu Ana Jina?

4. Je, Yehova anatujali?

Kama baba huyu mwenye upendo, Mungu anatenda kwa njia itakayotuletea manufaa ya kudumu

Kwa kuwa tunateseka sana leo, je, hilo linamaanisha kwamba Yehova ni Mungu asiyetujali? Watu fulani wanadai kuwa Mungu anatuacha tuteseke ili atujaribu. Lakini hilo si kweli.​—Soma Yakobo 1:13.

Mungu amempa mwanadamu uhuru wa kufanya maamuzi. Tunathamini sana uhuru tulio nao wa kuchagua kumtumikia Mungu. (Yoshua 24:15) Hata hivyo, watu wengi wamechagua kuwafanyia wengine mambo mabaya, ndiyo maana kuna mateso mengi. Yehova anaumia anapoona ukosefu huo wa haki.​—Soma Mwanzo 6:5, 6.

Yehova ni Mungu anayetujali. Anataka tufurahie maisha. Hivi karibuni, ataondoa mateso na wale wanaoyasababisha. Kwa sasa, ana sababu nzuri ya kuwaruhusu wanadamu wateseke kwa muda fulani. Tutajifunza kuhusu sababu hiyo katika Somo la 8.​—Soma 2 Petro 2:9; 3:7, 13.

5. Tunaweza jinsi gani kumkaribia Mungu?

Yehova anatualika tumkaribie kupitia sala. Anapendezwa nasi tukiwa mtu mmojammoja. (Zaburi 65:2; 145:18) Yuko tayari kutusamehe. Anatambua jitihada zetu za kumpendeza, hata ingawa nyakati nyingine tunakosea. Kwa hiyo, licha ya kutokamilika kwetu, kwa kweli tunaweza kufurahia urafiki wa karibu pamoja na Mungu.​—Soma Zaburi 103:12-14; Yakobo 4:8.

Kwa kuwa Yehova ametupa uhai, tunapaswa kumpenda kuliko tunavyompenda mtu mwingine yeyote. (Marko 12:30) Kadiri unavyoonyesha upendo wako kwa Mungu kwa kujifunza mengi kumhusu na kufanya yale anayotaka, ndivyo utakavyomkaribia zaidi.​—Soma 1 Timotheo 2:4; 1 Yohana 5:3.