Hamia kwenye habari

Walijitoa kwa Hiari—Nchini Guyana

Walijitoa kwa Hiari—Nchini Guyana

“Maneno hayatoshi kuelezea shangwe unayopata unapotumikia katika eneo lenye uhitaji!” Hivyo ndivyo alivyosema Joshua, anayeishi Marekani ambaye alitumikia huko Guyana. Hivyo ndivyo wanavyohisi pia Mashahidi wengi ambao wametumikia katika nchi hiyo yenye matokeo makubwa huko Amerika Kusini. a Tunaweza kujifunza mambo gani kutokana na wajitoleaji hao? Masomo hayo yanawezaje kukusaidia unapojitayarisha kutumikia katika nchi ya kigeni?

Walichochewa na Nini?

Linel

Kabla ya kuhamia Guyana, ndugu anayeitwa Linel alihubiri katika eneo lisilohubiriwa kwa ukawaida nchini kwao, Marekani. “Tukiwa kikundi cha wahubiri 20 tulipewa mgawo wa kuhubiri eneo la mashambani huko West Virginia,” anasema. “Maisha yangu yalibadilika kutokana na mambo niliyojionea tulipohubiri na ushirika tuliofurahia majuma mawili tuliyokuwa huko! Niliazimia hata zaidi kumtumikia Yehova kikamili zaidi.”

Erica na Garth

Gath na mke wake Erica walianzia kufikiria kwa uzito kuhusu kutumikia katika nchi ya kigeni, na wakachagua kwenda Guyana. Kwa nini? “Mimi na mume wangu tuliwafahamu wenzi wa ndoa waliokuwa wamehamia huko,” anasema Erica. “Tulichochewa kuhamia huko kutokana na shauku yao na upendo wao kuelekea mambo waliyokuwa wakifanya.” Erica na Garth walitumikia kwa miaka mitatu katika “mgawo waliouthamini” sana. Garth anasema: “Tulionja utumishi wa kigeni na kuona kwamba ulikuwa mzuri sana.” Baadaye, yeye na mke wake walihudhuria Shule ya Gileadi na sasa wanatumikia Bolivia.

Wale wanaotumikia katika nchi ya kigeni mara nyingi hufurahia mazungumzo mazuri kuhusu Biblia

Walijitayarishaje?

Kanuni za Biblia zinatusaidia kuishi maisha rahisi. (Waebrania 13:5) Vilevile, tunatiwa moyo kuhesabu gharama kabla ya kufanya maamuzi makubwa maishani. (Luka 14:26-33) Hilo linatia ndani maamuzi yanayohusu kuhamia nchi ya kigeni! Garth anasema: “Kabla ya kwenda Guyana, mimi na Erica tulihitaji kurahisisha maisha yetu. Hilo lilitia ndani kuuza biashara yetu, nyumba yetu, na vitu vyote ambavyo havikuwa vya lazima katika nyumba yetu. Hilo lilichukua miaka kadhaa. Wakati huohuo, tulidumisha tamaa yetu ya kutumikia Guyana kwa kuendelea kukazia fikira mradi wetu na kutembelea nchi hiyo kila mwaka.”

Sinead na Paul

Jambo lingine la kuzingatia ni kipato. Baadhi ya wajitoleaji wanaweza kufanya kazi katika nchi ya kigeni ikiwa sheria ya nchi hiyo inawaruhusu. Baadhi yao hufanya kazi ambayo walikuwa wakifanya nyumbani kwao wakitumia kompyuta iliyounganishwa na Intaneti. Wengine huamua kurudi nchini kwao kwa vipindi vifupi ili kufanya kazi. Paul na mke wake Sinead walirudi nyumbani kwao Ireland mara moja kwa mwaka ili kufanya kazi. Hilo liliwasaidia kutumikia Guyana kwa miaka 18 yenye kufurahisha, kutia ndani miaka saba baada ya binti yao kuzaliwa.

Christopher na Lorissa

Andiko la Zaburi 37:5 linasema: “Mkabidhi Yehova njia yako; Mtegemee yeye, naye atatenda kwa niaba yako.” Christopher na Lorissa kutoka Marekani walisali kwa ukawaida kuhusu mradi wao wa kutumikia katika nchi ya kigeni. Pia, wakati wa ibada ya familia, walichunguza mambo ambayo wangefanya ili wafaulu kuhama, kwa kuorodhesha faida na hasara. Kwa sababu lugha ilikuwa jambo kuu kwao, walichagua Guyana ambako Kiingereza ndiyo lugha rasmi.

Kisha wakatenda kulingana na kanuni ya Methali 15:22: “Mipango huvunjika watu wasiposhauriana, lakini mambo hufanikiwa kupitia washauri wengi.” Waliandikia barua ofisi ya tawi inayosimamia kazi nchini Guyana, b na kueleza kipindi watakachopatikana na habari zao za kibinafsi. Wakati uleule waliulizia kuhusu huduma za afya, hali ya hewa, na utamaduni wa nchi hiyo. Ofisi ya tawi ilijibu maswali yao na kuwaunganisha na baraza la wazee katika eneo ambalo wangetumikia.

Linel, aliyetajwa awali, sasa ni mwangalizi anayesafiri huko Guyana. Kabla ya kuhamia huko, yeye pia alitumia kanuni ya Methali 15:22. Anasema: “Mbali na kuweka akiba kwa ajili ya safari hiyo, nilizungumza na wengine ambao walikuwa wametumikia katika nchi ya kigeni. Nilizungumza na familia yangu kuhusu jambo hilo, wazee wa kutaniko, na mwangalizi wa mzunguko. Na nikasoma habari nyingi katika machapisho yetu kuhusu kutumikia katika eneo lenye uhitaji.

Joseph na Christina

Wengi wanaotaka kutumikia katika nchi ya kigeni, kwa hekima huamua kutembelea nchi hiyo kwanza. Joseph na mke wake Christina wanasema: “Mara ya kwanza tulipoenda Guyana tulikaa huko kwa miezi mitatu. Muda huo ulitutosha kuona hali ilivyokuwa. Kisha tukarudi nyumbani, tukakamilisha mipango yetu, na kuhama.”

Waliwezaje Kufanya Mabadiliko?

Joshua

Ili wafanikiwe kumtumikia Mungu katika nchi ya kigeni, wajitoleaji wanahitaji kuwa na roho ya kujidhabihu na kuwa tayari kufanya mabadiliko kulingana na hali na tamaduni za nchi hiyo. Kwa mfano, wale wanaotoka maeneo yenye baridi na kuhamia maeneo yenye joto hutambua kwamba maeneo waliyohamia yana wadudu wa kila aina. “Sikuzoea kuona wadudu wengi hivyo,” anasema Joshua, aliyenukuliwa awali. “Na wadudu nchini Guyana ni wakubwa! Lakini baada ya muda nikawazoea. Vilevile niligundua kwamba unaweza kupunguza idadi ya wadudu kwa kudumisha usafi nyumbani. Hilo linatia ndani kusafisha vyombo, kutupa takataka, na kusafisha nyumba kwa ukawaida.”

Kufanya mabadiliko katika nchi ya kigeni kunatia ndani pia kuanza kula vyakula ambavyo hukuzoea na kujifunza jinsi ya kuvitayarisha. “Mimi na mwenzangu tuliwaomba ndugu na dada watufundishe jinsi ya kupika chakula cha eneo hilo,” anakumbuka Joshua. “Baada ya kujifunza kupika chakula fulani, tuliwaalika baadhi ya ndugu kutoka kutanikoni ili tule pamoja. Hiyo ilikuwa njia nzuri pia ya kuwafahamu akina ndugu na kuanzisha urafiki.”

Paul na Kathleen

Kuhusu utamaduni, Paul na Kathleen wanasema hivi: “Hatukuwa tumezoea tabia na mavazi yanayokubalika katika sehemu zenye joto. Basi tulihitaji kuwa wanyenyekevu na kufanya mabadiliko bila kuvunja kanuni za Biblia. Kujifunza utamaduni wa eneo hilo kulifanya tuwe karibu zaidi na kutaniko na kulifanya tupate matokeo katika huduma.”

Walifaidikaje?

Joseph na Christina wanazungumza kwa niaba ya wengi wanaposema: “Baraka ni nyingi kuliko matatizo na changamoto. Kuishi maisha mapya kulitusaidia kubadili maoni yetu kuhusu mambo tunayotanguliza. Vitu tulivyoviona kuwa vya thamani sana maishani havikuwa muhimu tena. Kila jambo tulilojionea lilituchochea tuendelee kufanya yote tuwezayo katika utumishi wa Yehova. Tuliridhika na kutosheka sana.”

Erica, aliyenukuliwa awali alisema: “Kutumikia eneo lenye uhitaji kulitusaidia mimi na mume wangu tujifunze kikamili kile kinachomaanishwa na kumtegemea Yehova. Tumeona mkono wake ukitusaidia katika njia ambazo hatukujionea mwanzoni. Na mambo tuliyojionea pamoja, yaliimarisha uhusiano wetu tukiwa mume na mke.”

a Historia ya kazi ya kuhubiri nchini Guyana inapatikana katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2005.

b Ofisi ya tawi ya Trinidad na Tobago inasimamia kazi nchini humo.