Hamia kwenye habari

Kampeni Yenye Mafanikio Kwenye Eneo la Lapland

Kampeni Yenye Mafanikio Kwenye Eneo la Lapland

Katika eneo kubwa linaloenea kutoka nchi ya Finland, Norway, na Sweden kuna watu wenye utamaduni, desturi na lugha yao wenyewe wanaoitwa Wasami. Hivi karibuni Mashahidi wa Yehova walifanya kampeni mara mbili ya kuwaeleza Wasami ujumbe wa Biblia.

Kwanza, katika majira ya kupukutika kwa majani ya mwaka wa 2015, Mashahidi walianza kutayarisha machapisho ya Biblia na video katika lugha ya Kisami. * Pili, wakati wa kampeni mbili za pekee, katika mwaka wa 2016 na pia 2017, Mashahidi wa Yehova walisafiri hadi eneo la Lapland​—eneo la mbali ambako makundi ya mbawala hutembea-tembea​—ili kuwapelekea Wasami habari zilizotafsiriwa katika lugha yao.

“Kazi yenye thamani katika jamii”

Katika kampeni ya pekee iliyofanywa Mei 2017, Mashahidi zaidi ya 200 kutoka Finland, Norway, na Sweden walijitolea kwenda kwenye vijiji vingi vidogo vilivyotapakaa maelfu ya kilomita katika eneo la Lapland. Mashahidi fulani walijiandaa kwa kujifunza sentensi kadhaa katika Kisaami, na hilo liliwavutia wenyeji. Denis ambaye alijitolea katika eneo la Karigasniemi, anasimulia hivi: “Wenyeji walithamini jitihada zetu za kuzungumza lugha yao na walitambua kwamba tunapendezwa nao kibinafsi.”

Kwa sababu wanathamini uumbaji na wanyama-pori, Wasaami wanathamini sana ahadi ya Biblia kuhusu paradiso duniani. (Zaburi 37:11) Kwa mfano, mwanamke Msaami alipoanza kujifunza Biblia akitumia broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu! na kujifunza mambo ambayo Mungu atawatimizia wanadamu, aliuliza kwa mshangao kwa nini kasisi wake hakuwa amemwambia kuhusu paradiso duniani.

Wengi walishukuru sana kwa Mashahidi kuwatembelea. Mwenye duka mmoja aliwapongeza Mashahidi wawili aliokuwa amewatazama kwa muda. Aliwaambia kwamba walikuwa wakifanya “kazi muhimu na yenye thamani katika jamii” na akawaalika waingie dukani na kuchukua chakula chochote walichohitaji. Mwenye duka huyo alisisitiza kwamba atashughulikia gharama zote.

Wakati wa kampeni hiyo, Wasaami walitazama video 180 hivi na kupokea machapisho zaidi ya 500. Mara nyingi, waliomba machapisho yote yaliyopatikana katika lugha yao. Isitoshe, watu 14 walianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.

‘Kazi iliyofanywa na wataalamu’

Wasaami kadhaa waliosoma machapisho ya Mashahidi wa Yehova walithamini ubora wa hali ya juu wa tafsiri zetu. Nilla Tapiola, mwalimu na mshiriki Baraza la Kuu la Bunge la Wasaami, alisema hivi: “Machapisho yenu yametafsiriwa vizuri sana.” Alieleza kwamba machapisho hayo “ni rahisi kuyasoma na yamefuata sheria za lugha.” Mwanamume Msaami anayeishi katika sehemu ya kaskazini kabisa ya Finland alisema hivi: “Ni wazi kwamba machapisho hayo yanathibitisha kazi hiyo ilifanywa na wataalamu.”

Huko Karigasniemi, kwenye mpaka kati ya Finland na Norway, Mashahidi walizungumzia na mwalimu Msaami somo la kwanza la broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu! Akiwa amevutiwa sana na ubora wa tafsiri hiyo, mwalimu huyo aliwaomba Mashahidi ruhusa ya kutumia broshua hiyo shuleni kufundisha lugha ya Saami.

Tayari video kadhaa pamoja na trakti, na broshua moja zimetafsiriwa katika lugha ya Saami. Tovuti ya jw.org imepatikana katika lugha ya Saami tangu Februari 29, 2016. Kila mwezi, wazungumzaji wa lugha ya Saami wanatembelea tovuti hiyo mara zaidi ya 400 na kupakua machapisho, rekodi za kusikiliza, na video.

Wasaami na wale waliojitolea kuwatembelea wanahisi wameimarishwa na kampeni hiyo. Henrick na Hilja-Maria, ambao alisafiri hadi Utsjoki walieleza kwamba wenyeji wangeweza kusema kwamba “wameona Biblia inaweza kuwanufaisha Wasaami.” Lauri na Inga, ambao pia walijitolea huko Utsjoki, anasema hivi: “Kampeni hii ilitukumbusha kwamba Mungu hana ubaguzi. Tunafurahi kuwaonyesha wakaaji wa maeneo haya ya mbali upendo wake.”

^ fu. 3 Kuna lugha kadhaa za Saami (pia zinajulikana kama Sami). Encyclopædia Britannica inasema kwamba “lugha kuu, Kisami cha Kaskazini, kinazungumzwa na asilimia 66 hivi ya Wasami.” Mashahidi wa Yehova wanatafsiri machapisho yao katika Kisaami cha Kaskazini. Ili kurahisisha mambo, makala hii inatumia neno “Saami” kurejelea lugha inayozungumzwa na watu wengi.