Hamia kwenye habari

Kuhubiri Ujumbe wa Biblia Katika Maeneo ya Kaskazini Zaidi ya Ulaya na Amerika

Kuhubiri Ujumbe wa Biblia Katika Maeneo ya Kaskazini Zaidi ya Ulaya na Amerika

Mwaka wa 2014, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova liliandaa programu mpya ya kuhubiri ujumbe wa Biblia katika maeneo ya mbali zaidi ya Kaskazini mwa Ulaya na Amerika Kaskazini. (Matendo 1:8) Mwanzoni, programu hiyo ilikazia fikira jamii fulani za Alaska (Marekani), Lapland (Finland), Nunavut na Maeneo ya Kaskazini Magharibi ya Kanada.

Kwa miaka mingi Mashahidi wa Yehova wametembelea maeneo hayo ya mbali ili kuhubiri. Hata hivyo, Mashahidi hao walikaa kwa muda mfupi na walisambaza tu machapisho ya Biblia.

Chini ya programu hiyo mpya, ofisi za tawi zinazosimamia kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova katika maeneo ya mbali ya Kaskazini ziliwaomba wahudumu wa wakati wote (mapainia) watumikie katika maeneo yaliyoteuliwa kwa angalau miezi mitatu. Ikiwa wangepata watu kadhaa katika jamii hizo wanaotaka kujifunza Biblia, wahudumu hao wangekaa hapo kwa muda mrefu zaidi na hata kufanya mikutano ya watu wote.

Maeneo hayo ya Kaskazini yana changamoto za pekee. Mapainia wawili walipata mgawo wa kwenda Barrow, Alaska, mmoja alitoka kusini mwa California na mwingine alitoka Georgia, Marekani. Katika majira yao ya kwanza ya baridi kali huko Barrow, kiwango cha baridi kilifikia Selsiasi 38 chini ya sufuri! Hata hivyo, miezi michache tu baada ya kuwasili, walikuwa wametembelea asilimia 95 hivi ya nyumba katika jiji hilo na kuanzisha mafunzo manne ya Biblia. Kwa mfano, walianzisha funzo na kijana anayeitwa John. Yeye na mchumba wake wanajifunza kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? John huwaeleza marafiki na wafanyakazi wenzake mambo anayojifunza. Isitoshe, yeye husoma andiko la siku katika kitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku kupitia programu ya JW Library katika simu yake.

Hakuna barabara kwenda Rankin Inlet, kijiji kidogo kilicho katika eneo la Kanada la Nunavut. Hivyo mapainia wawili walitumia ndege kufika huko na wakaanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia. Baada ya mwanamume mmoja kutazama video yenye kichwa Ni Nini Hutendeka Katika Jumba la Ufalme? aliuliza Jumba la Ufalme litajengwa lini katika eneo hilo. Alisema hivi: “Ikiwa nitakuwa hapa mtakapolijenga, nitahudhuria mikutano yenu.”

Mapainia waliopewa mgawo wa kwenda Savukoski, Finland ambapo mbawala wanazidi idadi ya watu kwa mara kumi, waliripoti hivi: “Kuna baridi kali na theluji nyingi sana.” Hata hivyo, wanasema kuwa walifika wakati mwafaka. Kwa nini? Walieleza hivi: “Tumefaulu kuhubiri maeneo haya kikamili. Barabara zinazoelekea kwenye vijiji na maeneo ya mbali zinatunzwa vizuri. Baridi kali imesababisha watu kutumia wakati mwingi zaidi nyumbani.”

Jitihada yetu ya kuhubiri kweli za Biblia katika maeneo ya mbali zaidi katika jamii hizo za Kaskazini zimetambuliwa. Baada ya mapainia wawili kumtembelea meya wa jiji moja la Alaska, meya huyo aliandika ujumbe mzuri katika mtandao mmoja wa kijamii, akieleza kuhusu mambo aliyozungumzia na mapainia hao na akaweka picha ya trakti Ufalme wa Mungu Ni Nini? katika mtandao huo.

Katika eneo la Haines, Alaska, ambapo mapainia wawili waliwakaribisha angalau watu wanane kwenye mikutano iliyofanywa katika maktaba ya umma, gazeti liliripoti kuwa wanaume wawili kutoka Texas na North Carolina waliwasili kuwafundisha watu Biblia nyumbani mwao. Tangazo hilo lilimalizia kwa kusema hivi: “Tembelea jw.org ili ujifunze zaidi.”