Ona video zinazopatikana

Biblia Inasema Nini Juu ya Kuchunga Wazazi Wenye Kuzeeka?

Biblia Inasema Nini Juu ya Kuchunga Wazazi Wenye Kuzeeka?

Jibu la Biblia

 Watoto wenye walishakomaa wako na daraka la maana la kuhangaikia wazazi wao wenye kuzeeka. Biblia inasema kama ni lazima watoto “wafundishwe kwanza kuwatendea kwa mapendo watu wa nyumba yao wenyewe na kuwarudishia wazazi wao waliyopokea kwao . . . , maana hiyo inamupendeza Mungu.” (1 Timoteo 5:4, Verbum Bible) Wakati watoto wanahangaikia wazazi wao wenye kuzeeka, wanaonyesha pia kama wanatii amri ya Biblia ya kuheshimia wazazi wao.​—Waefeso 6:2, 3.

 Mu Biblia hamuna liste ya mambo yenye watoto wanapaswa kufanya ili kuhangaikia wazazi wao wenye kuzeeka. Lakini, muko mifano ya wanaume na wanamuke wenye walikuwa na imani wenye walihangaikia wazazi wao. Muko pia mashauri yenye inaweza kusaidia wale wenye kuchunga wazazi wenye kuzeeka.

 Wakati wa zamani, namna gani watu fulani walihangaikia wazazi wao wenye kuzeeka?

 Walifanya vile mu njia mbalimbali, kulingana na hali.

  •   Yosefu aliishi mbali na baba yake mwenye kuzeeka, Yakobo. Wakati iliwezekana, Yosefu alifanya mipango ili baba yake ahamie karibu naye. Kisha alimupatia fasi ya kuishi, alikuwa anamupatia chakula, na alimulinda.​—Mwanzo 45:9-11; 47:11, 12.

  •   Rutu alihamia mu inchi ya mama-mukwe wake na alitumika sana ili kumuhangaikia.​—Rutu 1:16; 2:2, 17, 18, 23.

  •   Yesu alichagua mutu ili achunge mama yake, mwenye inaonekana ile wakati alikuwa mujane. Alifanya vile wakati mufupi mbele akufe.​—Yohana 19:26, 27. *

 Mu Biblia muko mashauri gani yenye inaweza kusaidia wale wenye kuchunga wazazi wenye kuzeeka?

 Haiko mwepesi kuchunga wazazi wenye kuzeeka. Wakati fulani, mutu anaweza kuchoka na kuvunjika moyo. Lakini, mu Biblia muko kanuni zenye zinaweza kusaidia wale wenye kuchunga wazazi wenye kuzeeka.

  •   Heshimia wazazi wako.

     Mambo yenye Biblia inasema: “Heshimia baba yako na mama yako.”​—Kutoka 20:12.

     Namna gani unaweza kutumia ile kanuni? Onyesha kama unaheshimia wazazi wako kwa kuwaachia uhuru kadiri inawezekana. Kadiri inawezekana, uwaache wajiamulie namna wanapenda kuhangaikiwa. Hata vile, uonyeshe kama unawaheshimia kwa kufanya mambo yenye unawaza inaweza kuwasaidia.

  •   Uwaelewe na uwasamehe.

     Mambo yenye Biblia inasema: “Ufahamu wa mutu hakika unatuliza kasirani yake, na ni uzuri kwake kuachilia kosa.”​—Mezali 19:11.

     Namna gani unaweza kutumia ile kanuni? Kama muzazi mwenye kuzeeka anasema jambo lenye haufurahie ao inaonekana kuwa hana shukrani, ujiulize hivi: ‘Kama ningekuwa mu hali sawa yake, ningejisikia namna gani?’ Kujikaza kumuelewa na kumusamehe kutasaidia usifanye hali ikuwe mubaya zaidi.

  •   Uzungumuze na wengine.

     Mambo yenye Biblia inasema: “Mipango inashindikana wakati hakuna mazungumuzo, lakini mambo yanatimizwa kupitia washauri wengi.”​—Mezali 15:22.

     Namna gani unaweza kutumia ile kanuni? Utafute habari zenye kuzungumuzia namna unaweza kushugulikia matatizo ya afya yenye pengine wazazi wako wanapambana nayo. Tafuta kujua ikiwa mu eneo lenu muko mipango ya kusaidia watu wenye kuzeeka. Zungumuza na wengine wenye wamehangaikia wazazi wao wenye kuzeeka. Ufanye mukutano pamoja na watu wengine wa familia ili kuzungumuzia mahitaji ya wazazi wenu, namna ya kuwahangaikia, na mambo yenye kila mutu anaweza kufanya ili kuwasaidia.

    Mufikirie kufanya mukutano wa jamaa ili muzungumuzie namna mutachunga wazazi wenu wenye wamezeeka

  •   Ukuwe na kiasi.

     Mambo yenye Biblia inasema: “Lakini wenye kiasi wako na hekima.”​—Mezali 11:2.

     Namna gani unaweza kutumia ile kanuni? Ujue kama uko na mipaka. Kwa mufano, hakuna mutu mwenye anakuwaka na wakati na nguvu ya kufanya mambo yote yenye anapenda. Kwa hiyo, unaweza kushindwa kufanya mambo yote yenye ungependa kufanyia wazazi wako. Kama unaona inakuwa nguvu kuhangaikia wazazi wako wenye kuzeeka, omba watu wengine wa familia wakusaidie ao watu wenye wamezoezwa ili kuchunga watu wenye kuzeeka.

  •   Usijiachilie.

     Mambo yenye Biblia inasema: “Hakuna mutu mwenye anachukia mwili wake; lakini anaukulisha na kuutunza kwa upendo.”​—Waefeso 5:29.

     Namna gani unaweza kutumia ile kanuni? Hata kama uko na daraka la kuhangaikia mahitaji ya wazazi wako, uko pia na daraka la kujihangaikia na kuhangaikia watu familia yako kama ulishaoa ao kuolewa. Unapaswa kula muzuri. Ujikaze kuwa na wakati wa kutosha wa kulala na kupumuzika. (Muhubiri 4:6) Na wakati inawezekana, uende kujifurahisha kidogo. Kama unafanya vile, utakuwa na furaha, amani ya akili, na afya ya muzuri. Na kwa hiyo, utaweza kuhangaikia wazazi wako.

 Je, Biblia inasema kama wazazi wenye kuzeeka wanapaswa kuchungiwa tu ku nyumba?

 Biblia haitie sheria kama watoto wanapaswa tu kuchungia wazazi wao ku nyumba. Familia fulani zinaamua kuchungia wazazi wao ku nyumba kadiri inawezekana. Lakini wakati fulani wanaweza kuona kama ni muzuri zaidi wawapeleke ku nyumba za kuchungia watu wenye kuzeeka. Watu wa familia wanaweza kukutana ili kuamua ni njia gani yenye inafaa zaidi.​—Wagalatia 6:4, 5.

^ Kuhusu ile habari, kitabu kimoja chenye kufasiria Biblia kinasema hivi: “Inaonekana kulikuwa kumepita muda murefu tangu Yosefu [bwana ya Maria] akufe, na kwa hiyo, Yesu njo alikuwa anahangaikia mama yake. Sasa, juu Yesu alikuwa karibu kufa, nani njo angehangaikia mama yake? . . . Hapa, Kristo anafundisha watoto kuhangaikia wazazi wao wenye wamezeeka.”​—The NIV Matthew Henry Commentary in One Volume, ukurasa wa 428-429.