Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA

Namna ya Kushinda—Mahangaiko ya Akili

Namna ya Kushinda—Mahangaiko ya Akili

“Nilijisikia kama panya anayekimbia juu ya kitu kinachozunguka na chenye hakiendi mahali popote. Kwa ukawaida nilifanya kazi saa 16 kwa siku na mara nyingi sikupumuzika mwisho wa juma. Nilijisikia kuwa mwenye kukasirika kwa sababu kila siku nilimuona mutoto wangu mudogo mwanamuke akiwa tu mwenye kulala. Mahangaiko ya akili yalinifanya niwe mugonjwa.”—Kari, anayeishi Finlande.

MAMBO Kari alipitia ni ya kawaida katika maisha. Kulingana na shirika la kutunza magonjwa ya akili katika inchi ya Uingereza, mufanyakazi 1 kati ya wafanyakazi 5 Waingereza walisema kwamba mahangaiko ya akili yalikuwa yamewafanya wawe wagonjwa wakati wa kazi yao, na mikazo ya maisha yenye hawakuweza kushinda yalikuwa yamefanya mufanyakazi 1 kati ya wafanyakazi 4 alie wakati wa kazi. Watu walioandikiwa madawa ya kupunguza mahangaiko ya akili waliongezeka sana hivi karibuni wakati hali ya feza iliharibika ulimwenguni.

Mambo yanayokuletea mahangaiko ya akili

  • Kukosa usalama—wa kifeza ao katika mambo mengine

  • Kuwa na mambo mengi ya kufanya

  • Kukosa kuelewana na wengine

  • Kupatwa na mambo yenye kuogopesha

Mahangaiko ya akili yanakufanya ujisikie namna gani?

  • Hali mubaya ya afya

  • Kuchoka moyoni

  • Matatizo ya kukosa usingizi

  • Kushuka moyo

  • Kuharibika kwa mahusiano pamoja na wengine

Mahangaiko ya akili yanachochea mufumo wenye kushangaza katika mwili wetu, yanalinganishwa na kituo cha kiganga kinachojibu watu wanaoita kwenye telefone ili wapate musaada wa haraka sana. Homoni zinatokezwa ili kuongeza namna yako ya kupumua, pigo la moyo, na mwendo wa damu katika mwili. Tena, mabaki ya chembe za damu pamoja na sukari vinatiririka katika damu yako. Utendaji huo mbalimbali wenye kufuatana unakutayarisha kupambana na hali inayotokeza na kuchochea mahangaiko ya akili. Hali hiyo inayotokeza mahangaiko ya akili inapopita, mwili wako unaweza kurudilia tena hali yake ya kawaida. Lakini wakati hali hiyo inaendelea, inaweza kukuacha katika wasiwasi yenye kuendelea ao mukazo, kama vile injini (moteur) inayoendelea kufanya kazi. Kwa hiyo, kujua namna ya kupambana na mahangaiko ya akili ni jambo la maana kwa mwili wako na kunaweza kufanya hali yako ya akili iwe nzuri.

Kushinda Mahangaiko ya Akili

Mahangaiko ya akili yenyewe hayana hatari. Shirika la Amerika Linalojifunza Mambo ya Akili ya Mwanadamu, linasema hivi: “Mahangaiko ya akili yanafananishwa na sauti ya kamba ya gitaa: wakati inaregezwa, muziki pia unakuwa na sauti ya chini na ya polepole; lakini inapokazwa, muziki pia unakuwa na sauti ya juu na yenye kupanda kabisa. Kuwa na mahangaiko mengi ya akili kunaweza kutokeza kifo lakini kuwa na mahangaiko ya akili ya kadiri kunaweza kufanya maisha yetu yawe yenye kupendeza. Kwa kweli, jambo la lazima ni kujua namna ya kupambana na mahangaiko ya akili.”

Jambo lingine la kufikiria ni kwamba watu wanatofautiana katika tabia na hali yao ya afya. Kwa hiyo, jambo linalomuhangaisha mutu mumoja kiakili pengine lisimuhangaishe mutu mwengine. Kwa sababu hiyo, unaweza kuonekana kuwa unahangaishwa sana kiakili ikiwa kazi yako ya kawaida inakuletea mukazo na hivyo unashindwa kupumuzika ao kushugulikia hali zisizo za kawaida, lakini zinazoomba kutenda kwa haraka.

Watu wengine wanatumia pombe, dawa za kulewesha, ao tumbaku ili kuwasaidia “kupambana” na mahangaiko ya akili yenye kuendelea. Wengine wanaanza kula kwa namna isiyo ya kawaida, kutazama televisheni ao ordinatere kwa muda murefu, tabia hizo haziwasaidie kupunguza hali hiyo, lakini zinaweza tu kuiongeza. Kwa hiyo, namna gani tunaweza kupambana na mahangaiko ya akili kwa njia yenye kufaa?

Watu wengi wameweza kupambana na mahangaiko ya akili katika maisha yao kwa kufuata mashauri mazuri yaliyo katika Biblia. Hekima ya Biblia yenye imesaidia watu wengi kwa muda murefu inaweza kukusaidia pia? Fikiria ulizo hilo kwa kuchunguza sababu ine zinazoleta mahangaiko ya akili.

1 KUKOSA USALAMA

Hakuna mutu kati yetu aliye salama kabisa. Kama Biblia inavyosema, ‘wakati na tukio lisilotazamiwa linatupata [sisi] wote.’ (Mhubiri 9:11) Namna gani unaweza kupambana na hali ya kukosa usalama? Jaribu kufanya mambo haya:

  • Zungumuza na mutu wa familia ao rafiki unayemutumainia. Uchunguzi unaonyesha kwamba musaada kutoka kwa watu wanaotupenda unatulinda siku zote na mahangaiko ya akili. Kwa kweli, “rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

  • Usiendelee kuwazia tu mambo mabaya yanayoweza kutokea. Mawazo kama hayo yanatuchokesha moyoni. Na mambo unayoogopa labda hayatatokea! Ni kwa sababu hiyo Biblia inasema hivi: ‘Musihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.’—Mathayo 6:34.

  • Faidika na nguvu ya sala. Andiko la 1 Petro 5:7 linasema hivi: ‘Mutupe mahangaiko yenu yote juu [ya Mungu], kwa sababu yeye anawajali ninyi.’ Mungu anatuonyesha kuwa anatuhangaikia kwa kutupatia amani ya moyo na kwa kutuhakikishia kwamba ‘hatawatupa hata kidogo’ wale wanaotafuta kwelikweli kufarijiwa na kutegemezwa naye wakati wa magumu.—Waebrania 13:5; Wafilipi 4:6, 7.

2 KUWA NA MAMBO MENGI YA KUFANYA

Kuzoea kusafiri-safiri, kufanya kazi, kuenda kwenye masomo, kuhangaikia watoto ao wazazi waliozeeka, kunaweza kufanya mahangaiko ya akili yaongezeke zaidi. Zaidi ya hayo, labda isiwezekane kuacha kufanya mambo hayo. (1 Timotheo 5:8) Basi, unaweza kufanya nini ili kupambana na hali hiyo?

  • Jaribu kupata wakati wa kujifurahisha, na upumuzike vya kutosha. Biblia inasema hivi: ‘Konzi [mukono] moja ya pumuziko ni afazali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.’—Mhubiri 4:6.

  • Utangulize mambo ya maana zaidi, na uwe na maisha mepesi. (Wafilipi 1:10) Fanya namna yako ya kuishi iwe nyepesi, pengine kwa kupunguza garama za maisha ao wakati ambao unatumia kwenye kazi.—Luka 21:34, 35.

Kari, tuliyezungumuzia hapo mbele, alichunguza upya maisha yake. Aliandika hivi: “Nilitambua kwamba nilikuwa ninafuatilia maisha ya kutafuta faida zangu mwenyewe.” Aliuzisha biashara yake na akaanza kufanya kazi yenye ilimuruhusu apate wakati mwingi wa kuwa nyumbani. Anasema hivi: “Hali yetu ya maisha imeshuka kidogo, lakini mimi na bibi yangu hatuna tena mahangaiko ya akili, na tuna wakati mwingi wa kuwa pamoja na familia na marafiki. Siwezi kubadilisha utulivu wangu wa moyoni nilio nao sasa na kazi yoyote.”

3 KUKOSA KUELEWANA NA WENGINE

Kukosa kuelewana na wengine, zaidi sana nafasi ya kazi, kunaweza kuleta mahangaiko ya akili kabisa. Ikiwa una shida kama hiyo, kuna njia nyingi sana zinazoweza kukusaidia.

  • Wakati mutu fulani anakukasirisha, jaribu kukaa kimya. Usiongeze makaa kwenye moto. Andiko la Methali 15:1 linasema hivi: ‘Jibu, linapokuwa la upole, linageuza gazabu, lakini neno linaloumiza linafanya hasira ipande.’

  • Jaribu kumaliza ugomvi ulio kati yako na mutu mwengine mukiwa peke yenu, na ufanye hivyo kwa heshima, hilo litaonyesha kuwa unamuheshimu mutu huyo.—Mathayo 5:23-25.

  • Jaribu kujua anajisikia namna gani na pia mawazo yake. Kufanya hivyo ‘kunapunguza hasira [yetu]’ kwa sababu kunatusaidia tufikirie hali ya mutu mwengine. (Methali 19:11) Kunatusaidia pia tujione namna wengine wanatuona.

  • Jaribu kusamehe. Kusamehe ni jambo nzuri, lakini pia ni dawa nzuri. Kama ilivyoonyeshwa katika uchunguzi mumoja wa mwaka wa 2001, “mawazo ya kutokusamehe” yalitokeza “mwendo wa haraka sana” wa damu na yalifanya moyo upige haraka sana, lakini kusamehe wengine kulipunguza mahangaiko ya akili.—Wakolosai 3:13.

4 KUPATWA NA MAMBO YENYE KUOGOPESHA

Nieng, anayeishi katika inchi ya Kambodia, alipatwa na magumu mengi yenye kufuatana. Katika mwaka wa 1974, aliumia wakati bomu ililipuka kwenye uwanja wa ndege. Mwaka uliofuata, watoto wake wawili, mama yake, na bwana yake, wote walikufa. Katika mwaka wa 2000, nyumba yake na vitu vingine viliharibiwa na moto, na miaka tatu kisha hapo, bwana yake wa pili akakufa. Kwa sababu ya magumu hayo yote, alitaka kujiua.

‘Konzi [mukono] moja ya pumuziko ni afazali kuliko konzi mbili za kazi ngumu’

Lakini, Nieng alipata njia ya kupambana na magumu hayo yote. Kama Kari alivyofanya, Nieng pia alichunguza Biblia, akafaidika sana kutokana na mambo aliyojifunza, na akatumia wakati wake kuwasaidia wengine ili wafaidike na mambo hayo. Habari yake inatukumbusha uchunguzi wa mwaka wa 2008 uliofanywa na wachunguzi Waingereza. Walivumbua kwamba njia moja ya kuwa na “nguvu ya kupambana na mahangaiko ya akili,” ni “kutolea wengine . . . kwa njia fulani,” shauri hilo lilitolewa na Biblia tangu zamani.—Matendo 20:35.

Kwa kuongezea, Nieng alipata tumaini hakika juu ya wakati unaokuja ulio muzuri zaidi. Wakati huo matatizo yote yanayosumbua wanadamu yataisha, na “amani” nyingi itakuwa katika dunia yote.—Zaburi 72:7, 8.

Tumaini la kweli na hekima ya kupambana na mahangaiko mengi ya akili katika maisha, ni mambo mawili ya maana sana na yanaweza kupatikana katika Biblia. Mamilioni ya watu wamefaidika na kitabu hicho cha ajabu na kisichoweza kulinganishwa na vitabu vingine. Wewe pia unaweza kufaidika.