Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Injili ya Yuda” Ni Nini?

“Injili ya Yuda” Ni Nini?

KATIKA Mwezi wa 4, 2006, magazeti mengi duniani pote yalizungumuza juu ya habari yenye kushangaza iliyosema kwamba kikundi kimoja cha watu wenye elimu kingetolea watu mambo yaliyo katika maandishi fulani ya zamani, ambayo yalivumbuliwa hivi karibuni yenye kichwa “Injili ya Yuda.” Habari za magazeti hayo zilizungumuza juu ya mambo ambayo watu wenye elimu walidai, kwa kusema kwamba maandishi ya Injili hiyo yanabadilisha kabisa namna tunavyofikiri juu ya Yuda, mwanafunzi aliyemusaliti Yesu. Kulingana na mambo hayo yaliyosemwa na watu wenye elimu, kwa kweli Yuda alikuwa shujaa, mutume aliyemuelewa Yesu vizuri sana, na aliyemutoa Yesu ili auawe kwa sababu Yesu mwenyewe alimuomba Yuda afanye hivyo.

Je, maandishi hayo ni ya kweli? Na ikiwa ni ya kweli, je, yanafunua ujuzi fulani uliofichwa juu ya watu wanaojulikana katika historia kama vile Yuda Iskariote, Yesu Kristo, ao Wakristo wa kwanza? Je, maandishi hayo yanapaswa kubadilisha namna tunavyomuelewa Yesu na mafundisho yake?

NAMNA “INJILI YA YUDA” ILIVYOVUMBULIWA

Mupaka sasa watu hawajue vizuri namna “Injili ya Yuda” ilivyovumbuliwa. Kuliko kuvumbuliwa na kuchunguzwa na watu wanaochimba vitu vya zamani, maandishi hayo yalipatikana tu kwa gafula kwenye soko la vitu vya zamani sana mwishoni mwa miaka ya 1970 ao mwanzoni mwa miaka ya 1980. Inawezekana maandishi hayo yalivumbuliwa huko Misri katika mwaka wa 1978 ndani ya kaburi lililoachwa, labda katika pango ao shimo kubwa chini ya mulima ao chini ya jiwe kubwa. Injili hiyo ya Yuda ilikuwa kati ya maandishi 4 yaliyokuwa katika kodeksi (aina ya kitabu cha zamani) iliyoandikwa katika Koptiki (luga iliyotokana na luga ya zamani ya Misri).

Kwa sababu ya kulindwa kwa mamia ya miaka katika majira ya Misri yenye joto, kodeksi hiyo yenye jalada ya ngozi iliharibika haraka. Watu wachache wenye elimu walionyeshwa kwa muda mufupi kodeksi hiyo katika mwaka wa 1983; lakini haikununuliwa kwa sababu ilikuwa ya bei ya juu sana. Kodeksi hiyo iliharibika zaidi kwa sababu, kwa miaka mingine mingi, iliachwa na haikulindwa vizuri. Katika mwaka wa 2000, ilinunuliwa na mwanamuke mumoja wa inchi ya Suisse anayefanya biashara ya vitu vya zamani. Mwishowe, mwanamuke huyo alipana kodeksi hiyo kwa kikundi kimoja cha kimataifa cha watu wenye elimu, ambacho kilikuwa kinafanya kazi chini ya usimamizi wa shirika moja (Maecenas Foundation for Ancient Art and the National Geographic Society), watu wa kikundi hicho walishugulika na kazi ngumu ya kurudisha kodeksi hiyo katika hali nzuri, ambayo sehemu zake fulani zilikuwa zimekwisha kuachana-achana. Watu wa kikundi hicho walipaswa pia kujua mwaka ambao kodeksi hiyo iliandikwa, kuitafsiri, na kueleza mambo yaliyokuwa ndani.

Ufundi wa kujua tarehe ya vitu vya zamani unaoitwa Karboni-14 ulionyesha kama inawezekana kodeksi hiyo iliandikwa kati ya mwaka wa 201 na 300 ao kati ya mwaka wa 301 na 400 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Hata hivyo, watu wenye elimu waliwazia kama maandishi ya Koptiki ya “Injili ya Yuda” yaliyotafsiriwa kutoka katika luga ya Kigiriki cha zamani ndiyo yaliyokuwa ya zamani zaidi. Maandishi hayo ya zamani zaidi ya “Injili ya Yuda” yaliandikwa wakati gani na katika hali gani?

“INJILI YA YUDA” NI INJILI YA TANGU WAKATI WA WANYOSTI

“Injili ya Yuda” inatajwa kwa mara ya kwanza katika maandishi ya Irénée, askofu wa muji wa Lyon aliyeishi kati ya mwaka wa 101 na 200 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Irénée alipinga mafundisho ya vikundi vingi. Katika kitabu chake (Contre les hérésies) aliandika juu ya kikundi kimoja kati ya vikundi hivyo, alisema hivi: “Wanasema kwamba Yuda yule musaliti alijua vizuri mambo haya, na kwamba yeye peke yake, kwa kuwa alijua kweli kuliko wengine wote, alitimiza tendo la kusaliti ambalo lilikuwa fumbo. Kupitia yeye, vitu vyote, vya duniani na vya mbinguni, vilivurugika kabisa. Wanatokeza habari ya kuwazia tu ya aina hiyo, ambayo wanaita Injili ya Yuda.”

“Injili hiyo haikuandikwa wakati wa Yuda na mutu fulani aliyemujua Yuda”

Irénée aliazimia kabisa kupinga mafundisho mbalimbali ya Wakristo Wanyosti, waliojiwazia kuwa na ujuzi wa pekee ambao walifunuliwa. Kati ya mwaka wa 101 na 200 kisha kuzaliwa kwa Yesu, Wanyosti hao walieneza mafundisho yaliyotegemea maandishi yao wenyewe.

Mara nyingi, maandishi kama hayo ya Wanyosti yalisema bila usadikisho kwamba mitume wa Yesu wenye kujulikana sana hawakuelewa ujumbe wake na kwamba kuna fundisho la siri ambalo Yesu alifundisha na ni wachache tu ndio walilielewa. * Wanyosti fulani waliamini kwamba ulimwengu ambamo tunaishi ni gereza. Kwa hiyo, “mungu muumbaji” anayezungumuziwa katika Maandiko ya Kiebrania ni mungu wa hali ya chini sana, ambaye alilinganishwa na miungu mingine mitakatifu. Mutu aliyekuwa na “ujuzi” wa kweli alielewa “siri” hiyo na alitafuta kukombolewa kutokana na mwili huu wa nyama.

“Injili ya Yuda” inategemea mafundisho hayo. Inaanza kwa maneno haya: “Neno la siri lililosemwa na Yesu katika mazungumuzo yake na Yuda Iskariote kwa muda wa siku munane, mazungumuzo yaliyomalizika siku tatu mbele ya Yesu kufanya sikukuu ya Pasaka.”

Je, kodeksi hiyo ndiyo maandishi ambayo Irénée alizungumuzia, ambayo yalipotea kwa muda wa mamia ya miaka? Marvin Meyer, mushiriki wa kikundi ambacho kilichunguza na kutafsiri kodeksi hiyo, anasema kwamba “maelezo mafupi” ya Irénée “yanapatana kabisa na maandishi ya Koptiki yanayoitwa Injili ya Yuda.”

MABISHANO KATI YA WATU WENYE ELIMU JUU YA NAMNA YUDA ANAVYOELEZWA KATIKA INJILI HIYO

Katika “Injili ya Yuda,” Yesu anacheka kwa zarau wakati wanafunzi wake wanaonyesha ukosefu wa ujuzi unaofaa. Lakini kati ya mitume 12 wa Yesu, ni Yuda tu ndiye anaonyesha kwamba anamuelewa Yesu vizuri zaidi. Kwa hiyo, Yesu anamuelezea kwa siri “mafumbo ya ufalme.”

Kikundi cha kwanza cha watu wenye elimu waliotafsiri “Injili ya Yuda” na kuirudisha tena katika hali nzuri kilichochewa na mawazo ya Irénée. Katika tafsiri yao, Yuda anaonyeshwa kuwa yeye ndiye mwanafunzi aliyependwa sana na Yesu na ambaye angeelewa mafumbo na “kuingia” katika “ufalme.” Mitume waliodanganyika wangechagua mutu mwengine ambaye angechukua nafasi ya Yuda, lakini Yuda angekuwa “roho ya kumi na tatu” ambayo “ingepita [wale wanafunzi wengine] wote” kwa sababu, Yesu anamuambia, “utanisaidia kukombolewa kutoka katika mwili huu wa nyama.”

Waandikaji wa vitabu vyenye kuuzwa sana, kama vile Bart Ehrman na Elaine Pagels, ambao pia ni watu wenye elimu wanaojulikana sana wa wakati wa Wakristo wa kwanza na Wanyosti, walitangaza haraka uchunguzi wao mbalimbali na maelezo yao juu ya “Injili ya Yuda” ambayo yalifanana sana na tafsiri iliyofanywa na kile kikundi cha kwanza. Hata hivyo, muda mufupi kisha hapo, watu wengine wenye elimu, kama vile April DeConick na Birger Pearson, walionyesha hangaiko lao. Walidai kwamba shirika moja (National Geographic Society), katika juhudi za kutaka kueneza habari juu ya Injili hiyo, liliharakisha kuchapisha maandishi hayo ya zamani. Zaidi ya hilo, hatua ya kawaida ya kufanyiwa uchunguzi kwa uangalifu na watu wengine wenye elimu haikufuatwa, kwa sababu kikundi hicho kiliombwa kutia sahihi kwenye karatasi za makubaliano ya kutotangaza maandishi hayo.

Kati ya watu hao wenye elimu waliochunguza maandishi hayo, hakuna hata mumoja wao anayeonyesha kwamba maandishi hayo yana habari za kweli za kihistoria

Bila kutegemea kile kikundi cha kwanza, DeConick na Pearson wote wawili walifikia uamuzi wa kwamba sehemu fulani za maana za kodeksi hiyo, iliyokwisha kuachana-achana, zilitafsiriwa vibaya na kikundi cha kwanza cha watu wenye elimu. Kulingana na maandishi ambayo DeConick alirudisha katika hali nzuri, Yesu anamuita Yuda “Roho Muovu wa Kumi na Tatu,” wala si “roho ya kumi na tatu.” * Pia, Yesu anamuambia Yuda waziwazi kwamba hataingia katika “ufalme.” Kuliko kuwa mwenye “kuwapita” wanafunzi wengine, Yesu anamuambia Yuda hivi: “Utatenda vibaya zaidi kuliko wengine wote. Kwa sababu utanisaidia kukombolewa kutoka katika mwili huu wa nyama.” Kulingana na maoni ya DeConick, “Injili ya Yuda” ni maandishi ya zamani ya Wanyosti ambayo yanawazarau mitume wengine wote. Uamuzi wa mwisho wa DeConick na Pearson ni kwamba katika “Injili ya Yuda,” Yuda si shujaa.

TUNAWEZA KUJIFUNZA NINI KUTOKANA NA “INJILI YA YUDA”?

Iwe watu hao wenye elimu walimuona Yuda kuwa shujaa ao roho muovu katika injili hiyo, kati ya watu hao wenye elimu waliochunguza maandishi hayo, hakuna hata mumoja wao anayeonyesha kwamba maandishi hayo yana habari za kweli za kihistoria. Bart Ehrman anaeleza hivi: “Injili ya Yuda si Injili iliyoandikwa na Yuda, wala si Injili inayodai kuwa iliandikwa na Yuda. . . . Injili hiyo haikuandikwa wakati wa Yuda na mutu fulani aliyemujua Yuda . . . Kwa hiyo, si kitabu ambacho kitatutolea habari zaidi juu ya mambo yaliyotokea wakati wa maisha ya Yesu.”

“Injili ya Yuda” ni maandishi ya Wanyosti yaliyoandikwa kwanza katika luga ya Kigiriki kati ya mwaka wa 101 na 200 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Iwe “Injili ya Yuda” iliyovumbuliwa hivi karibuni inafanana na maandishi ambayo Irénée alizungumuzia ao hapana, jambo hilo linaendelea kuleta mabishano kati ya watu wenye elimu. Lakini “Injili ya Yuda” inatoa tu usadikisho wa maana juu ya wakati ambapo “Ukristo” uligawanyika katika vikundi vingi na mafundisho yaliyopingana. Kuliko kupunguza uzito wa Maandiko, “Injili ya Yuda” inahakikisha kwamba maonyo ya mitume ni ya kweli, kama vile onyo hili la Paulo linalopatikana katika andiko la Matendo 20:29, 30: “Ninajua kwamba baada ya kuondoka kwangu . . . kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.”

^ Mara nyingi, injili hizo ziliitwa kwa majina ya wale ambao walielewa vizuri mafundisho ya kweli ya Yesu, kama ilivyo kuhusu “Injili ya Tomasi” na “Injili ya Maria Magdalene.” Kwa ujumla, maandishi ya zamani karibu 30 yamepatikana.

^ Katika maandishi hayo, watu wenye elimu walio na maoni ya kwamba Yuda ni roho muovu, ni kusema, mutu ambaye alimuelewa Yesu vizuri kuliko wanafunzi wengine, wanatetea maoni yao kwa kusema kama, katika masimulizi ya Biblia ya Injili, roho waovu walimutambua Yesu vizuri.​—Marko 3:11; 5:7.