Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAMBO YA KUFANYA ILI KUWA NA FURAHA KATIKA FAMILIA

Ikiwa Mutoto Wako Ni Mulemavu

Ikiwa Mutoto Wako Ni Mulemavu

CARLO * anasema hivi: “Mutoto wetu, Angelo, ana ugonjwa wa kupooza miguu. Ugonjwa wake unatumaliza nguvu za mwili, za akili, na za moyo. Wazia nguvu unazohitaji ili kushugulikia mutoto aliye na afya nzuri, na kisha uzidishe nguvu hizo mara mia moja. Nyakati nyingine, tunakosa muda wa kushugulikia ndoa yetu.”

MIA alisema hivi: “Inaomba wakati murefu na uvumilivu mwingi ili kumufundisha Angelo kufanya mambo mepesi. Ninapojisikia kuwa nimechoka kabisa, nina mwelekeo wa kukasirika na kukosa uvumilivu kuelekea bwana yangu, Carlo. Nyakati nyingine, tunakosana juu ya mambo fulani, na kisha tunaanza kubishana.”

Je, unaweza kukumbuka tarehe ambayo mutoto wako alizaliwa? Bila shaka, ulikuwa na tamaa kubwa ya kumubeba mikononi. Hata hivyo, kwa wazazi wengi kama Carlo na Mia, furaha yao inachangana na mahangaiko wanapoambiwa kwamba mutoto wao ni mugonjwa ao mulemavu.

Je, una mutoto mulemavu? Kama ni hivyo, labda unaweza kujiuliza ikiwa utaweza kupambana na tatizo hilo. Hata hivyo, usivunjike moyo. Wazazi kama wewe wameweza kupambana na matatizo kama hayo. Fikiria matatizo matatu ya kawaida ambayo unaweza kupambana nayo na namna hekima ya Biblia inavyoweza kukusaidia.

TATIZO LA 1: UNAONA KUWA NI VIGUMU KUKUBALI KAMA MUTOTO WAKO NI MULEMAVU.

Wazazi wengi wanajisikia kuwa wenye kuvunjika moyo wanapojulishwa kwamba mutoto wao ni mugonjwa. Juliana, mama mumoja huko Mexique, anasema hivi: “Waganga waliponiambia kama mutoto wetu Santiago alikuwa na ugonjwa wa kupooza ubongo, sikuweza kuamini jambo hilo. Nilijisikia kuwa dunia inaniangukia.” Wengine wanaweza kujisikia kama vile Villana, mama mumoja huko Italie. Anasema hivi: “Niliamua kuzaa mutoto hata ikiwa kuzaa kunaleta matatizo kwa mama walio na umri wangu. Sasa, mutoto wangu anapopatwa na matatizo yanayotokana na ugonjwa wake wa kupooza miguu, ninajisikia kuwa mwenye kosa.”

Ikiwa unapambana na mawazo ya kujisikia kuwa mwenye kuvunjika moyo ao mwenye kosa, tambua kwamba mawazo hayo yanaeleweka. Hapo mwanzoni, Mungu hakukusudia watu wagonjwe. (Mwanzo 1:27, 28) Hakuumba wazazi wakiwa na uwezo wa kukubali kwa vyepesi mambo yasiyo ya kawaida. Katika njia fulani, unaweza “kuhuzunika sana” kwa sababu ya afya mbaya ya mutoto wako. Inaweza kukuchukua wakati ili kushinda mawazo ya kujisikia kuwa mwenye kuvunjika moyo ao mwenye kosa na kukubali kuishi kulingana na hali yako mupya.

Utafanya nini ikiwa unajisikia kuwa mwenye kosa kwa sababu ya ulemavu wa mutoto wako? Kumbuka kwamba hakuna mutu anayeelewa kabisa namna chembe za uriti, mazingira, na mambo mengine yanavyoweza kuchangia katika afya ya mutoto. Kwa upande mwengine, unaweza kuwa na mwelekeo wa kumulaumu bibi ao bwana yako. Pinga mwelekeo huo. Itakuwa vizuri zaidi ikiwa unamuunga mukono bibi ao bwana yako na kukaza akili juu ya namna ya kumutunza mutoto wenu.​—Mhubiri 4:9, 10.

PENDEKEZO: Ujifunze juu ya hali ya mutoto wako. Tafsiri fulani ya Biblia inasema hivi: “Inaomba hekima ili kuwa na familia nzuri, na inaomba uelewaji ili kuifanya iwe yenye nguvu.”​—Methali 24:3.

Unaweza kujifunza mambo mengi kutoka kwa waganga na vichapo vyenye kutumainika. Hatua ya kujifunza juu ya hali ya mutoto wako inaweza kulinganishwa na kujifunza luga mupya. Mwanzoni, itakuwa vigumu kwako kujifunza juu ya hali ya mutoto wako, lakini unaweza kufanya hivyo.

Carlo na Mia, waliotajwa mwanzoni mwa habari hii, walitafuta habari kutoka kwa muganga wao na kutoka kwa shirika fulani ambalo linashugulika na hali kama ile ya mutoto wao. Wanasema hivi: “Jambo hilo lilitusaidia kuelewa matatizo ambayo tulitazamia kupambana nayo na pia tulijifunza mambo ambayo mutu aliye na ugonjwa wa kupooza miguu anaweza kufanya. Tuliona kwamba mutoto wetu anaweza kuishi maisha ambayo ni ya kawaida katika hali nyingi. Jambo hilo lilitufariji sana.”

MUJARIBU KUFANYA HIVI: Mukaze akili juu ya mambo ambayo mutoto wenu anaweza kufanya. Mupange kufanya mambo mbalimbali mukiwa familia. Mutoto wenu anapoweza kufanya hata jambo fulani ndogo, muwe tayari kumupongeza na kushangilia “ushindi” huo pamoja naye.

TATIZO LA 2: UNAJISIKIA KUWA PEKE YAKO NA MWENYE KUCHOKA.

Unaweza kujisikia kuwa kumutunza mutoto wako aliye mugonjwa kunamaliza nguvu zako zote. Jenney, mama mumoja huko Nouvelle-Zélande anasema hivi: “Kwa miaka michache kisha mutoto wetu kupatwa na ugonjwa wa uti wa mugongo, nilikuwa ninachoka kabisa na kulia ikiwa nilijaribu kufanya kazi ya zaidi nyumbani.”

Tatizo lingine linaweza kuwa kujisikia uko peke yako. Ben ana mutoto anayesumbuliwa na ugonjwa wa kasoro ya misuli na ugonjwa wa akili. Anasema, “Watu wengi hawataelewa hata kidogo namna maisha yetu yalivyo.” Unaweza kutaka sana kuzungumuza na mutu fulani. Lakini, wengi kati ya marafiki wako wana watoto walio na afya nzuri. Kwa hiyo, unasita kuwaelezea namna unavyojisikia.

PENDEKEZO: Uombe musaada. Na watu wengine wanapokutolea musaada huo, uwe tayari kuukubali. Juliana, aliyetajwa hapo juu, anasema hivi: “Nyakati nyingine, mimi na bwana yangu tunasikia haya kuomba musaada.” Hata hivyo, Juliana anaongeza, “Tumejifunza kwamba hatuwezi kujitegemea. Watu wengine wanapotusaidia, hatujisikie kuwa peke yetu.” Ikiwa rafiki unayependa sana ao mutu wa familia anaomba kukaa na mutoto wako kwenye tukio fulani la watu wengi ao kwenye mikutano ya kutaniko, ukubali kwa moyo wote. Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

Shugulikia afya yako mwenyewe. Kama vile tu motokari inayobeba wagonjwa inavyopaswa kutiwa mafuta kwa ukawaida ili kuendelea kubeba wagonjwa kwenye hopitali, wewe pia unapaswa kujitia nguvu kwa kula vizuri, kufanya mazoezi, na kupumuzika vya kutosha ili uendelee kumutolea mutoto wako matunzo anayohitaji. Javier, aliye na mutoto mulemavu anasema hivi: “Mutoto wangu hawezi kutembea, kwa hiyo ninapaswa kula vizuri kwa sababu ni mimi ninayemutembeza. Miguu yangu ndiyo miguu yake!”

Namna gani unaweza kupata wakati wa kushugulikia afya yako mwenyewe? Wazazi fulani wanagawanya siku ambazo kila mumoja wao atamushugulikia mutoto wao mugonjwa. Kwa hiyo, muzazi mumoja anaweza kupumuzika ao kushugulikia mahitaji yake mengine. Utahitaji kukomboa wakati kwa kuacha mambo yasiyo ya lazima, na inaweza kuwa vigumu kuendelea kuwa na usawaziko. Lakini, kama Mayuri, mama mumoja huko Inde alivyosema, “Mwishowe utazoea hali hiyo.”

Uzungumuze na rafiki unayetumainia. Hata marafiki ambao hawana watoto wagonjwa wanaweza kukusikiliza na kukufariji. Unaweza pia kusali kwa Yehova Mungu. Je, sala inaweza kusaidia kabisa? Yazmin aliye na watoto wawili walio na ugonjwa fulani unaovimbisha sehemu mbalimbali za ndani ya mwili, anasema hivi: “Kuna nyakati za mikazo mingi ambapo nilijisikia kama kwamba nitakufa tu.” Lakini anaongeza hivi: “Ninasali kwa Yehova ili kupata kitulizo na nguvu. Kisha, ninajisikia kuwa na nguvu za kuendelea kupambana na tatizo langu.”​—Zaburi 145:18.

MUJARIBU KUFANYA HIVI: Mufikirie chakula munachokula, ni wakati gani munafanya mazoezi, na ikiwa munalala kwa muda wa saa ngapi. Muone namna munavyoweza kununua wakati kwa kuacha mambo yasiyo ya lazima ili muweze kushugulika na afya yenu wenyewe. Muendelee kubadilisha programu yenu kadiri inavyowezekana.

TATIZO LA 3: MUNAMUHANGAIKIA ZAIDI MUTOTO WENU MUGONJWA KULIKO WATOTO WENGINE KATIKA FAMILIA.

Kuhangaikia sana mutoto aliye na ugonjwa fulani kunaweza kubadilisha mambo mengi katika familia, kama vile kula, mahali familia inapopanga kutembelea na wakati ambao wazazi wanapitisha pamoja na kila mutoto. Kwa sababu hiyo, watoto wengine wanaweza kujisikia kuwa wanapuuzwa. Zaidi ya hilo, wazazi wanaweza kushugulikia sana mutoto wao aliye mugonjwa hivi kwamba wanakosa kushugulikia ndoa yao. Lionel, baba fulani huko Liberia anasema hivi: “Nyakati fulani, bibi yangu anasema kwamba yeye ndiye anafanya kazi nyingi zaidi na kwamba mimi simuhangaikie mutoto wetu aliye mugonjwa. Ninajisikia kuwa ananizarau na wakati fulani ninamujibu vibaya.”

PENDEKEZO: Ili kuhakikishia watoto wenu wote kwamba munapendezwa nao, mupange kufanya mambo wanayofurahia. Jenney anayetajwa hapo juu anasema hivi: “Wakati mwengine, tunafanya jambo fulani la pekee kwa ajili ya mutoto wetu mukubwa, hata ikiwa tulitoka tu kula chakula cha muchana kwenye restora anayopenda sana.”

Upendezwe na watoto wako wote

Ili kulinda ndoa yenu, ni vizuri kuzungumuza na kusali pamoja. Aseem, baba mumoja huko India ambaye mutoto wake anasumbuliwa na ugonjwa wa kifafa, anasema hivi: “Hata ikiwa wakati fulani mimi na bibi yangu tunajisikia kuwa wenye kuchoka sana na kuvunjika moyo, tunapanga wakati wa kukaa, kuzungumuza na kusali pamoja. Kila asubuhi, mbele watoto wetu waamuke, tunapitisha wakati pamoja ili kuzungumuzia andiko fulani la Biblia.” Watu wengine waliooana wanazungumuza kipekee mbele ya kuenda kulala. Mazungumuzo yenu ya siri na sala za kutoka moyoni zitatia nguvu ndoa yenu wakati wa shida kali za maisha. (Methali 15:22) Kama vile bwana mumoja na bibi yake walivyosema, “nyakati nzuri zaidi katika maisha yetu ya ndoa ni nyakati tunapokuwa na matatizo makubwa zaidi.”

MUJARIBU KUFANYA HIVI: Muwapongeze watoto wenu wengine kwa musaada wowote ambao wanamutolea mutoto wenu mugonjwa. Mara kwa mara, umuelezee bibi ao bwana yako na pia watoto wako wengine kwamba unawapenda na kuwasamini.

ENDELEA KUWA NA TUMAINI

Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni Mungu ataondoa kila aina ya ugonjwa na ulemavu ambao unawasumbua vijana na wazee. (Ufunuo 21:3, 4) Wakati huo, ‘hakuna mukaaji atakayesema: Mimi ni mugonjwa.’ *​—Isaya 33:24.

Muzazi, unapongojea kutimizwa kwa ahadi hiyo, unaweza kufanikiwa kumutunza mutoto aliye mulemavu. Carlo na Mia waliotajwa mwanzoni mwa habari hii, wanasema hivi: “Usivunjike moyo inapoonekana kwamba mambo hayaende vizuri. Kaza akili juu ya mambo mazuri ambayo mutoto wako anafanya, kwa sababu kuna mambo mengi mazuri anayofanya.”

^ Majina katika habari hii yamebadilishwa.

^ Unaweza kusoma habari nyingi zaidi juu ya ahadi ya Biblia kuhusu afya kamilifu katika sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

UJIULIZE . . .

  • Ninafanya nini ili afya yangu ya kimwili, ya kiroho, na ya moyoni iendelee kuwa nzuri?

  • Ni wakati gani niliwapongeza kwa mara ya mwisho watoto wangu kwa musaada wanaotoa?