Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sababu Gani Kuna Mateso Mengi Sana?

Sababu Gani Kuna Mateso Mengi Sana?

Ili kuelewa sababu gani kuna mateso mengi sana na sababu gani wanadamu wameshindwa kuyaondoa hata ikiwa wanajikaza sana, tunahitaji kujua sababu za kweli zinazofanya kuwe na mateso. Ijapokuwa sababu ni nyingi na ngumu kuelewa, tunafurahi kwa sababu Biblia inatusaidia kuelewa sababu hizo. Katika habari hii, tutachunguza sababu tano kubwa ambazo zinafanya kuwe na mateso. Tunakuomba uchunguze kwa uangalifu mambo ambayo Biblia inasema na kuona namna Neno la Mungu linaweza kukusaidia kuelewa waziwazi sababu ya kweli inayofanya kuwe na mateso.​—2 Timotheo 3:16.

Biblia inasema kwamba ‘mutu yeyote muovu anapotawala, watu wanaugua.’​—Methali 29:2.

Historia ya wanadamu inajaa na madikteta ambao walitawala bila huruma, na hivyo wakaletea raia wao mateso mengi sana. Bila shaka, si watawala wote ambao wanatawala bila huruma. Watawala fulani wanaweza kuwa na nia nzuri kuelekea wanadamu wenzao. Hata hivyo, mara tu wanapopata mamlaka, wanatambua kwamba bidii yao inazuiwa na watu ambao wanagombania mamlaka. Ao wanaweza kutumia vibaya mamlaka yao ili kujifaidi wenyewe, na kuacha watu wengine wateseke. Henry Kissinger, waziri wa zamani wa Amerika wa mambo ya inje alisema hivi: “Historia inasimulia kuhusu bidii ya wanadamu iliyoshindwa na matumaini yaliyokosa kutimizwa.”

Biblia nayo inasema hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Wanadamu wasio wakamilifu hawana hekima na uwezo unaohitajiwa wa kuona matukio yaliyo mbele na kupanga mambo yao yote ili kupata matokeo mazuri. Ikiwa wanadamu hawawezi kuongoza hatua zao wenyewe, namna gani wanaweza kuongoza hatua za taifa? Je, unaona sababu gani watawala wa kibinadamu hawana uwezo wa kuondoa mateso? Kwa kweli, mara nyingi serikali ao utawala mubaya, ndio unaletea watu mateso!

Yesu alisema hivi: ‘Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mukiwa na upendo kati yenu wenyewe.’​—Yohana 13:35.

Viongozi wa dini zote wanafundisha upendo na umoja. Jambo la kweli ni kwamba wameshindwa kuingiza ndani ya mioyo ya wafuasi wao upendo wenye nguvu sana ambao unaweza kuwasaidia kumaliza ubaguzi. Kuliko kuwasaidia kuwa na upendo, mara nyingi dini inachangia kuleta migawanyiko, ubaguzi, na magomvi kati ya watu na kati ya mataifa. Mwishoni mwa kitabu chake, mwanateolojia Hans Küng, aliandika hivi: “Mapambano ya kisiasa ambayo yamekuwa mabaya na yenye kuua watu wengi zaidi ni yale ambayo yamechochewa, yameongozwa na kuruhusiwa na dini.” (Christianity and the World Religions)

Zaidi ya hilo, viongozi wa dini nyingi wameruhusu waziwazi uasherati na uzinifu, na ngono kati ya wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake. Hilo limefanya magonjwa yaenee sana, kutoa mimba, mimba ambazo hazitakiwe, na ndoa na familia zinazovunjika, mambo yote hayo yanatokeza maumivu na huzuni nyingi sana.

‘Kila mutu anajaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, inazaa zambi.’​—Yakobo 1:14, 15.

Kwa sababu ya kutokamilika ambako tumeriti, sisi wote tunafanya makosa na tunapaswa kupiganisha tamaa ya ‘kufanya mambo yanayopendwa na mwili.’ (Waefeso 2:3) Ni vigumu zaidi kushinda tamaa mbaya wakati tunapata nafasi nzuri ili kutimiza tamaa hiyo. Matokeo yanaweza kuwa mabaya ikiwa tunashindwa na tamaa mbaya.

Mwandikaji Phiroz Mehta aliandika hivi: “Mateso mengi zaidi yanatokana na tamaa yetu wenyewe, kushindwa kujizuia katika kujifurahisha na kuponda raha, pupa yetu na tamaa ya kutafuta makuu.” Tamaa na kuzoea kutumia vitu kama vile pombe, dawa za kulewesha, kucheza michezo ya feza, kufanya ngono, na kazalika, mambo yote hayo yameharibu “watu wengi wenye kuheshimika” na yameletea mateso familia zao, marafiki wao, na watu wengine. Kwa sababu ya hali ya kutokamilika kwa wanadamu, tunapaswa kukubaliana na maneno haya ya Biblia : “Kwa maana tunajua kwamba uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja.”​—Waroma 8:22.

Biblia inaonyesha kwamba Shetani ndiye ‘mungu wa mufumo huu wa mambo’ na kwamba anaungana na roho waovu wenye nguvu wanaoitwa mashetani.​—2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 12:9.

Kama Shetani, mashetani wanafanya bidii sana ili kutia watu chini ya mamlaka yao na kuwaongoza vibaya. Mutume Paulo alijua jambo hilo aliposema hivi: “Tuna kushindana mweleka, si juu ya damu na mwili, bali juu ya serikali, juu ya mamlaka, juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.”​—Waefeso 6:12.

Ijapokuwa mashetani wanafurahia kusumbua watu, jambo hilo si kusudi lao la kwanza. Kusudi lao la kwanza ni kufanya watu wamuache Yehova, Mungu Aliye Juu Zaidi. (Zaburi 83:18) Mazoea kama vile elimu ya nyota, uchawi, ulozi, na uaguzi ni kati ya mitego ambayo mashetani wanatumia ili kuwadanganya watu na kuwatia chini ya mamlaka yao. Ndiyo sababu Yehova anatuonya juu ya hatari hizo na analinda wale wote wanaomupinga Shetani na mashetani wake.​—Yakobo 4:7.

Kumepita miaka karibu elfu mbili tangu Biblia ilipotabiri hivi: ‘Ujue jambo hili, ya kwamba katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushugulika nazo.’

Ili kuonyesha mambo yanayofanya nyakati zetu ziwe za hatari, Biblia inaendelea kusema hivi: ‘Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, . . . wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumupenda Mungu.’ Kwa kweli, sababu kubwa inayofanya kuwe na mateso yote ambayo tunaona leo ni kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.”​—2 Timotheo 3:1-4.

Kwa sababu ya mambo ambayo tumechunguza, je, umeona waziwazi sababu gani wanadamu hawawezi kumaliza mateso, hata ikiwa wana nia nzuri? Ni wapi basi tunaweza kupata musaada? Tunapaswa kumutumainia Muumbaji wetu, ambaye ameahidi kwamba ‘atazivunja kazi za Ibilisi’ na wafuasi wake. (1 Yohana 3:8) Habari inayofuata itazungumuzia mambo ambayo Mungu atafanya ili kumaliza mambo yote yanayofanya kuwe na mateso.