Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

“Yehova Hakunisahau”

“Yehova Hakunisahau”
  • ALIZALIWA MWAKA WA 1922

  • ALIZALIWA KATIKA INCHI YA HISPANIA

  • ALIKUWA MWALIMU WA DINI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa katika muji wa Bilbao, eneo la watu wa kawaida, kaskazini mwa Hispania. Nilikuwa mutoto wa pili kati ya watoto ine. Watu wa familia yetu walikuwa Wakatoliki wenye bidii, na nilienda kwenye Misa kila siku. Nilipokuwa na miaka 23, nikakuwa mwalimu, nilipenda kazi hiyo ya ualimu na nikaiendelesha kwa miaka 40. Pia nilipenda sana kufundisha imani ya dini ya Katoliki, ndiyo maana wakati wa mangaribi nilikuwa ninafundisha watoto wanawake ili kuwatayarisha kwa ajili ya kukomonika ao kula ekaristia mara ya kwanza.

Kisha miaka 12 ya furaha katika ndoa, nilibaki mujane nikichunga mabinti wangu 4. Nilikuwa tu na miaka 33! Nilijikaza kupata faraja katika imani yangu ya dini ya Katoliki, lakini nilikuwa na maulizo ambayo nilijiuliza mara kwa mara. Nilijiuliza hivi: ‘Sababu gani wanadamu wanaendelea kufa ikiwa Kristo alitukomboa? Sababu gani tunasali Ufalme wa Mungu uje ikiwa watu wazuri wanaenda mbinguni?’ Na zaidi ya yote, niliwaza hivi: ‘Ikiwa Mungu anatuhukumu wakati tunakufa, sababu gani tunahitaji baadaye kutoka mbinguni, kutoka katika pirigatori, ao katika moto wa mateso kwa ajili ya hukumu ya mwisho?’

Niliwauliza mapadri fulani niliokutana nao maulizo hayo. Mumoja wao alinijibu hivi: “Sijue. Umuulize askofu. Sababu gani jambo hilo linakusumbua? Unaamini Mungu, sivyo? Achana na mambo hayo!” Lakini niliendelea kutafuta majibu. Kisha hapo, nilifuata mafundisho ya Wajesuti, Wapentekoste, na Wanyosti. Lakini hakuna mumoja wao aliyenipatia majibu yenye kunisadikisha.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU:

Nilipokuwa na miaka 60 na kitu, mwanafunzi mumoja wa miaka saba alinialika nihuzurie mukutano wa Mashahidi wa Yehova. Nilifurahia sana mambo niliyoona na kusikia, lakini kwa sababu nilikuwa na mambo mengi ya kufanya katika maisha, sikuonana tena na Mashahidi wa Yehova wakati huo. Miaka miwili kisha hapo, Juan na Maite ambao ni bibi na bwana waligonga kwenye mulango wangu. Kwa muda wa miezi tatu, tulikuwa na mazungumuzo ya mara kwa mara ya maulizo na majibu, na mwishowe nilikubali kujifunza nao Biblia.

Nilikuwa ninangojea kwa hamu sana siku ya kujifunza Biblia! Nilichunguza kila jambo kwa uangalifu kabisa, kwa kutumia tafsiri tatu za Biblia ili kuhakikisha ikiwa mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni ya kweli. Bila kukawia nilitambua namna dini ilinidanganya kwa miaka mingi. Nilivurugika kwa sababu ya tofauti kati ya mafundisho ambayo niliamini mbele na yale ambayo nilikuwa ninajifunza sasa katika Biblia. Nilichanganyikiwa sana, kwa sababu mafundisho yangu ya zamani yalikuwa ndani yangu kama muti wenye mizizi mirefu na uliokuwa unaongolewa.

Nilijua kuwa nilipata hazina

Kisha, bwana yangu wa pili akagonjwa sana na akakufa. Karibu na wakati huo, niliacha kazi yangu ya ualimu na nikatoka katika muji wa Bilbao kwa muda. Juan na Maite walihama pia. Jambo la kusikitisha ni kwamba niliacha kujifunza Biblia. Lakini ndani yangu, nilijua kuwa nilipata hazina. Sikusahau hazina hiyo hata kidogo.

Miaka 20 baadaye, nilipokuwa na miaka 82, Juan na Maite walirudia Bilbao na wakanitembelea. Nilifurahi sana kuwaona tena! Nilitambua kwamba Yehova hakunisahau, na nikaanza tena kujifunza Biblia. Juan na Maite walinivumilia sana, nilipowauliza maulizo yaleyale tena na tena. Nilihitaji kusikia mawazo ya Biblia mara kwa mara ili kuachana kabisa na mafundisho yangu ya zamani. Pia nilitaka kuwa na musingi muzuri ili niweze kuwafasiria marafiki wangu na watu wa familia yangu kweli ya Biblia.

Mwishowe, nilibatizwa nikiwa na miaka 87, hiyo ilikuwa siku ya furaha sana katika maisha yangu. Nilibatizwa kwenye mukusanyiko wa Mashahidi wa Yehova. Muzee Mukristo alitoa hotuba yenye kutegemea Biblia ambayo ilielekezwa hasa kwa wale waliobatizwa siku hiyo. Hotuba hiyo ilinifanya nitoe machozi. Nilisikiliza hotuba hiyo vizuri, ni kama tu Yehova alikuwa akizungumuza na mimi moja kwa moja. Kisha tu kubatizwa, Mashahidi wengi walikuja kunipongeza, hata kama wengi kati yao walikuwa hawanijue!

FAIDA AMBAYO NIMEPATA:

Nilikuwa ninajua kwamba Yesu Kristo ndiye “njia.” (Yohana 14:6) Lakini funzo langu la Biblia liliniwezesha kumujua Yehova, ambaye Yesu anatuongoza kwake. Sasa ninaweza kusali kwa Mungu kama vile kwa Baba na Rafiki mupendwa. Kusoma kitabu Mkaribie Yehova * lilikuwa jambo la maana sana katika maisha yangu. Mara ya kwanza nilikisoma chote katika usiku mumoja! Niliguswa moyo sana kujua kwamba Yehova ni mwenye rehema sana.

Wakati ninafikiria muda murefu ambao nilitumia ili kutafuta dini ya kweli, ninakumbuka maneno haya ya Yesu: ‘Endeleeni kuomba, nanyi mutapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mutapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mutafunguliwa.’ (Mathayo 7:7) Sasa nimepata majibu ya maulizo ambayo nilitafuta kwa muda murefu, na ninafurahi kuwaambia wengine mambo hayo.

Nikiwa sasa na miaka 90, ninajisikia kwamba ningali na mambo mengi ya kujifunza kumuhusu Yehova. Kila mukutano ninaohuzuria kwenye Jumba la Ufalme ni kipindi cha pekee kwangu katika njia mbili, kwanza ninapata mafundisho mazuri na tena ninashirikiana na ndugu na dada zangu Wakristo. Ninatamani sana kuwa mwalimu tena katika dunia Paradiso iliyoahidiwa. (Ufunuo 21:3, 4) Ninangojea kwa hamu sana kuwaona tena watu niliowapenda waliokufa wafufuliwe na kupata nafasi ya kuwafundisha kweli ya Biblia. (Matendo 24:15) Ninatamani sana pia kuwaeleza juu ya zawadi nzuri ambayo Yehova alinipatia katika siku zangu za uzee.

^ Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.