Hamia kwenye habari

Yesu Alisema Tunapaswa Kuwatendeaje Wengine?

Yesu Alisema Tunapaswa Kuwatendeaje Wengine?

Jibu la Biblia

 Katika Mahubiri ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu alifundisha jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine. Katika Kiingereza, maneno yake yamepewa jina “Kanuni Bora” ingawa jina hilo halipatikani katika Biblia. Yesu alisema hivi: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12; Luka 6:31.

 Ile Kanuni Bora inamaanisha nini?

 Ile Kanuni Bora inatutia moyo tuwatendee wengine kama ambavyo sisi tungependa kutendewa. Kwa mfano, watu wengi wanathamini sana wanapotendewa kwa heshima, fadhili, na upendo. Hivyo, inapatana na akili kwamba tuwatendee wengine vivyo hivyo.

 Kwa nini ile Kanuni Bora ina manufaa?

 Ile Kanuni Bora inatumika karibu katika hali zote. Kwa mfano, inaweza . . .

 Ile Kanuni Bora inaongoza mambo mengi kati ya yanayotajwa katika ile inayojulikana kuwa Agano la Kale. Kanuni hiyo ambayo Yesu alitaja “ndiyo maana ya Sheria [vile vitabu vitano vya kwanza katika Biblia] na Manabii [vitabu vya kinabii].” (Mathayo 7:12) Kwa maneno mengine, ile Kanuni Bora inaonyesha kweli ya msingi inayofanyiza Agano la Kale: upendo kwa jirani.—Waroma 13:8-10.

 Je, ile Kanuni Bora inaonyesha tu wazo la nipe-nikupe?

 Hapana. Ile Kanuni Bora inakazia hasa kutoa. Yesu alipotoa ile Kanuni Bora alikuwa akizungumzia jinsi ya kuwatendea watu wote kutia ndani maadui wa mtu. (Luka 6:27-31, 35) Hivyo, ile Kanuni Bora inawatia moyo watu wawatendee watu wote mema.

 Unaweza kuionyeshaje ile Kanuni Bora?

  1.  1. Uwe makini. Wakazie uangalifu wale wanaokuzunguka. Kwa mfano, huenda ukamwona mtu aliyebeba mfuko mzito, ukasikia kwamba jirani amelazwa hospitalini, au ukaona mfanyakazi mwenzako amevunjika moyo. Unapoangalia “faida za wengine,” huenda utapata nafasi za kusema au kufanya jambo litakalowasaidia.—Wafilipi 2:4.

  2.  2. Onyesha hisia-mwenzi. Jiweke katika hali ya yule mtu mwingine. Ungehisije ikiwa ungekabili hali kama yake? (Waroma 12:15) Unapojaribu kuelewa hisia za wengine, huenda ukachochewa kuwasaidia.

  3.  3. Uwe mwenye usawaziko. Kumbuka kwamba kila mtu ni tofauti. Mambo ambayo huenda wengine wakapenda kufanyiwa yasiwe yale ambayo wewe ungependa kufanyiwa. Kwa hiyo, kati ya mambo mengi unayoweza kufanya, jaribu kuchagua kile ambacho watathamini zaidi.—1 Wakorintho 10:24.