Hamia kwenye habari

Je, Biblia Inafundisha Mtu Anaweza Kuzaliwa Upya Katika Mwili Mwingine?

Je, Biblia Inafundisha Mtu Anaweza Kuzaliwa Upya Katika Mwili Mwingine?

Jibu la Biblia

 Hapana, haifundishi hivyo. Maneno “kuzaliwa upya katika mwili mwingine” hayapatikani katika Biblia wala wazo lenyewe halifundishwi katika Biblia. Imani katika kuzaliwa upya katika mwili mwingine inategemea fundisho la kutokufa kwa nafsi. a Hata hivyo, Biblia inafundisha kwamba nafsi ndiye mtu mwenyewe na hivyo anaweza kufa. (Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4) Mtu anapokufa, anaacha kuwepo.​—Mwanzo 3:​19; Mhubiri 9:​5, 6.

Kuna tofauti gani kati ya kuzaliwa upya katika mwili mwingine na ufufuo?

 Fundisho la Biblia la ufufuo halitegemei kutokufa kwa nafsi. Katika ufufuo, watu waliokufa watafanywa kuwa hai tena kupitia nguvu za Mungu. (Mathayo 22:23, 29; Matendo 24:15) Ufufuo unatoa tumaini hakika la mtu kurudishwa awe hai katika dunia mpya akiwa na tumaini la kuishi bila kufa tena.​—2 Petro 3:​13; Ufunuo 21:​3, 4.

Maoni yasiyo ya kweli kuhusu kuzaliwa upya katika mwili mwingine na Biblia

 Uwongo: Biblia inasema kwamba nabii Eliya alizaliwa upya katika mwili mwingine na kutokea akiwa Yohana Mbatizaji.

 Ukweli: Mungu alitabiri hivi: “Nawatumia ninyi nabii Eliya,” naye Yesu alionyesha kwamba Yohana Mbatizaji ndiye aliyetimiza unabii huu. (Malaki 4:5, 6; Mathayo 11:13, 14) Hata hivyo, hilo halikumaanisha kwamba Eliya alikuwa amezaliwa upya katika mwili wa Yohana Mbatizaji. Yohana mwenyewe alisema kwamba yeye si Eliya. (Yohana 1:​21) Badala yake, Yohana alifanya kazi kama ile ya Eliya, kutangaza ujumbe wa Mungu kuhusu toba. (1 Wafalme 18:36, 37; Mathayo 3:1) Pia Yohana alikuwa na “nguvu za Eliya.”​—Luka 1:13-17.

 Uwongo: Biblia inamaanisha kuzaliwa upya katika mwili mwingine inapozungumzia “kuzaliwa tena.”

 Ukweli: Biblia inaonyesha kwamba kuzaliwa tena ni kuzaliwa kwa njia ya kiroho jambo linalotokea mtu anapokuwa hai bado. (Yohana 1:​12, 13) Kuzaliwa huko tena, si kwa sababu ya matendo ambayo mtu alifanya zamani, bali ni baraka kutoka kwa Mungu, na wote wanaoipokea wanapata tumaini la pekee la wakati ujao.​—Yohana 3:3; 1 Petro 1:​3, 4.

a Imani katika kutokufa kwa nafsi na kuzaliwa upya katika mwili mwingine ni imani ambazo inaonekana zilianzia Babiloni la kale. Baadaye, wanafalsafa Wahindi walianzisha fundisho la Karma. Kulingana na kitabu Britannica Encyclopedia of World Religions, Karma ni “sheria ya kisababishi na tokeo, ambayo inasema kwamba mambo ambayo mtu anafanya katika maisha ya sasa atapata matokeo yake katika maisha yake yanayofuata.”​—Ukurasa wa 913.