Hamia kwenye habari

Ufufuo Ni Nini?

Ufufuo Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Katika Biblia, neno linalotafsiriwa “ufufuo” linatokana na neno la Kigiriki a·naʹsta·sis, linalomaanisha “kuinua” au “kusimama tena.” Mtu ambaye amefufuliwa ameinuliwa kutoka kwenye kifo na kurudishwa awe hai akiwa mtu aliyekuwa hapo awali.​—1 Wakorintho 15:12, 13.

 Ingawa neno “ufufuo” halipatikani katika Maandiko ya Kiebrania, ambayo mara nyingi yanaitwa Agano la Kale, fundisho hilo linapatikana humo. Kwa mfano, kupitia nabii Hosea, Mungu aliahidi: “Nitawakomboa wao kutoka katika mkono wa Kaburi; nitawaokoa wao kutoka kwenye kifo.”​—Hosea 13:14; Ayubu 14:13-​15; Isaya 26:19; Danieli 12:​2, 13.

 Watu watafufuliwa waishi wapi? Watu fulani watafufuliwa waishi mbinguni ili watawale wakiwa wafalme pamoja na Kristo. (2 Wakorintho 5:1; Ufunuo 5:​9, 10) Biblia inasema huu ndio “ufufuo wa kwanza” na pia inauita “ufufuo wa mapema,” na hilo linaonyesha kuna ufufuo mwingine utakaofuata. (Ufunuo 20:6; Wafilipi 3:​11) Watu watakaofufuliwa katika ufufuo huo wa pili wataishi duniani, na watu wengi sana watafaidika kutokana na ufufuo huo.​—Zaburi 37:29.

 Watu watafufuliwaje? Mungu amempa Yesu nguvu za kuwafufua wafu. (Yohana 11:25) Yesu atawafufua “wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho,” kila mmoja wao akiwa na sura yake, utu wake, na kumbukumbu lake. (Yohana 5:28, 29) Wale watakaofufuliwa waishi mbinguni watapata mwili wa roho, na watakaofufuliwa waishi duniani watapata mwili wa nyama ulio na afya nzuri kabisa.​—Isaya 33:24; 35:5, 6; 1 Wakorintho 15:42-44, 50.

 Ni nani watakaofufuliwa? Biblia inasema kwamba “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Waadilifu watatia ndani watu waaminifu, kama vile Noa, Sara, na Abrahamu. (Mwanzo 6:9; Waebrania 11:11; Yakobo 2:​21) Wasio waadilifu watatia ndani wale waliokosa kufikia viwango vya Mungu lakini hawakuwa na nafasi ya kujifunza viwango hivyo na kuvifuata.

 Hata hivyo, wale ambao ni waovu sana hivi kwamba hawawezi kubadilika hawatafufuliwa. Watu hao wanapokufa, wanakufa kifo cha kudumu bila tumaini la kuwa hai tena.​—Mathayo 23:33; Waebrania 10:26, 27.

 Ufufuo utatukia lini? Biblia ilitabiri kwamba ufufuo wa watu watakaoishi mbinguni utatukia wakati wa kuwapo kwa Kristo, ambao ulianza mwaka wa 1914. (1 Wakorintho 15:21-​23) Ufufuo wa watu watakaoishi duniani utatukia wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo, wakati ambapo dunia itageuzwa kuwa paradiso.​—Luka 23:43; Ufunuo 20:​6, 12, 13.

 Kwa nini ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba kutakuwa na ufufuo? Biblia ina masimulizi tisa ya watu waliofufuliwa, na kila simulizi linathibitishwa na mashahidi. (1 Wafalme 17:17-​24; 2 Wafalme 4:​32-​37; 13:20, 21; Luka 7:​11-​17; 8:​40-​56; Yohana 11:38-​44; Matendo 9:​36-​42; Matendo 20:​7-​12; 1 Wakorintho 15:​3-6) Tukio lenye kutokeza zaidi ni lile lililotukia Yesu alipomfufua Lazaro, kwani Lazaro alikuwa amekufa kwa siku nne na Yesu alifanya muujiza huo mbele ya umati wa watu. (Yohana 11:39, 42) Hata wale waliokuwa wakimpinga Yesu hawangeweza kupinga ukweli wa jambo hilo, kwa hiyo wakapanga kumwua Yesu pamoja na Lazaro.​—Yohana 11:47, 53; 12:​9-​11.

 Biblia inaonyesha kwamba Mungu ana uwezo na tamaa ya kuwafufua wafu. Katika kumbukumbu lake lisilo na mipaka ameweka rekodi yenye mambo mengi ya kila mtu ambaye atamfufua kwa nguvu zake zisizo na kifani. (Ayubu 37:23; Mathayo 10:30; Luka 20:37, 38) Mungu anaweza kuwafufua wafu, naye anataka kufanya hivyo! Ikifafanua kuhusu ufufuo utakaotukia hivi karibuni, Biblia inasema hivi kumhusu Mungu: “Utaitamani sana kazi ya mikono yako.”​—Ayubu 14:15.

Mambo yanayoeleweka kimakosa kuhusu ufufuo

 Uwongo: Ufufuo ni kuunganishwa tena kwa nafsi na mwili.

 Ukweli: Biblia inafundisha kwamba nafsi ni mtu mwenyewe, si sehemu fulani inayoendelea kuishi baada ya kifo. (Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4) Mtu ambaye amefufuliwa hajaunganishwa na nafsi yake; ameumbwa upya akiwa nafsi hai.

 Uwongo: Watu fulani wanafufuliwa kisha wanaharibiwa mara moja.

 Ukweli: Biblia inasema kwamba “wale waliokuwa na zoea la kutenda mambo maovu” watapata “ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:​29) Hata hivyo, watahukumiwa kwa kutegemea kile wanachofanya baada ya kufufuliwa, si kabla. Yesu alisema: “Wafu wataisikia sauti ya Mwana wa Mungu na wale ambao wamesikiliza wataishi.” (Yohana 5:​25) Majina ya wale ‘wanaosikiliza,’ au kutii mambo wanayojifunza baada ya kufufuliwa, yataandikwa katika “kitabu cha uzima.”​—Ufunuo 20:12, 13.

 Uwongo: Mtu anapofufuliwa, yeye hupokea mwili uleule aliokuwa nao kabla ya kufa.

 Ukweli: Baada ya kufa, inaelekea kwamba mwili wa mtu huvunjikavunjika.​—Mhubiri 3:​19, 20.