Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uliwahi Kuishi Katika Mwili Mwingine?

Je, Uliwahi Kuishi Katika Mwili Mwingine?

“Kuishi tena ni jambo hakika, na ni kweli kwamba watu walio hai wanatokana na watu waliokufa na nafsi za watu waliokufa zinaendelea kuishi.”​—PLATO, MWANAFALSAFA MGIRIKI, KARNE YA 5 K.W.K., AKIMNUKUU “SOKRATESI.”

“Kwa sababu nafsi inahitaji mwili ili iishi na bado si mwili, inaweza kuwa ndani ya mwili mmoja au mwingine, na inaweza kupitishwa kutoka kwa mwili mmoja hadi mwingine.”​—GIORDANO BRUNO, MWANAFALSAFA MWITALIANO, KARNE YA 16 W.K.

“Hakuna kitu kinachokufa: watu huonekana ni kana kwamba wamekufa . . . kisha wanaanza kuona mambo ni kana kwamba wanatazama kupitia dirisha, wakiwa salama ndani ya mwili mwingine.”​—RALPH WALDO EMERSON, MWANDISHI NA MSHAIRI KUTOKA MAREKANI, KARNE YA 19 W.K.

JE, UMEWAHI kujiuliza wewe ni nani hasa? Je, umewahi kuwazia kwamba uliwahi kuishi katika mwili mwingine? Ikiwa ndivyo, basi si wewe peke yako umewahi kuwa na maswali hayo. Tangu zamani, watu kutoka tamaduni mbalimbali wamekuwa wakijiuliza maswali hayo. Watu fulani wanapoendelea kutafuta majibu, huanza kuamini fundisho la kuzaliwa katika mwili mwingine. Fundisho hilo linadai kwamba mtu anapokufa, “nafsi” fulani ambayo haiwezi kuonekana inatoka ndani ya mwili na kuzaliwa katika mwili mwingine​—wa mwanadamu, mnyama, au hata mmea—​mara moja ua mara kadhaa mfululizo.

Ingawa watu fulani wanaamini fundisho hilo, tunawezaje kujua kama ni la kweli? Neno la Mungu Biblia linasema nini kuhusu fundisho hilo? Hata hivyo, kwanza tunahitaji kujiuliza, Fundisho hilo lilitoka wapi?

Fundisho la Watu Kuzaliwa Katika Mwili Mwingine Lilianzaje?

Kulingana na wanahistoria na wasomi fulani, wakazi wa Babiloni la kale, jiji lilikuwapo mwishoni mwa milenia ya tatu K.W.K., walianza kuamini kwamba nafsi ya mwanadamu haiwezi kufa. Tatizo la fundisho la kutokufa kwa nafsi ni kwamba “wanatheolojia Wababiloni walikisia kisia jambo hilo,” anasema Morris Jastrow, Jr., katika kitabu chake The Religion of Babylonia and Assyria. Kwa Wababiloni, “kifo kilikuwa njia ya kuingia katika aina tofauti ya uhai,” anaeleza. “Ndiyo sababu, hawakuamini wazo la kwamba mtu anaweza kufa kabisa.”

Kuanzia mwanzo huo huko Babiloni, fundisho hilo la nafsi kutoka kwa mwili uliokufa na kuingia katika mwili unaozaliwa lilianza kuenea katika sehemu nyingine za dunia. Wanafalsafa wa India walianzisha fundisho lingine ambalo linaonyesha kwa undani kwamba maisha ambayo mtu aliishi yangeamua mwili ambao angezaliwa tena. Pia, wanafalsafa Wagiriki waliokuwa na ushawishi mkubwa, walianza kuamini fundisho hilo la nafsi kutoka na kuingia katika mwili mwingine, na kwa sababu hiyo watu wengi wakaanza kuamini.

Wakati wetu pia, watu wengi wamekuwa wakivutiwa na fundisho hilo katika nchi za Magharibi. Watu mashuhuri na vijana, wamekuwa wakifurahishwa na mawazo na desturi za dini za Mashariki. Leo kuna vitabu vingi na vituo vya Intaneti ambavyo vinazungumzia maana ya mambo ambayo watu wanadhania walifanya katika maisha yao yaliyopita. Katika nchi nyingi watu wameanza kuamini kwa wingi yale yanayodaiwa kuwa matibabu ya maisha yaliyopita. Matibabu hayo yanahusisha kupumbaza akili ili kuchunguza yale yanayodaiwa kuwa maisha yaliyopita kwa kusudi la kuelewa afya na tabia ya sasa ya mtu.

Je, Fundisho la Kuzaliwa Katika Mwili Mwingine Ni la Kweli?

Hata ingawa fundisho la kuzaliwa katika mwili mwingine lilianza zamani, bado tunahitaji kupata jibu la swali muhimu kabisa—Je, fundisho hilo ni la kweli? Na Wakristo wangependa kujua ikiwa fundisho hilo linapatana na Biblia. (Yohana 17:17) Kwa kuwa Muumba wetu, Yehova Mungu, ndiye Chanzo cha uhai na “Mfunuaji wa siri,” anafunua mambo yanayohusu uhai na kifo ambayo wanadamu hawajui. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Neno lake, Biblia, linaweza kutupa majibu ya fundisho hilo.​—Danieli 2:28; Matendo 17:28.

Tunapojifunza Biblia kwa makini, tutapata majibu ya Mungu kuhusu kinachotupata tunapokufa. Kwa mfano, katika Mwanzo 3:19, tunapata maneno ambayo Mungu alimwambia Adamu baada ya Adamu na Hawa kumwasi. Mungu alisema: “Kwa jasho la uso wako utakula mkate mpaka utakaporudi katika udongo, kwa kuwa ulitolewa katika huo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” Adamu aliumbwa kutokana na mavumbi. Alipokufa, alirudi mavumbini. Hayo ndiyo maneno ya Mungu yaliyo wazi kabisa. Hivyo, mtu anapokufa hazaliwi katika mwili mwingine bali hukoma kuwapo. * Kama tu joto lilivyo kinyume cha baridi, mvua ilivyo kinyume cha ukame, na mwangaza ulivyo kinyume cha giza, ndivyo kifo kilivyo kinyume cha uhai. Watu waliokufa wamekufa kabisa! Bila shaka jambo hilo ni rahisi na linapatana na akili.

Basi lazima kuna sababu inayofanya watu wakumbuke mambo yanayodaiwa yalitukia katika maisha yao yaliyopita. Kufikia leo, bado hakuna mtu anayeelewa vizuri jinsi akili ya mwanadamu inavyofanya kazi, kutia ndani hali ya kupoteza fahamu, na athari za dawa na hali zenye kuhangaisha au kufadhaisha. Ndoto na matukio ya kuwaziwa yanayotegemea habari nyingi zinazohifadhiwa katika kumbukumbu ya akili yanaweza kukumbukwa vizuri hivi kwamba yakaonekana kuwa ya kweli. Katika hali fulani, roho waovu wanatokeza mawazo ya kiuchawi ambayo yanaweza kufanya mambo yasiyo ya kweli yaonekane kuwa ya kweli.​—1 Samweli 28:7-19.

Ni jambo la kawaida kwa wanadamu kutaka kuishi na kujua kuhusu wakati wao ujao. Lakini tamaa hiyo ilitoka wapi? Jambo la kupendeza ni kwamba Biblia inasema hivi kumhusu Muumba: “Ameweka milele ndani ya mioyo yao.” (Mhubiri 3:11, Zaire Swahili Bible) Hivyo, wanadamu wanatamani kutoka moyoni kuishi milele.

Ikiwa Muumba wetu, Yehova Mungu, ameweka tamaa ya kuishi milele katika mioyo ya wanadamu, basi ni jambo linalopatana na akili atueleze jinsi tamaa hiyo inavyoweza kutimizwa. Biblia inafunua kwamba kusudi kuu la Muumba wetu ni kuwabariki wanadamu waaminifu kwa kuwapa uzima wa milele katika dunia paradiso. “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake,” akasema mwandishi wa zaburi, Mfalme Daudi, aliyeongozwa na roho ya Mungu. (Zaburi 37:29) Fundisho lingine kuu katika Biblia ambalo linahusianishwa na kusudi la Mungu la kuishi milele ni ufufuo wa wafu.​—Matendo 24:15; 1 Wakorintho 15:16-19.

Ufufuo​—Tumaini Lililothibitishwa kwa Ajili ya Wafu

Biblia ina masimulizi manane kuhusu watu waliojionea wafu wakifufuliwa hapa duniani. * Masimulizi hayo yanataja watu hao walifufuliwa wala si kubadilika na kuwa na mwili mwingine. Watu wa ukoo na marafiki waliwatambua watu wao waliofufuliwa. Watu hao wa ukoo hawakuhitaji kutafuta kati ya watoto waliokuwa wamezaliwa hapo karibu na kuchagua yupi kati yao alikuwa na nafsi ya mtu wao aliyekuwa amekufa.​—Yohana 11:43-45.

Jambo lenye kufariji ni kwamba Neno la Mungu linaonyesha kuwa watu wengi ambao wamekufa watafufuliwa wakati Mungu atakapowafufua watu katika ulimwengu mpya, ambao hivi karibuni utachukua mahali pa ulimwengu huu mwovu. (2 Petro 3:13, 14) Wakati huu, mtindo wa maisha wa mabilioni ya watu umehifadhiwa katika kumbukumbu kamilifu la Yehova ambalo halina kipimo, Mungu ambaye anakumbuka majina ya nyota zote! (Zaburi 147:4; Ufunuo 20:13) Atakapomaliza kuwarudishia watu wengi uhai katika ulimwengu mpya, watakuwa na uwezo wa kufuatilia ukoo wao na kutambua mababu zao. Hilo ni tumaini lenye kuvutia kama nini!

^ fu. 13 Ili upate habari zaidi, ona sura ya 6, yenye kichwa “Wafu Wako Wapi?” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 18 Masimulizi hayo manane yanapatikana katika 1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37; 13:20, 21; Luka 7:11-17; 8:40-56; Yohana 11:38-44; Matendo 9:36-42; 20:7-12. Unaposoma masimulizi hayo, ona jinsi ufufuo huo ulivyofanywa mbele ya watu wengi waliojionea. Simulizi la tisa linaeleza kuhusu kufufuliwa kwa Yesu Kristo.​—Yohana 20:1-18.