Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Uhuru wa Kuchagua? Je, Mungu Ndiye Anayeamua Mapema?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Uhuru wa Kuchagua? Je, Mungu Ndiye Anayeamua Mapema?

Jibu la Biblia

 Mungu anatuheshimu sana kwa kutupa uhuru wa kuchagua, uwezo wa kujifanyia maamuzi yetu wenyewe badala ya Mungu au majaliwa kuamua mambo tunayofanya. Fikiria mambo ambayo Biblia inafundisha.

  •   Mungu aliwaumba wanadamu kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26) Tofauti na wanyama, ambao huongozwa na silika, wanadamu tunafanana na Muumba kwa sababu tunaweza kuonyesha sifa kama vile upendo na haki. Na kama vile Muumba wetu, tuna uhuru wa kuchagua.

  •   Kwa kadiri kubwa, tunaweza kuamua jinsi wakati wetu ujao utakavyokuwa. Biblia inatutia moyo ‘tuchague uzima . . . kwa kuisikiliza sauti ya [Mungu],’ yaani, kwa kuchagua kutii amri zake. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Ahadi hiyo ingekuwa haina maana, tena ya kikatili, ikiwa hatungekuwa na uhuru wa kuchagua. Badala ya kutulazimisha tufanye mambo anayosema, Mungu anatusihi hivi kwa upendo: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto.”—Isaya 48:18.

  •   Kufanikiwa au kutofanikiwa kwetu maishani hakujaamuliwa mapema. Ikiwa tunataka kufanikiwa katika jambo fulani, ni lazima tulifanye kwa bidii. Biblia inasema hivi: “Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote.” (Mhubiri 9:10) Pia inasema: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.”—Methali 21:5.

 Uhuru wa kuchagua ni zawadi ya thamani sana kutoka kwa Mungu, kwa sababu unatupa nafasi ya kumpenda Mungu kwa “moyo wote”—kwa sababu tunataka kufanya hivyo.—Mathayo 22:37.

Je, Mungu anadhibiti mambo yote?

 Biblia inafundisha kwamba Mungu ni mweza yote, na kwamba nguvu zake haziwezi kuzuiwa na mtu yeyote isipokuwa yeye mwenyewe. (Ayubu 37:23; Isaya 40:26) Hata hivyo, hatumii nguvu zake ili kuongoza kila kitu. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba Mungu aliendelea “kujizuia” dhidi ya Babiloni la kale, jiji lililokuwa na uadui na watu wake. (Isaya 42:14) Vivyo hivyo, wakati wetu leo, anachagua kuwavumilia wale wanaotumia uhuru wao wa kuchagua vibaya kwa kuwaumiza wengine. Hata hivyo Mungu hatavumilia hivyo milele.—Zaburi 37:10, 11.