Hamia kwenye habari

Je, Wakati Wetu wa Kufa Umeamuliwa Mapema?

Je, Wakati Wetu wa Kufa Umeamuliwa Mapema?

Jibu la Biblia

 Hapana, wakati wetu wa kufa haujaamuliwa mapema. Badala ya kuunga mkono imani ya kwamba maisha ya mwanadamu yameamuliwa mapema, Biblia inasema kwamba mara nyingi kifo husababishwa na ‘matukio yasiyotazamiwa.’​—Mhubiri 9:​11.

Je, Biblia haisemi kwamba kuna “wakati wa kufa”?

 Ndiyo, Mhubiri 3:2 inasema kwamba kuna “wakati wa kuzaliwa, na wakati wa kufa; wakati wa kupanda, na wakati wa kung’oa kilichopandwa.” Hata hivyo, muktadha wa mstari huu unaonyesha kwamba Biblia inazungumzia mambo ya kawaida yanayotukia katika maisha ya mwanadamu. (Mhubiri 3:​1-8) Mungu hajaweka wakati hususa wa mtu kufa kama tu ambavyo hamlazimishi mkulima kuanza kupanda wakati fulani hususa. Jambo linalokaziwa ni kwamba hatupaswi kukazia fikira mambo yasiyo ya maana hivi kwamba tunampuuza Muumba wetu.​—Mhubiri 3:​11; 12:​1, 13.

Uhai unaweza kurefushwa

 Licha ya hali zisizotarajiwa maishani, kwa kawaida tunaweza kuishi muda mrefu tukifanya maamuzi ya hekima. Biblia inasema: “Sheria ya mwenye hekima ni chemchemi ya uzima, ili kumwepusha mtu na mitego ya kifo.” (Methali 13:14) Pia, Musa aliwaambia Waisraeli kwamba wangeweza ‘kufurahia maisha marefu’ ikiwa wangetii amri za Mungu. (Kumbukumbu la Torati 6:2, Neno—Biblia Takatifu) Tofauti na hilo, tunaweza kufupisha uhai wetu kwa kutenda isivyofaa au kipumbavu.​—Mhubiri 7:​17.

 Hata hivyo, hatuwezi kuepuka kifo kwa sababu tu ya kuwa na hekima au kuwa waangalifu. (Waroma 5:​12) Lakini, hali hii itabadilika, kwa sababu Biblia inaahidi kwamba kuna wakati ambapo “kifo hakitakuwapo tena.”​—Ufunuo 21:4.